Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 128

Pilato na Herode Wakosa Kumpata Yesu na Hatia

Pilato na Herode Wakosa Kumpata Yesu na Hatia

Yesu hajaribu kumficha Pilato kwamba kwa kweli yeye ni mfalme. Hata hivyo, Ufalme wake si tishio kwa Roma. “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu,” Yesu anasema. “Kama Ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, Ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Naam, Yesu ana Ufalme, lakini si sehemu ya ulimwengu huu.

Pilato hapuuzi jambo hilo. Anauliza hivi: “Kwa hiyo, wewe ni mfalme?” Yesu anataka Pilato ajue kwamba jibu lake ni sahihi, anaposema: “Wewe mwenyewe unasema kwamba mimi ni mfalme. Nimezaliwa kwa ajili ya hili, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi kuhusu kweli. Kila mtu aliye upande wa kweli huisikiliza sauti yangu.”—Yohana 18:37.

Hapo awali Yesu alikuwa amemwambia hivi Tomasi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.” Sasa hata Pilato anasikia kwamba kusudi la Yesu kutumwa duniani ni ili kutoa ushahidi kuhusu “kweli,” hasa kweli kuhusu Ufalme wake. Yesu ameazimia kushikamana na kweli hiyo hata kama itamgharimu uhai wake. Pilato anauliza: “Kweli ni nini?” lakini hasubiri ufafanuzi zaidi. Anafikiri kwamba mambo aliyosikia yanatosha kumhukumu mtu huyu.—Yohana 14:6; 18:38.

Pilato anarudi kuongea na umati unaosubiri nje ya jumba la mfalme. Inaonekana Yesu yuko kando yake anapowaambia hivi wakuu wa makuhani na wale wote walio pamoja nao: “Sioni mtu huyu akiwa na kosa lolote.” Umati ukiwa umekasirishwa na uamuzi huo, unasisitiza hivi: “Anawachochea watu kwa kufundisha katika Yudea yote, kuanzia Galilaya mpaka hapa.”—Luka 23:4, 5.

Lazima Pilato anashangazwa na ushupavu wa Wayahudi usio na msingi. Wakuu wa makuhani na wanaume wazee wanapoendelea kupaza sauti, Pilato anamuuliza Yesu: “Je, husikii ni mambo mangapi wanayoshuhudia dhidi yako?” (Mathayo 27:13) Yesu hatoi jibu lolote. Utulivu wake anapokabili mashtaka ya uwongo unamshangaza Pilato.

Wayahudi walisema kwamba Yesu ‘alianzia Galilaya.’ Pilato anapofuatilia jambo hilo, anagundua kwamba kwa kweli Yesu ni Mgalilaya. Hilo linampa Pilato wazo la jinsi anavyoweza kuepuka jukumu la kumhukumu Yesu. Herode Antipa (Mwana wa Herode Mkuu) ndiye mtawala wa Galilaya, naye yuko Yerusalemu majira hayo ya Pasaka. Basi Pilato anaagiza Yesu apelekwe kwa Herode. Herode Antipa ndiye aliyeamuru Yohana Mbatizaji akatwe kichwa. Baadaye aliposikia kwamba Yesu alikuwa anafanya miujiza, Herode alikuwa na wasiwasi kwamba huenda Yesu ni Yohana ambaye amefufuka kutoka kwa wafu.—Luka 9:7-9.

Sasa Herode anafurahi anapotazamia kumwona Yesu. Si kwamba anataka kumsaidia Yesu au anataka kujua kama kweli kuna mashtaka halali dhidi yake. Kwa ufupi, Herode ni mdadisi, naye ‘anatamani kumwona akifanya miujiza.’ (Luka 23:8) Hata hivyo, Yesu hatoshelezi udadisi wa Herode. Kwa kweli, Herode anapomuuliza maswali, Yesu hajibu. Herode na wanajeshi wake wakiwa wamekasirika, wanamtendea Yesu “kwa dharau.” (Luka 23:11) Wanamvika vazi la kifahari na kumdhihaki. Kisha Herode anaagiza Yesu arudishwe kwa Pilato. Herode na Pilato walikuwa maadui, lakini sasa wanakuwa marafiki.

Yesu anaporudi, Pilato anawaita pamoja wakuu wa makuhani, viongozi wa Wayahudi, na watu wote na kusema: “Nilimhoji mbele yenu lakini sikupata msingi wa mashtaka yenu dhidi yake. Kwa kweli, hata Herode hakupata, ndiyo maana alimrudisha kwetu, tazama! ni wazi hajafanya jambo lolote linalostahili kifo. Kwa hiyo nitamwadhibu na kumfungua.”—Luka 23:14-16.

Pilato anataka kumweka Yesu huru, kwa kuwa anagundua kwamba makuhani wamemleta kwake kwa sababu ya wivu. Pilato anapojaribu kumweka Yesu huru, anapata sababu nyingine inayomchochea kufanya hivyo. Akiwa kwenye kiti chake cha hukumu, mke wake anamtumia ujumbe huu: “Mwache mtu huyo mwadilifu, kwa maana niliteseka sana leo katika ndoto [inaonekana ilitoka kwa Mungu] kwa sababu yake.”—Mathayo 27:19.

Pilato anawezaje kumweka huru mtu huyu asiye na hatia, kama anavyopaswa kufanya?