Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 112

Mufano wa Mabikira Kumi​—Somo Kuhusu Kukesha

Mufano wa Mabikira Kumi​—Somo Kuhusu Kukesha

MATAYO 25:1-13

  • YESU ANATOA MUFANO WA MABIKIRA KUMI

Yesu anaendelea kujibu ulizo la mitume wake kuhusu alama ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mupangilio wa mambo. Sasa, anawatolea shauri lenye hekima kupitia mufano mwengine. Wale wenye kuishi wakati wa kuwapo kwake wataona kutimizwa kwa mufano huo.

Anaanza mufano wake, kwa kusema: “Ufalme wa mbinguni unaweza kufananishwa na mabikira kumi (10) wenye walikamata taa zao na kuenda kumupokea bwana-arusi. Watano (5) kati yao walikuwa wapumbavu, na watano (5) walikuwa wenye busara.”—Matayo 25:1, 2.

Yesu hatake kusema kama nusu ya wanafunzi wake wenye wanariti Ufalme wa mbinguni ni wapumbavu na kama wengine nusu ni wenye busara. Lakini anapenda kuonyesha kwamba kuhusu Ufalme, kila mwanafunzi wake anaweza kuchagua kukesha ao kukengeushwa. Yesu iko hakika kwamba kila mwanafunzi wake anaweza kubaki muaminifu na kupokea baraka kutoka kwa Baba yake.

Katika mufano, mabikira wote kumi wanaenda kumupokea bwana-arusi na wanaenda kujiunga na kikundi cha kusindikiza bwana-arusi na bibi-arusi. Wakati anafika, mabikira wataangazia njia kwa taa zao, wakionyesha heshima kwa bwana-arusi wakati analeta bibi-arusi wake katika nyumba yenye ilitayarishwa kwa ajili yake. Lakini sasa mambo yanatendeka namna gani?

Yesu anaeleza hivi: “Wale wapumbavu walibeba taa zao lakini hawakubeba mafuta ya kuongeza, lakini wale wenye busara walibeba taa zao pamoja na mafuta katika chupa zao. Wakati bwana-arusi alikawia kuja, wote walisinzia na kuanza kulala.” (Matayo 25:3-5) Bwana-arusi hafike haraka kama vile alitazamiwa. Inaonekana anachelewa sana, kwa hiyo mabikira wanalala. Pengine mitume wanakumbuka yale yenye Yesu alieleza kuhusu mutu fulani wa familia ya kifalme mwenye alisafiri na ‘mwishowe alirudia kisha kupokea ufalme.’—Luka 19:11-15.

Katika mufano wa mabikira kumi, Yesu anaeleza jambo lenye linatokea wakati mwishowe bwana-arusi anafika: “Katikati ya usiku kukatokea sauti kubwa: ‘Bwana-arusi anafika! Muende mumupokee.’” (Matayo 25:6) Je, mabikira wako tayari na wenye kukesha?

Yesu anaendelea hivi: “Kisha wale mabikira wote wakasimama na kutayarisha taa zao. Wale wapumbavu wakaambia wenye busara, ‘Mutupatie sehemu kidogo ya mafuta yenu, kwa sababu taa zetu zinakaribia kuzimika.’ Wale wenye busara wakawajibu, na kusema: ‘Pengine hakutakuwa ya kutuenea sisi na ninyi. Lakini muende kwa wenye kuyauzisha, na mujinunulie yenu.’”—Matayo 25:7-9.

Kwa hiyo mabikira watano wapumbavu hawakeshe na hawako tayari kwa ajili ya kufika kwa bwana-arusi. Wanakosa mafuta yenye kuenea kwa ajili ya taa zao na wanajaribu kutafuta mafuta. Yesu anaeleza: “Wakati walikuwa wanaenda kununua mafuta, bwana-arusi akafika. Wale mabikira wenye walikuwa tayari wakaingia pamoja naye kwenye karamu ya ndoa, na mulango ukafungwa. Kisha, wale mabikira wengine pia wakakuja, na kusema, ‘Bwana, Bwana, tufungulie!’ Akawajibu, ‘Ninawaambia kweli, siwajue ninyi.’” (Matayo 25:10-12) Matokeo yenye kuhuzunisha kabisa kwa sababu hawakuendelea kuwa tayari na hawakukesha.

Mitume wanaweza kutambua kwamba bwana-arusi mwenye Yesu anazungumuzia ni yeye mwenyewe. Hapo mbele alijifananisha na bwana-arusi. (Luka 5:34, 35) Sasa mabikira wenye busara ni nani? Wakati alizungumuzia “kundi ndogo,” wenye wangepewa Ufalme, Yesu alitumia maneno haya: “Muvae nguo na mukuwe tayari na taa zenu zikuwe zenye kuwaka.” (Luka 12:32, 35) Kwa hiyo katika mufano huu kuhusu mabikira, mitume wanaweza kuelewa kwamba Yesu anazungumuzia juu yao wenyewe. Kwa hiyo, ni ujumbe gani Yesu anapenda kutoa kupitia mufano huo?

Yesu anapenda kuhakikisha kwamba wanaelewa. Kwa hiyo anamalizia mufano huo kwa kuwaambia hivi: “Muendelee kukesha, kwa sababu hamujue siku wala saa.”—Matayo 25:13.

Ni wazi kwamba Yesu anaonya wafuasi wake waaminifu kwamba wakati wa kuwapo kwake, wanapaswa, ‘kuendelea kukesha.’ Atakuja, na wanapaswa kuwa tayari na kukesha, kama wale mabikira tano ili wasipoteze tumaini lao la maana sana na kukosa baraka.