Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 124

Kristo Anasalitiwa na Kufungwa

Kristo Anasalitiwa na Kufungwa

MATAYO 26:47-56 MARKO 14:43-52 LUKA 22:47-53 YOHANA 18:2-12

  • YUDA ANAMUSALITI YESU KATIKA BUSTANI

  • PETRO ANAKATA SIKIO LA MWANAUME FULANI

  • YESU ANAKAMATWA

Katikati ya usiku imepita kabisa. Makuhani wamekubali kumupatia Yuda vipande 30 vya feza ili amusaliti Yesu. Kwa hiyo, Yuda anaongoza kikundi kikubwa cha makuhani wakubwa na Wafarisayo ili kuenda kumutafuta Yesu. Wanasindikizwa na kikundi fulani cha maaskari Waroma chenye kuwa na silaha na chenye kuongozwa na kamanda.

Inaonekana kuwa wakati Yesu aliambia Yuda aondoke kwenye chakula cha Pasaka, Yuda alienda mara moja kwa wakubwa wa makuhani. (Yohana 13:27) Walikusanya walinzi wao na kikundi cha maaskari. Pengine Yuda aliwapeleka kwanza kwenye chumba ambamo Yesu na mitume wake walifanyia sikukuu ya Pasaka. Lakini sasa kikundi hicho kikubwa kimevuka Bonde la Kidroni na kinaenda kwenye bustani. Zaidi ya silaha, wako pia na mienge na taa, wanapenda kabisa kumupata Yesu.

Wakati Yuda anaongoza kikundi hicho cha watu kwenye Mulima wa Mizeituni, iko hakika kuwa atamupata Yesu huko. Juma lenye lilipita wakati Yesu na mitume wake walikuwa wanafanya safari kati ya Betania na Yerusalemu, mara kwa mara walisimama katika bustani ya Getsemane. Lakini sasa ni usiku, na Yesu anaweza kuwa katika vivuli vya miti ya mizeituni katika bustani. Kwa hiyo, namna gani maaskari wenye pengine walikuwa hawajamuona Yesu hata siku moja wangeweza kumujua? Ili kuwasadia, Yuda atawatolea alama fulani. Anasema hivi: “Kila mutu mwenye nitabusu, ni yeye; mumukamate na kumufunga.”—Marko 14:44.

Wakati Yuda anaongoza kikundi hicho katika bustani, anamuona Yesu na mitume wake na anaenda mara moja nafasi kwenye iko. Yuda anasema hivi: “Jambo Rabi!” na anamubusu Yesu kwa wororo. Yesu anamuambia hivi: “Mwenzangu, umekuja kufanya nini?” (Matayo 26:49, 50) Yesu anajibu ulizo lake mwenyewe, anasema hivi: “Yuda, unamusaliti Mwana wa binadamu kwa busu?” (Luka 22:48) Yesu anaachia pale, hahangaike tena juu ya musaliti wake!

Sasa Yesu anaingia katika mwangaza wa mienge na taa na kuuliza hivi: “Munatafuta nani?” Kikundi hicho kinajibu hivi: “Yesu Munazareti.” Bila kuogopa, Yesu anasema hivi: “Ni mimi.” (Yohana 18:4, 5) Kwa sababu hawakujua mambo yatakuwa namna gani, wanaume hao wanaanguka chini.

Kuliko kuchukua nafasi hiyo ili kukimbilia katika giza, Yesu anauliza tena wanatafuta nani. Wakati wanasema tena, “Yesu Munazareti,” kwa utulivu, anasema hivi: “Niliwaambia ni mimi. Basi, kama munanitafuta, muache hawa waende.” Hata katika wakati huu mugumu sana, Yesu anakumbuka mambo yenye alikuwa amesema, kuwa hatapoteza hata mumoja wao. (Yohana 6:39; 17:12) Yesu amelinda mitume wake waaminifu na hakuna mwenye amepotea, “isipokuwa ule mwana wa uharibifu,” ni kusema, Yuda. (Yohana 18:7-9) Kwa hiyo, anaomba sasa waache mitume wake waaminifu waende.

Wakati maaskari wanasimama na kuanza kumukaribia Yesu, mitume wanaelewa mambo yenye yanafanyika. Wanauliza hivi: “Bwana, tuwapige kwa upanga?” (Luka 22:49) Hata mbele Yesu ajibie, Petro anachukua upanga moja kati ya panga mbili zenye mitume wako nazo. Anamushambulia Malko, mutumishi wa kuhani mukubwa, na kumukata sikio la upande wa kuume.

Yesu anagusa sikio la Malko na kuponyesha kidonda. Kisha anafundisha somo la maana kwa kumuamuru Petro hivi: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wote wenye wanatumikisha upanga watakufa kwa upanga.” Yesu iko tayari kufungwa, kwa sababu anasema hivi: “Maandiko yenye kusema kuwa mambo haya yanapaswa kutendeka, yatatimizwa namna gani?” (Matayo 26:52, 54) Anaongeza hivi: “Je, sipaswe kunywa kikombe chenye Baba amenipatia?” (Yohana 18:11) Yesu alikubali mapenzi ya Mungu yatendeke juu yake, hata kufikia hatua ya kufa.

Yesu anauliza hivi kikundi hicho cha watu: “Je, mumekuja kunikamata mukiwa na mapanga na marungu kama vile munakuja kumukamata munyanganyi? Kila siku nilikuwa ninakaa katika hekalu nikifundisha, lakini hamukunikamata na kunifunga. Lakini yote haya yametokea ili kutimiza mambo yenye manabii waliandika.”—Matayo 26:55, 56.

Kikundi cha maaskari, kamanda wa jeshi, na walinzi wa Wayahudi wanamukamata Yesu na kumufunga. Wakati mitume wanaona jambo hilo, wanakimbia. Hata hivyo, “kijana mumoja,” pengine mwanafunzi Marko anabakia pamoja na kikundi hicho ili kumufuata Yesu. (Marko 14:51) Kijana huyo anatambuliwa, na kikundi hicho cha watu kinajaribu kumukamata, kwa hiyo, anaacha nguo yake ya kitani na kukimbia.