Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 119

Yesu​—Njia, Kweli, na Uzima

Yesu​—Njia, Kweli, na Uzima

YOHANA 14:1-31

  • YESU ANAENDA KUTAYARISHA MAHALI

  • ANAWAAHIDI WAFUASI WAKE MSAIDIZI

  • BABA NI MKUU KULIKO YESU

Akiwa bado katika chumba cha juu pamoja na mitume baada ya mlo wa ukumbusho, Yesu anawatia moyo hivi: “Mioyo yenu isitaabike. Iweni na imani katika Mungu; iweni na imani pia katika mimi.”—Yohana 13:36; 14:1.

Yesu anawapa mitume wake sababu itakayowasaidia wasiwe na wasiwasi atakapoondoka: “Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. . . . Nikienda na kuwatayarishia mahali, nitakuja tena nami nitawapokea nyumbani kwangu, ili mahali nilipo, ninyi pia muwe hapo.” Hata hivyo, mitume hawaelewi kwamba anazungumza kuhusu kwenda mbinguni. Tomasi anasema: “Bwana, sisi hatujui unakoenda. Tunawezaje kuijua njia?”—Yohana 14:2-5.

Yesu anajibu hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.” Mtu anaweza kuingia katika nyumba ya Baba yake wa mbinguni ikiwa tu atamkubali Yesu, mafundisho yake, na kuiga maisha yake. Yesu anasema: “Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.”—Yohana 14:6.

Filipo ambaye anasikiliza kwa makini, anatoa ombi hili: “Bwana, tuonyeshe Baba na hilo linatutosha.” Inaonekana Filipo anataka ishara fulani kutoka kwa Mungu, kama vile maono ambayo Musa, Eliya, na Isaya walipokea. Hata hivyo, mitume wana kitu bora kuliko maono hayo. Yesu anaonyesha jambo hilo anaposema: “Je, hata baada ya kuwa pamoja nanyi kwa muda mrefu hivyo, bado Filipo hujanijua? Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” Yesu anawakilisha kikamili utu wa Baba; kwa hiyo, kuishi pamoja na Yesu na kumtazama ni kama kumwona Baba. Bila shaka, Baba ni mkuu kuliko Mwana, kwa maana Yesu anasema: “Mambo ninayowaambia sisemi kwa kujitungia.” (Yohana 14:8-10) Mitume wanaona kwamba Yesu anampa sifa Baba yake kwa mambo yote anayofundisha.

Mitume wa Yesu wamemwona akifanya kazi za ajabu na wamemsikia akitangaza habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu. Sasa anawaambia: “Yeyote anayeniamini atafanya pia kazi ambazo mimi hufanya; naye atafanya kazi kubwa kuliko hizi.” (Yohana 14:12) Yesu hamaanishi kwamba watafanya miujiza mikubwa kuliko ile aliyofanya. Hata hivyo, watafanya huduma yao kwa kipindi kirefu zaidi, katika eneo kubwa zaidi, na kuwahubiria watu wengi zaidi.

Yesu atakapoondoka hatawaacha peke yao, anawaahidi hivi: “Mkiomba jambo lolote katika jina langu, nitalifanya.” Isitoshe anasema: “Nitamwomba Baba, naye atawapa msaidizi mwingine awe pamoja nanyi milele, roho ya ile kweli.” (Yohana 14:14, 16, 17) Anawahakikishia kwamba watapokea msaidizi mwingine, yaani, roho takatifu. Jambo hilo linatokea siku ya Pentekoste.

Yesu anasema: “Bado muda kidogo nao ulimwengu hautaniona tena, lakini ninyi mtaniona, kwa sababu ninaishi, nanyi mtaishi.” (Yohana 14:19) Yesu atawatokea katika umbo la kimwili baada ya kufufuliwa, na pia, baadaye, atawafufua ili wawe pamoja naye mbinguni wakiwa viumbe wa roho.

Sasa Yesu anataja ukweli huu: “Yeyote aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye anayenipenda. Na yeyote anayenipenda atapendwa na Baba yangu, nami nitampenda na kujionyesha waziwazi kwake.” Kisha mtume Yuda, ambaye pia anaitwa Thadayo, anauliza: “Bwana, imekuwaje kwamba unakusudia kujionyesha waziwazi kwetu bali si kwa ulimwengu?” Yesu anamjibu hivi: “Ikiwa yeyote ananipenda, atalishika neno langu, naye Baba yangu atampenda . . . Yeyote asiyenipenda hayashiki maneno yangu.” (Yohana 14:21-24) Tofauti na wafuasi wake, ulimwengu hautambui kwamba Yesu ndiye njia, kweli, na uzima.

Yesu ataondoka, basi wanafunzi wake watakumbukaje mambo yote aliyowafundisha? Yesu anaeleza hivi:“Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba ataituma katika jina langu, hiyo itawafundisha mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” Mitume wameona jinsi roho takatifu ilivyo na nguvu, basi wanatiwa moyo na uhakikisho huo. Yesu anaongezea hivi: “Ninawaachia amani; ninawapa amani yangu. . . . Mioyo yenu isitaabike wala kuogopa.” (Yohana 14:26, 27) Basi wanafunzi hawapaswi kuwa na wasiwasi, kwa kuwa Baba ya Yesu atawaongoza na kuwalinda.

Baada ya muda mfupi, itathibitika wazi kwamba Mungu anawalinda. Yesu anasema: “Mtawala wa ulimwengu anakuja, naye hana uwezo juu yangu.” (Yohana 14:30) Ibilisi alifaulu kumwingia Yuda na kumwongoza. Lakini Yesu hana udhaifu unaoletwa na dhambi ambao Shetani anaweza kuutumia kumfanya amwasi Mungu. Wala Ibilisi hataweza kumzuia Yesu katika kifo. Kwa nini? Yesu anasema: “Ninafanya kama vile Baba alivyoniamuru.” Ana uhakika kwamba Baba yake atamfufua.—Yohana 14:31.