Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 107

Mfalme Awaita Wale Walioalikwa Kwenye Karamu ya Ndoa

Mfalme Awaita Wale Walioalikwa Kwenye Karamu ya Ndoa

MATHAYO 22:1-14

  • MFANO WA KARAMU YA NDOA

Huduma ya Yesu inapokaribia kwisha, anaendelea kutumia mifano ili kufunua uovu wa waandishi na wakuu wa makuhani. Basi, wanataka kumuua. (Luka 20:19) Lakini bado Yesu hajamaliza kufunua uovu wao. Anasimulia mfano mwingine.

“Ufalme wa mbinguni ni kama mfalme aliyemwandalia mwanawe karamu ya ndoa. Akawatuma watumwa wake wawaite wale walioalikwa kwenye karamu ya ndoa, lakini hawakutaka kuja.” (Mathayo 22:2, 3) Yesu anaanza mfano huo kwa kutaja “Ufalme wa mbinguni.” Basi, kwa hakika “mfalme” ni Yehova Mungu. Namna gani mwana wa mfalme na wale walioalikwa kwenye karamu ya ndoa? Pia, si vigumu kutambua kwamba mwana wa mfalme ni Mwana wa Yehova ambaye yuko hapo akisimulia mfano huo, na pia kuelewa kwamba wale walioalikwa ndio watakaokuwa pamoja na Mwana katika Ufalme wa mbinguni.

Ni nani wanaoalikwa kwanza? Yesu na mitume wamekuwa wakiwahubiria nani kuhusu Ufalme? Wamewahubiria Wayahudi. (Mathayo 10:6, 7; 15:24) Taifa hilo lilikubali agano la Sheria mwaka wa 1513 K.W.K., na hivyo kupata nafasi ya kwanza ya kutokeza “ufalme wa makuhani.” (Kutoka 19:5-8) Lakini ni wakati gani hasa ambapo wangealikwa kwenye “karamu ya ndoa”? Inapatana na akili kwamba mwaliko huo ulitolewa mwaka wa 29 W.K., Yesu alipoanza kuhubiri kuhusu Ufalme wa mbinguni.

Waisraeli wengi waliitikiaje mwaliko huo? Kama Yesu alivyosema, “hawakutaka kuja.” Idadi kubwa ya viongozi wa kidini na watu hawakukubali kwamba Yesu ndiye Masihi na Mfalme aliyechaguliwa na Mungu.

Hata hivyo, Yesu anaonyesha kwamba Wayahudi wangepewa nafasi nyingine: “Tena [mfalme] akawatuma watumwa wengine, akasema, ‘Waambieni wale walioalikwa: “Tazameni! Nimetayarisha chakula changu cha mchana, ng’ombe dume wangu na wanyama waliononeshwa wamechinjwa, na vitu vyote viko tayari. Njooni kwenye karamu ya ndoa.”’ Lakini wakapuuza na kwenda zao, wengine kwenye mashamba yao, na wengine kwenye biashara zao; lakini wengine wakawakamata wale watumwa wakawatendea kwa dharau na kuwaua.” (Mathayo 22:4-6) Hilo linapatana na jambo ambalo lingetokea baada ya kutaniko la Kikristo kuanzishwa. Wakati huo bado Wayahudi walikuwa na nafasi ya kuwa katika Ufalme. Hata hivyo, wengi walikataa mwaliko huo hata wakawatendea vibaya ‘watumwa wa mfalme.’​—Matendo 4:13-18; 7:54, 58.

Taifa hilo litapatwa na matokeo gani? Yesu anasimulia hivi: “Mfalme akakasirika sana, akatuma majeshi yake yakawaue wauaji hao na kulichoma jiji lao.” (Mathayo 22: 7) Wayahudi walipatwa na jambo hilo mwaka wa 70 W.K. Waroma walipoharibu “jiji lao,” Yerusalemu.

Wanapokataa mwaliko wa mfalme, je, inamaanisha kwamba hakuna watu wengine watakaoalikwa? Mfano wa Yesu hauonyeshi hivyo. Anaendelea kusema hivi: “Kisha [mfalme] akawaambia watumwa wake, ‘Karamu ya ndoa iko tayari, lakini walioalikwa hawakustahili. Kwa hiyo, nendeni kwenye barabara zinazotoka jijini, na kumwalika kwenye karamu ya ndoa mtu yeyote mtakayemwona.’ Basi watumwa wakaenda barabarani na kuwaalika wote waliowaona, waovu na wema; na chumba cha sherehe za harusi kikajaa wageni.”—Mathayo 22:8-10.

Kwa kupatana na jambo hilo, baadaye mtume Petro angeanza kuwasaidia Watu wa Mataifa—watu ambao hawakuwa Wayahudi kwa kuzaliwa au kwa kugeuzwa imani—wawe Wakristo. Katika mwaka wa 36 W.K., ofisa wa jeshi Mroma, Kornelio na familia yake walipokea roho ya Mungu, na hivyo wakawa na tumaini la kuwa katika Ufalme wa Mbinguni ambao Yesu alitaja.—Matendo 10:1, 34-48.

Yesu anaonyesha kwamba si wote wanaokuja kwenye karamu ambao mwishowe watakubalika mbele za “mfalme.” Anasema: “Mfalme alipoingia kuwakagua wageni, akamwona mtu ambaye hakuwa amevaa vazi la ndoa. Basi akamuuliza, ‘Mwenzangu, umeingiaje humu bila vazi la ndoa?’ Akakosa la kusema. Ndipo mfalme akawaambia watumishi wake, ‘Mfungeni mikono na miguu, kisha mmtupe nje gizani. Huko ndiko atalia na kusaga meno yake.’ Kwa maana kuna wengi walioalikwa, lakini waliochaguliwa ni wachache.”—Mathayo 22:11-14.

Huenda viongozi wa kidini wanaomsikiliza Yesu wasielewe maana au matokeo ya mambo anayosema. Hata hivyo, wanakasirika na kuazimia hata zaidi kumuua mtu anayewaaibisha hivyo.