Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 138

Kristo Akiwa Kwenye Mkono wa Kuume wa Mungu

Kristo Akiwa Kwenye Mkono wa Kuume wa Mungu

MATENDO 7:56

  • YESU AKETI KWENYE MKONO WA KUUME WA MUNGU

  • SAULI ANAKUWA MWANAFUNZI

  • TUNA SABABU YA KUSHANGILIA

Siku kumi baada ya Yesu kupaa mbinguni, roho takatifu iliyomiminwa siku ya Pentekoste ilithibitisha kwamba kwa kweli alikuwa mbinguni. Na kungekuwa na uthibitisho mwingine zaidi kuhusu jambo hilo. Muda mfupi kabla ya mwanafunzi Stefano kupigwa mawe kwa sababu ya kutoa ushahidi kwa uaminifu, alipaza sauti hivi: “Tazama! Ninaziona mbingu zimefunguka na Mwana wa binadamu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.”—Matendo 7:56.

Akiwa pamoja na Baba yake mbinguni, Yesu angesubiri agizo hususa lililotabiriwa katika Neno la Mungu. Daudi aliandika hivi akiongozwa na roho takatifu: “Yehova alimtangazia hivi Bwana wangu [Yesu]: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka nitakapowaweka maadui wako kuwa kiti cha miguu yako.’” Baada ya kipindi hicho cha kusubiri kwisha, angeenda ‘akitiisha kati ya maadui wake.’ (Zaburi 110:1, 2) Lakini Yesu angekuwa akifanya nini mbinguni alipokuwa akisubiri muda ufike wa kuwachukulia hatua adui zake?

Siku ya Pentekoste 33 W.K., kutaniko la Kikristo lilianzishwa. Akiwa mbinguni, Yesu alianza kutawala juu ya wanafunzi wake watiwa mafuta. (Wakolosai 1:13) Aliwaongoza katika kazi yao ya kuhubiri na kuwatayarisha kwa ajili ya jukumu lao la wakati ujao. Jukumu gani? Wale ambao wangekuwa waaminifu hadi kifo hatimaye wangefufuliwa na kuwa wafalme pamoja na Yesu katika Ufalme.

Mfano mmoja unaopendeza wa mtu ambaye angekuwa mfalme wakati ujao ni Sauli, anayejulikana kwa jina lake la Kiroma, Paulo. Alikuwa Myahudi ambaye kwa muda mrefu alikuwa na bidii kwa ajili ya Sheria ya Mungu, lakini alikuwa amepotoshwa sana na viongozi wa kidini Wayahudi hivi kwamba hata alikubaliana kuwa Stefano apigwe mawe. Kisha Sauli alielekea Damasko ‘akiwatisha wanafunzi wa Bwana akitaka kuwaua.’ Alikuwa amepewa mamlaka na Kuhani Mkuu Kayafa awakamate wanafunzi wa Yesu na kuwaleta Yerusalemu. (Matendo 7:58; 9:1) Hata hivyo, Sauli alipokuwa njiani, nuru kubwa ikamulika kumzunguka naye akaanguka chini.

Sauti ya mtu asiyeonekana ikasema: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?” Sauli akauliza: “Wewe ni nani Bwana?” Akaambiwa: “Mimi ni Yesu, ambaye unamtesa.”—Matendo 9:4, 5.

Yesu alimwambia Sauli aingie Damasko kisha asubiri maagizo zaidi, lakini alihitaji kupelekwa kwenye jiji hilo kwa sababu ile nuru ya ajabu ilikuwa imempofusha. Katika maono mengine, Yesu alimtokea Anania, mmoja wa wanafunzi wake aliyeishi Damasko. Yesu alimwambia Anania aende kwenye nyumba fulani naye atampata Sauli. Anania alisitasita kufanya hivyo, lakini Yesu akamhakikishia hivi: “Mtu huyu ni chombo nilichokichagua ili kupeleka jina langu kwa mataifa na pia kwa wafalme na wana wa Israeli.” Sauli alianza kuona tena, na akiwa huko Damasko “akaanza kuhubiri katika masinagogi kuhusu Yesu, kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu.”—Matendo 9:15, 20.

Kwa msaada wa Yesu, Paulo na waeneza injili wengine waliendeleza kazi ya kuhubiri ambayo Yesu alikuwa ameanzisha. Mungu aliwabariki kwa kuwapatia mafanikio makubwa. Karibu miaka 25 baada ya Yesu kumtokea akiwa njiani kwenda Damasko, Paulo aliandika kwamba habari njema ilikuwa ‘imehubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu.’—Wakolosai 1:23.

Miaka mingi baadaye, Yesu alimpa mtume Yohana aliyempenda mfululizo wa maono, ambayo yanapatikana katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Kupitia maono hayo, kwa kweli Yohana alimwona Yesu akirudi akiwa na mamlaka ya Ufalme. (Yohana 21:22) “Kwa mwongozo wa roho [Yohana alikuja] kuwa katika siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10) Siku hiyo ingeanza lini?

Tunapochunguza unabii wa Biblia kwa makini tunatambua kwamba “siku ya Bwana” ilianza katika nyakati za kisasa. Mwaka wa 1914, vita ambavyo vimejulikana kama Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilianza. Na miaka iliyofuatia imekuwa na vita, magonjwa, njaa, matetemeko ya ardhi, na uthibitisho mwingine unaoonyesha utimizo mkubwa wa “ishara” ambayo Yesu aliwapa mitume wake kuhusu “kuwapo” kwake na “ule mwisho.” (Mathayo 24:3, 7, 8, 14) Sasa kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme haifanywi tu katika eneo la Milki ya Roma, bali duniani kote.

Yohana aliongozwa na roho ya Mungu kufafanua maana ya mambo hayo: “Sasa kumekuwa na wokovu na nguvu na Ufalme wa Mungu wetu na mamlaka ya Kristo wake.” (Ufunuo 12:10) Naam, Ufalme wa Mungu ulio mbinguni, ambao Yesu aliutangaza sana, sasa ni jambo halisi!

Hizo ni habari njema kwa wanafunzi washikamanifu wa Yesu. Wanaweza kuwa na uhakika na maneno haya ya Yohana: “Kwa sababu hiyo furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake! Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:12.

Basi, kwa sasa Yesu haketi tena akisubiri kwenye mkono wa kuume wa Baba yake. Anatawala akiwa Mfalme na hivi karibuni atawaangamiza maadui wake wote. (Waebrania 10:12, 13) Tunasubiri kuona mambo gani yenye kusisimua?