Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 111

Mitume Waomba Ishara

Mitume Waomba Ishara

MATHAYO 24:3-51 MARKO 13:3-37 LUKA 21:7-38

  • WANAFUNZI WANNE WAOMBA ISHARA

  • UTIMIZO KATIKA KARNE YA KWANZA NA BAADAYE

  • TUNAPASWA KUENDELEA KUWA MACHO

Ni siku ya Jumanne mchana, na Nisani 11 inakaribia kwisha. Pia, ni mwisho wa siku zenye shughuli nyingi kwa Yesu hapa duniani. Mchana amekuwa akifundisha hekaluni, na usiku amekuwa akilala nje ya jiji. Watu wanapendezwa sana naye, hivi kwamba wamekuwa “wakija hekaluni asubuhi na mapema ili wamsikilize.” (Luka 21:37, 38) Sasa hayo yamepita, naye Yesu amekaa kwenye Mlima wa Mizeituni na wanafunzi wake wanne—Petro, Andrea, Yakobo na Yohana.

Wanafunzi hao wanne wamekuja kuongea naye faraghani. Wanahangaikia hekalu kwa kuwa Yesu ametoka kutabiri kwamba hakuna jiwe la hekalu litakaloachwa juu ya jiwe lingine. Hata hivyo, pia wanafikiria mambo mengine. Hapo awali, Yesu aliwahimiza hivi: “Endeleeni kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja saa msiyotazamia.” (Luka 12:40) Pia, alikuwa amezungumzia “siku ambayo Mwana wa binadamu atafunuliwa.” (Luka 17:30) Je, maelezo hayo yanahusiana kwa vyovyote na mambo ambayo ametoka tu kusema kuhusu hekalu? Mitume wanataka kujua mengi zaidi. Wanamuuliza: “Tuambie, mambo haya yatatukia lini, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—Mathayo 24:3.

Huenda wanafikiria kuhusu kuharibiwa kwa hekalu wanaloliona. Pia, wanauliza kuhusu kuwapo kwa Mwana wa binadamu. Labda wanakumbuka kwamba Yesu alitoa mfano kuhusu “mtu fulani wa familia mashuhuri” ambaye ‘alisafiri ili akapokee mamlaka ya kifalme kisha arudi.’ (Luka 19:11, 12) Na mwishowe wanajiuliza “umalizio wa mfumo wa mambo” utahusisha nini.

Katika majibu yake, Yesu anatoa ishara inayoonyesha wakati ambao mfumo wa Kiyahudi uliopo, kutia ndani hekalu lake utakoma. Hata hivyo, anazungumzia mengi zaidi. Ishara hiyo itawasaidia Wakristo wakati ujao kujua ikiwa wanaishi wakati wa “kuwapo” kwake na karibu na mwisho wa mfumo mzima wa mambo duniani.

Kadiri miaka inavyopita, mitume wanaona unabii wa Yesu ukitimizwa. Naam, mambo mengi aliyotabiri yanaanza kutukia wakiwa hai. Hivyo, Wakristo walio macho wanaoishi miaka 37 baadaye, mwaka wa 70 W.K., wamejiandaa na wako tayari kwa ajili ya uharibifu unaokaribia wa mfumo wa Kiyahudi na hekalu lake. Hata hivyo, si mambo yote ambayo Yesu anatabiri yanatukia kabla na baada ya mwaka wa 70 W.K. Hivyo basi, ni nini kitakachoonyesha kuwapo kwake katika utawala wa Kifalme? Yesu anawafunulia mitume wake jibu.

Yesu anatabiri kwamba kutakuwa na “vita na habari za vita” na kwamba “taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:6, 7) Pia, anasema kwamba “kutakuwa na matetemeko makubwa ya ardhi, na magonjwa na upungufu wa chakula katika sehemu mbalimbali.” (Luka 21:11) Yesu anawaonya hivi wanafunzi wake: “Watu watawakamata ninyi na kuwatesa.” (Luka 21:12) Manabii wa uwongo watatokea na kuwapotosha wengi. Uasi sheria utaongezeka na upendo wa wengi utapoa. Pia, anasema kwamba “habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Ingawa unabii wa Yesu ulitimizwa kwa kadiri fulani kabla na wakati Yerusalemu lilipoharibiwa na Waroma, je, huenda Yesu alikuwa akizungumzia utimizo mkubwa zaidi baadaye? Je, unaona uthibitisho kwamba unabii muhimu wa Yesu umekuwa ukitimizwa kwa kiwango kikubwa katika nyakati zetu?

