Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 107

Mufalme Anaita Wenye Walialikwa Kwenye Karamu ya Ndoa

Mufalme Anaita Wenye Walialikwa Kwenye Karamu ya Ndoa

MATAYO 22:1-14

  • MUFANO WA KARAMU YA NDOA

Utumishi wa Yesu unakuwa karibu na kufika mwisho. Anaendelea kutumia mifano ili kuonyesha waziwazi tabia za waandishi na wakubwa wa makuhani. Kwa hiyo, wanataka kumuua. (Luka 20:19) Lakini Yesu anaendelea kufunua tabia zao. Anatoa mufano mwengine:

“Ufalme wa mbinguni unaweza kufananishwa na mufalme mwenye alifanyia mwana wake karamu ya ndoa. Na akatuma watumwa wake waite wale wenye walialikwa kwenye karamu ya ndoa, lakini hawakutaka kuja.” (Matayo 22:2, 3) Yesu anaanza mufano wake kwa kutaja “Ufalme wa mbinguni.” Bila shaka, “mufalme” anapaswa kuwa Yehova Mungu. Mwana wa mufalme na wale wenye kualikwa kwenye karamu ya ndoa ni nani? Hapo pia, haiko nguvu kutambua kwamba mwana wa mufalme ni Yesu, na wale wenye walialikwa ni wale wenye watakuwa pamoja na Mwana katika Ufalme wa mbinguni.

Ni nani wenye wanaalikwa wa kwanza? Yesu na mitume wamekuwa wakihubiria nani juu ya Ufalme? Wayahudi. (Matayo 10:6, 7; 15:24) Walikubali agano la Sheria katika mwaka wa 1513 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, na wakakuwa wa kwanza kupata nafasi ya kufanyiza “ufalme wa makuhani.” (Kutoka 19:5-8) Lakini, ni wakati gani wangeitwa kwenye “karamu ya ndoa”? Kwa kweli, mualiko huo ulianza katika mwaka wa 29 wakati wetu, wakati Yesu alianza kuhubiri juu ya Ufalme wa mbinguni.

Waisraeli wengi waliitikia mualiko huo namna gani? Kama vile Yesu alisema, “hawakutaka kuja.” Viongozi wengi wa dini na watu hawakukubali kama yeye ni Masiya na Mufalme mwenye aliwekwa na Mungu.

Kwa hiyo, Yesu alionyesha kwamba Wayahudi walipewa nafasi ingine: “Tena [mufalme] akatuma watumwa wengine, na kusema, ‘Muambie wale wenye walialikwa: “Muangalie! Nimetayarisha chakula changu cha muchana, ngombe-dume wangu na wanyama wenye kunona wamechinjwa, na kila kitu kiko tayari. Mukuje kwenye karamu ya ndoa.”’ Lakini kwa sababu hawakuhangaika, wakaenda, mumoja kwenye shamba lake mwenyewe, na mwingine kwenye biashara yake; lakini wengine wakakamata watumwa wake, wakawatendea kwa zarau na kuwaua.” (Matayo 22:4-6) Hilo linapatana na mambo yenye yangefanyika kisha tu kuanzishwa kwa kutaniko la Kikristo. Wakati huo, Wayahudi walikuwa wangali na nafasi ya kuwa katika Ufalme, lakini wengi walikataa mualiko huo, na hata kuwatendea mubaya ‘watumwa wa mufalme.’—Matendo 4:13-18; 7:54, 58.

Taifa hilo lilipatwa na nini? Yesu anaeleza: “Mufalme akakasirika sana, akatuma majeshi yake na kuua wale wauaji na kuchoma muji wao.” (Matayo 22:7) Wayahudi walipata matokeo hayo mabaya katika mwaka wa 70 kisha kuzaliwa kwa Yesu, wakati Waroma waliharibu “muji wao,” Yerusalemu.

Ni kusema kama hakuna mwengine mwenye angealikwa kwa sababu wao walikataa mualiko wa mufalme? Hapana, kulingana na mufano wa Yesu. Anaendelea kusema: “Kisha akaambia watumwa wake, ‘Karamu ya ndoa iko tayari, lakini wale wenye walialikwa hawakustahili. Kwa hiyo, muende kwenye barabara zenye kupeleka inje ya muji, na mualike kwenye karamu ya ndoa mutu yeyote mwenye mutapata.’ Basi watumwa hao wakaenda kwenye barabara na kukusanya wote wenye walipata, watu waovu na watu wazuri; na chumba cha karamu za ndoa kikajaa watu wenye kula chakula.”—Matayo 22:8-10.

Maneno hayo yalitimia wakati mutume Petro alisaidia watu wa mataifa, ni kusema, watu wenye hawakuwa Wayahudi kwa kuzaliwa ao kwa kugeuzwa imani, ili wakuwe Wakristo wa kweli. Katika mwaka wa 36 kisha kuzaliwa kwa Yesu, mukubwa wa jeshi Muroma Kornelio na familia yake walipokea roho ya Mungu, na kupata tumaini la kuwa sehemu ya ufalme wa mbinguni wenye Yesu alizungumuzia.—Matendo 10:1, 34-48.

Yesu anaonyesha kama haiko wote wenye kuja kwenye karamu ndio mwishowe watakubaliwa na “mufalme.” Anasema: “Wakati mufalme aliingia ili kuchunguza wageni, akaona mutu mwenye hakukuwa anavaa nguo ya ndoa. Basi akamuuliza, ‘Mwenzangu, uliingia humu namna gani bila nguo ya ndoa?’ Akakosa la kusema. Halafu mufalme akaambia watumishi wake, ‘Mumufunge mikono na miguu, kisha mumutupe inje katika giza. Ni kule atalia na kusaga meno yake.’ Kwa maana wenye walialikwa ni wengi, lakini wenye walichaguliwa ni wachache.”—Matayo 22:11-14.

Pengine viongozi wa dini hawaelewe maana ao mambo yote yenye iko anazungumuzia. Lakini, wanachukizwa na wanaazimia hata zaidi kuondolea mbali mutu mwenye kuwapatisha haya hivyo.