Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 122

Sala ya Mwisho ya Yesu Katika Chumba cha Juu

Sala ya Mwisho ya Yesu Katika Chumba cha Juu

YOHANA 17:1-26

  • MATOKEO YA KUMJUA MUNGU NA MWANA WAKE

  • UMOJA KATI YA YEHOVA, YESU, NA WANAFUNZI

Akichochewa na upendo wake mwingi kwa mitume wake, Yesu amekuwa akiwatayarisha kabla hajaondoka. Sasa anatazama mbinguni na kusali hivi kwa Baba yake: “Mtukuze mwana wako ili mwana wako akutukuze, kama vile ulivyompa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili awape uzima wa milele wote ambao umempa.”—Yohana 17:1, 2.

Kwa kweli, Yesu anatambua kwamba kumpa Mungu utukufu ndilo jambo muhimu zaidi. Lakini tumaini ambalo Yesu anataja linafariji sana—uzima wa milele! Akiwa amepokea “mamlaka juu ya wote wenye mwili,” Yesu anaweza kuwaletea wanadamu wote faida za fidia. Ingawa hivyo, ni wachache tu watakaopata baraka hiyo. Kwa nini ni wachache? Kwa sababu Yesu atawaletea baraka za fidia wale tu wanaotenda kulingana na jambo ambalo sasa Yesu anataja: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Lazima mtu amjue Baba na Mwana kwa undani, na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja nao. Anapaswa kuwa na maoni kama yao. Isitoshe, anapaswa kujitahidi kuiga sifa zao zisizo na kifani anaposhughulika na wengine. Anapaswa kuelewa kwamba jambo muhimu zaidi ni kutukuzwa kwa jina la Mungu, kisha jambo la pili ni wanadamu kupata uzima wa milele. Sasa Yesu anaendelea na mazungumzo yake.

“Nimekutukuza duniani, kwa kuwa nimemaliza kazi uliyonipa nifanye. Sasa Baba, nitukuze kando yako kwa utukufu niliokuwa nao kando yako kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:4, 5) Naam, Yesu anaomba kurudishwa katika utukufu wa mbinguni kupitia ufufuo.

Hata hivyo, Yesu hasahau mambo ambayo ametimiza katika huduma yake. Anasali hivi: “Nimelifunua jina lako kwa watu ulionipa kutoka ulimwenguni. Walikuwa wako, nawe ukanipa, nao wamelishika neno lako.” (Yohana 17:6) Katika huduma yake, Yesu alifanya mengi zaidi ya kulitamka tu jina la Mungu, Yehova. Aliwasaidia mitume wake waelewe kile kinachowakilishwa na jina hilo, yaani, sifa za Mungu na jinsi anavyoshughulika na wanadamu.

Mitume wamemjua Yehova, jukumu la Mwana wake, na mambo ambayo Yesu amefundisha. Yesu anasema hivi kwa unyenyekevu: “Nimewapa maneno uliyonipa, nao wameyakubali na kwa hakika wamejua kwamba nilikuja nikiwa mwakilishi wako, nao wameamini kwamba ulinituma.”—Yohana 17:8.

Kisha Yesu anataja tofauti kati ya wafuasi wake na ulimwengu wa wanadamu kwa ujumla: “Siombi kwa ajili ya ulimwengu, bali ninawaombea wale ulionipa, kwa sababu ni wako . . . Baba Mtakatifu, walinde kwa sababu ya jina lako ambalo umenipa, ili wawe kitu kimoja kama vile sisi tulivyo kitu kimoja. . . . Nimewalinda na hakuna hata mmoja wao aliyeangamizwa ila yule mwana wa maangamizi,” yaani, Yuda Iskariote, ambaye anaendelea na mipango ya kumsaliti Yesu.—Yohana 17:9-12.

“Ulimwengu umewachukia,” Yesu anaendelea kusali. “Sikuombi uwatoe ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14-16) Mitume na wanafunzi wengine wako ulimwenguni, yaani, jamii ya wanadamu inayotawaliwa na Shetani, lakini wanapaswa kujitenga na ulimwengu na uovu wake. Jinsi gani?

Wanapaswa kuendelea kuwa watakatifu, wakiwa wametengwa kwa ajili ya kumtumikia Mungu, kwa kufuata kweli zilizo katika Maandiko ya Kiebrania na kweli ambazo Yesu mwenyewe amefundisha. Yesu anasali hivi: “Watakase kupitia ile kweli; neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Baada ya muda, baadhi ya mitume wataandika vitabu vilivyoongozwa na roho ya Mungu ambavyo vitakuwa sehemu ya “kweli” inayoweza kumtakasa mtu.

Lakini baadaye kuna wengine ambao watakubali “kweli.” Basi Yesu anasali “si kwa ajili ya Hawa tu [yaani, wale walio hapo], bali pia wale [wanaomwamini] kupitia neno lao.” Yesu anaomba nini kwa ajili yao wote? “Wawe kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe Baba umo katika muungano nami, nami nimo katika muungano nawe, ili wao pia wawe katika muungano nasi.” (Yohana 17:20, 21) Kihalisi, Yesu na Baba yake si mtu mmoja. Wao ni kitu kimoja katika maana ya kwamba wanakubaliana katika mambo yote. Yesu anasali kwamba wafuasi wake wafurahie umoja huo.

Muda mfupi kabla ya hapo, Yesu alikuwa amemwambia Petro na wenzake kwamba alikuwa anaenda kuwatayarishia mahali, akimaanisha huko mbinguni. (Yohana 14:2, 3) Sasa Yesu anataja jambo hilo katika sala: “Baba, ninataka wale ambao umenipa wawe pamoja nami mahali nilipo, ili waone utukufu wangu ambao umenipa, kwa sababu ulinipenda kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu.” (Yohana 17:24) Kwa hiyo, anathibitisha kwamba zamani za kale—kabla Adamu na hawa hawajazaa watoto—Mungu alimpenda mwana wake mzaliwa wa pekee, ambaye alikuja kuwa Yesu Kristo.

Yesu anamalizia sala yake kwa kusisitiza jina la Baba yake na upendo wa Mungu kwa mitume na kwa wengine ambao watakubali ile “kweli,” anaposema: “Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda uwe ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”—Yohana 17:26.