Jambo moja ambalo Yesu anataja katika ishara ya kuwapo kwake ni kuonekana kwa “kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa.” (Mathayo 24:15) Mwaka wa 66 W.K., kitu hicho chenye kuchukiza kilikuwa “majeshi yaliyopiga kambi” ya Roma, yakiwa na sanamu zao. Waroma walizunguka Yerusalemu na kuvunja baadhi ya kuta zake. (Luka 21:20) Hivyo, “kitu chenye kuchukiza” kilisimama mahali ambapo hakikupaswa kusimama, mahali ambapo Wayahudi walipaona kuwa “patakatifu.”

Pia, Yesu anatabiri hivi: “Kutakuwa na dhiki kuu ambayo haijawahi kutokea tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatokea tena.” Katika mwaka wa 70 W.K., Waroma wanaliharibu Yerusalemu. Kuharibiwa kwa ‘jiji takatifu’ la Wayahudi, kutia ndani hekalu lake kunathibitika kuwa dhiki kuu, na watu wengi sana wanauawa. (Mathayo 4:5; 24:21) Ni uharibifu mkubwa zaidi kuliko uharibifu wowote ambao jiji hilo na Wayahudi wote wamewahi kushuhudia, nao unakomesha mfumo wote wa ibada ambao umefuatwa na Wayahudi kwa miaka mingi. Kwa hiyo, baadaye, utimizo wowote mkubwa wa unabii wa Yesu utakuwa wenye kuogopesha kwelikweli.

UHAKIKA KATIKA SIKU ZILIZOTABIRIWA

Mazungumzo ya Yesu na mitume wake kuhusu ishara ya kuwapo kwake katika utawala wa Ufalme na mwisho wa mfumo wa mambo hayajamalizika. Sasa anawaonya kuhusu kuwafuata “Kristo wengi wa uwongo na manabii wa uwongo.” Anasema watajaribu, “kuwapotosha, ikiwezekana, hata wale waliochaguliwa.” (Mathayo 24:24) Lakini wachaguliwa hao hawatapotoshwa. Kristo wa uwongo wanaweza kuonekana kwa macho. Tofauti na hilo, kuwapo kwa Yesu hakutaonekana kwa macho.

Akizungumza kuhusu dhiki kubwa zaidi ambayo itatokea mwishoni mwa mfumo huu wa mambo, Yesu anasema: “Jua litatiwa giza, mwezi hautatoa nuru yake, nyota zitaanguka kutoka mbinguni, na nguvu za mbingu zitatikiswa.” (Mathayo 24:29) Mitume wanaosikiliza maneno hayo yanayoogopesha hawajui kikamili mambo yatakayotokea, lakini ni wazi kwamba yatakuwa yenye kushtua.

Matukio hayo yenye kushtua yatawaathirije wanadamu? Yesu anasema: “Watu watazimia kwa woga wakitarajia mambo yatakayotokea juu ya dunia inayokaliwa, kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa.” (Luka 21:26) Bila shaka, Yesu anafafanua kuhusu kipindi kigumu zaidi katika historia ya wanadamu.

Yesu anawatia moyo mitume wake anapowafunulia kwamba si watu wote watakaokuwa wakiomboleza ‘Mwana wa binadamu atakapokuja akiwa na nguvu na utukufu mwingi.’ (Mathayo 24:30) Tayari ametaja kwamba Mungu ataingilia kati “kwa sababu ya wale waliochaguliwa.” (Mathayo 24:22) Wanafunzi hao waaminifu wanapaswa kutendaje watakapoona mambo hayo yenye kushtua ambayo Yesu anazungumzia? Yesu anawatia moyo wafuasi wake hivi: “Mambo hayo yatakapoanza kutukia, simameni wima na kuinua vichwa vyenu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.”—Luka 21:28.

