Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 136

Kwenye Ufuo wa Bahari ya Galilaya

Kwenye Ufuo wa Bahari ya Galilaya

YOHANA 21:1-25

  • YESU ATOKEA KWENYE BAHARI YA GALILAYA

  • PETRO NA WENGINE WATALISHA KONDOO

Katika jioni ya mwisho pamoja na mitume wake, Yesu alikuwa amewaambia: “Baada ya kufufuliwa nitawatangulia kuingia Galilaya.” (Mathayo 26:32; 28:7, 10) Sasa wengi kati ya wafuasi wake wanafunga safari hiyo, lakini watafanya nini huko Galilaya?

Pindi fulani, Petro anawaambia hivi mitume sita: “Ninaenda kuvua samaki.” Wote sita wanamwambia: “Sisi pia tutaenda nawe.” (Yohana 21:3) Hawavui samaki hata mmoja usiku kucha. Kunapoanza kupambazuka, Yesu anatokea ufuoni, lakini hawatambui ni nani. Yesu anauliza hivi kwa sauti kubwa: “Watoto, mna chakula chochote?” Wanamjibu: “Hapana!” Yesu anawaambia: “Utupeni wavu upande wa kulia wa mashua, nanyi mtapata.” (Yohana 21:5, 6) Wanavua samaki wengi sana mpaka wanashindwa kuuvuta wavu.

Yohana anamwambia Petro hivi: “Ni Bwana!” (Yohana 21:7) Mara moja, Petro anavaa vazi lake la nje ambalo hakuwa amelivaa alipokuwa akivua samaki. Anaruka ndani ya maji na kuogelea karibu mita 90 hadi ufuoni. Wengine walio katika mashua wanamfuata polepole, huku wakikokota wavu uliojaa samaki.

Wanapofika ufuoni wanaona “moto wa makaa na juu yake [kuna] samaki na mkate.” Yesu anasema: “Leteni baadhi ya samaki mliowavua sasa hivi.” Petro anauvuta wavu uliojaa samaki wakubwa 153! Yesu anasema: “Njooni mpate kiamshakinywa.” Hakuna hata mmoja wao aliye na ujasiri wa kumuuliza: “Wewe ni nani?” kwa sababu wanatambua kwamba ni Yesu. (Yohana 21:9-12) Hii ni mara yake ya tatu kuwatokea wanafunzi wake wakiwa kikundi.

Yesu anampa kila mmoja wao mkate na samaki ili wale. Kisha, labda akiwatazama wale samaki waliovuliwa anauliza: “Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda kuliko hawa?” Je, Petro anapenda sana biashara ya samaki kuliko kazi ambayo Yesu anataka afanye? Petro anajibu hivi: “Ndiyo, Bwana, unajua ninakupenda.” Basi Yesu anamhimiza hivi: “Lisha wanakondoo wangu.”—Yohana 21:15.

Yesu anauliza tena: “Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda?” Labda Petro akiwa ameshangaa anajibu hivi kwa hisia: “Ndiyo, Bwana, unajua ninakupenda.” Yesu anatoa jibu lilelile: “Chunga kondoo wangu wadogo.”—Yohana 21:16.

Yesu anauliza mara ya tatu: “Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda?” Sasa huenda Petro anawaza kuwa Yesu anashuku ushikamanifu wake. Petro anasema hivi kwa msisitizo: “Bwana, wewe unajua mambo yote; unajua kwamba ninakupenda.” Yesu anakazia tena jambo ambalo Petro anapaswa kufanya: “Lisha kondoo wangu wadogo.” (Yohana 21:17) Naam, wale wanaoongoza wanapaswa kuwahudumia watu walio katika kundi la kondoo wa Mungu.

Yesu alikamatwa na kuuawa kwa sababu alifanya kazi ambayo Mungu alimwagiza afanye. Sasa anafunua kwamba Petro atapatwa na jambo kama hilo. Yesu anasema: “Ulipokuwa kijana, ulikuwa unavaa mwenyewe na kutembea kokote ulikotaka. Lakini utakapozeeka, utanyoosha mikono yako na mtu mwingine atakuvalisha na kukupeleka usikotaka.” Hata hivyo, Yesu anamhimiza hivi: “Endelea kunifuata.”—Yohana 21:18, 19.

Petro anauliza hivi anapomwona mtume Yohana: “Bwana, namna gani kuhusu mtu huyu?” Naam, wakati ujao itakuwaje kwa mtume huyu ambaye anapendwa sana na Yesu? Yesu anajibu hivi: “Ikiwa ni mapenzi yangu akae mpaka nije, hilo linakuhusuje?” (Yohana 21:21-23) Petro anahitaji kumfuata Yesu bila kuhangaishwa na mambo ambayo wengine wanafanya. Hata hivyo, Yesu anaonyesha kwamba Yohana ataishi muda mrefu kuliko mitume wengine, naye atapewa maono ya Yesu akija katika mamlaka ya Ufalme.

Bila shaka, Yesu alifanya mambo mengine mengi, ambayo hayawezi kutoshea katika vitabu vingi vya kukunjwa.