Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 113

Mufano wa Talanta​—Somo Kuhusu Bidii

Mufano wa Talanta​—Somo Kuhusu Bidii

MATAYO 25:14-30

  • YESU ANATOA MUFANO WA TALANTA

Wakati angali na mitume wake ine kwenye Mulima wa Mizeituni, Yesu anawatolea mufano mwengine. Siku kidogo mbele ya hapo, wakati alikuwa Yeriko alitoa mufano wa mina ili kuonyesha kwamba Ufalme haungekuja wakati huo. Mufano wenye anatoa sasa uko na mambo yenye kufanana na mufano wenye alikuwa ametoa wakati huo. Mufano huu ni sehemu ya jibu lake kwa ulizo lenye kuhusu kuwapo kwake na kuhusu umalizio wa mupangilio wa mambo. Unaonyesha kwamba wanafunzi wake wanapaswa kufanya kwa bidii mambo yenye anawaomba.

Yesu anaanza kwa kusema hivi: “Ni kama mutu mwenye alikuwa karibu kusafiri kuenda katika inchi ingine, mwenye aliita watumwa wake na kuwapatia mali zake.” (Matayo 25:14) Kwa kuwa Yesu alikuwa tayari amejifananisha na mutu mwenye kusafiri katika inchi ingine “ili afanywe kuwa mufalme,” mitume wangeelewa haraka kwamba Yesu ndiye ule “mutu” mwenye kuzungumuziwa sasa.—Luka 19:12.

Mbele mutu huyo asafiri na kuenda katika inchi ingine, anaachia watumwa wake mali. Wakati wa utumishi wake wa miaka tatu na nusu, Yesu alikazia kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, na alizoeza wanafunzi wake kufanya kazi hiyo. Sasa anaenda zake, akiwa hakika kwamba wataendelea kufanya mambo kulingana na mazoezi yenye aliwatolea.—Matayo 10:7; Luka 10:1, 8, 9; linganisha na Yohana 4:38; 14:12.

Katika mufano huo, namna gani mutu huyo anagawanya mali zake? Yesu anaeleza: “Akapatia mumoja talanta tano (5), mwingine mbili, na mwingine moja, kila mumoja kulingana na uwezo wake mwenyewe, kisha akaenda katika inchi ingine.” (Matayo 25:15) Namna gani watumwa hao watatumikisha mali zenye walipewa? Watazitumia kwa bidii ili kuletea bwana wao faida nyingi? Yesu anaambia mitume hivi:

“Mara moja ule mwenye alipokea talanta tano (5) akaenda na kufanya nazo biashara, akapata faida ya talanta zingine tano (5). Vilevile, ule mwenye alipokea talanta mbili, akapata faida ya talanta zingine mbili. Lakini mutumwa mwenye alipokea talanta moja tu akaenda akachimba katika udongo na kuficha zile feza za bwana wake.” (Matayo 25:16-18) Mambo yanakuwa namna gani wakati bwana wao anarudi?

Yesu anaendelea: “Kisha wakati murefu, bwana wa watumwa hao akarudia na kufanya hesabu nao.” (Matayo 25:19) Wale watumwa wawili wa kwanza walifanya yao yote, “kila mumoja kulingana na uwezo wake mwenyewe.” Kila mutumwa alikuwa na bidii, alitumika sana, na alipata faida wakati alitumikisha mali yenye walimupatia. Ule mwenye alipokea talanta tano alipata ingine tano, na ule mwenye alipokea talanta mbili alipata ingine mbili. (Wakati huo, mufanyakazi alipaswa kutumika sana kwa miaka karibu 19 ili kupata mushahara wenye kulingana na talanta moja.) Bwana wao alisifu kila mumoja wao kwa maneno haya: “Umefanya muzuri, mutumwa mwema na mwaminifu! Ulikuwa mwaminifu katika mambo kidogo. Nitakuweka usimamie mambo mengi. Ingia katika furaha ya bwana wako.”—Matayo 25:21.

Mambo yako tofauti na mutumwa mwenye alipokea talanta moja. Anasema hivi: “Bwana nilijua wewe ni mutu mugumu, unavuna mahali kwenye haukupanda na unakusanya mahali kwenye haukupepulia. Kwa hiyo, niliogopa na nikaenda kuficha talanta yako katika udongo. Angalia, mali yako ndiyo hii.” (Matayo 25:24, 25) Hakuweza hata kutia feza hizo katika benki ili bwana wake azichukue pamoja na faida. Kwa kweli, ametenda tofauti na vile bwana wake alimuomba.

Ndiyo sababu, bwana wake anamuita “mutumwa muovu na muvivu.” Talanta yenye alikuwa nayo inapewa mutumwa mwingine mwenye iko tayari kutumika kwa bidii. Bwana anajulisha kanuni yake: “Kila mutu mwenye kuwa na kitu, ataongezewa, na atakuwa na vingi. Lakini ule mwenye hana, atanyanganywa hata kile chenye iko nacho.”—Matayo 25:26, 29.

Mufano huu unapaswa kufanya wanafunzi wafikiri sana. Wanapaswa kuelewa kwamba, pendeleo la kufanya wanafunzi, lenye Yesu amewatolea ni la maana sana. Na anatazamia kwamba watatumika kwa bidii. Yesu hawaze kama wote wanapaswa kutimiza kwa namna ileile kazi ya kuhubiri yenye amewatolea. Kama vile inaonyeshwa katika mufano huo, kila mumoja wao angefanya yote yenye anaweza “kulingana na uwezo wake mwenyewe.” Inamaanisha kama Yesu hatapendezwa hata kidogo ikiwa mumoja kati yao anakuwa “muvivu” na anashindwa kufanya yake yote ili kuongeza mali za Bwana.

Mitume wanapaswa kufurahi kabisa, wakati wanasikia maneno haya: “Kila mutu mwenye kuwa na kitu, ataongezewa”!