Hata hivyo, wanafunzi wa Yesu wanaoishi katika kipindi hicho kilichotabiriwa watatambuaje kwamba mwisho umekaribia? Yesu anawapa mfano wa mtini: “Mara tu matawi yake machanga yanapokuwa laini na kuchipua majani, mnajua kwamba kiangazi kinakaribia. Vivyo hivyo, ninyi pia mtakapoona mambo yote hayo, jueni kwamba yuko karibu milangoni. Kwa kweli ninawaambia kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo haya yote yatukie.”—Mathayo 24:32-34.

Kwa hiyo, wanafunzi wake wanapoona mambo mbalimbali ya ile ishara yakitimizwa, wanapaswa kutambua kwamba mwisho umekaribia. Akiwashauri wanafunzi ambao watakuwa hai wakati huo muhimu, Yesu anasema hivi:

“Kuhusu siku hiyo na saa hiyo, hakuna mtu anayejua, hata malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu. Kwa maana kama siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. Kwa maana kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya Gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina, nao hawakujali mpaka Gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mathayo 24:36-39) Tukio ambalo Yesu anatumia kama mfano—Gharika ya kihistoria ya siku za Noa—liliathiri dunia nzima.

Bila shaka, mitume wanaomsikiliza Yesu kwenye Mlima wa Mizeituni wanatambua umuhimu wa kuendelea kuwa macho. Yesu anasema: “Jiangalieni wenyewe ili mioyo yenu isilemewe kamwe na kula na kunywa kupita kiasi na mahangaiko ya maisha, na siku ile iwakute ghafla kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wale wote wanaoishi juu ya uso wa dunia. Basi, endeleeni kukesha sikuzote mkiomba dua ili mfanikiwe kuponyoka mambo yote hayo ambayo lazima yatukie, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.”—Luka 21:34-36.

Kwa mara nyingine tena, Yesu anawaonyesha kwamba mambo anayotabiri hayatatokea kwa kiwango kidogo. Hatabiri kuhusu matukio ambayo yatatokea miaka michache ijayo na yatakayoathiri jiji la Yerusalemu au taifa la Wayahudi peke yake. Hapana, anazungumzia mambo ambayo yatakuja “juu ya wale wote wanaoishi juu ya uso wa dunia.”

Anasema kwamba wanafunzi wake watahitaji kuendelea kuwa macho, kuendelea kukesha, na kuwa tayari. Yesu anakazia onyo hilo kwa mfano mwingine: “Jueni jambo hili: Ikiwa mwenye nyumba angejua mwizi atakuja katika kesha gani, angekaa macho na hangeruhusu nyumba yake ivunjwe. Kwa hiyo ninyi pia iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja saa msiyotazamia.”—Mathayo 24:43, 44.

Yesu anaendelea kuwapa wanafunzi wake sababu ya kuwa na tumaini. Anawahakikishia kwamba unabii wake utakapokuwa ukitimizwa, kutakuwa na “mtumwa” atakayekuwa macho na mwenye bidii. Yesu anazungumzia hali ambayo mitume wanaweza kuilewa kwa urahisi: “Kwa kweli ni nani mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi asimamie watumishi wake wa nyumbani na kuwapa chakula chao kwa wakati unaofaa? Mwenye furaha ni mtumwa huyo ikiwa bwana wake atakapokuja atamkuta akifanya hivyo! Kwa kweli ninawaambia, atamweka rasmi asimamie mali zake zote.” Hata hivyo, “mtumwa” huyo akikuza mtazamo mwovu na kuanza kuwatesa wengine, bwana wake “atamwadhibu kwa ukali sana.”—Mathayo 24:45-51; linganisha na Luka 12:45, 46.

Hata hivyo, Yesu hasemi kwamba kikundi cha wafuasi wake kitakuwa na mtazamo mwovu. Hivyo basi, Yesu anataka kuwafundisha wanafunzi wake somo gani? Anataka wawe macho na wenye bidii, kama anavyoonyesha tena katika mfano mwingine.