Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 139

Yesu Aleta Paradiso na Kumaliza Mgawo Wake

Yesu Aleta Paradiso na Kumaliza Mgawo Wake

1 WAKORINTHO 15:24-28

  • MATOKEO KWA KONDOO NA MBUZI

  • WENGI WATAFURAHIA PARADISO DUNIANI

  • YESU ATHIBITIKA KUWA NJIA, KWELI, NA UZIMA

Mara tu baada ya kubatizwa, Yesu alikabiliana na adui aliyekuwa ameazimia kumfanya ashindwe hata kabla hajaanza huduma yake. Naam, Ibilisi alimjaribu Yesu tena na tena. Baadaye, Yesu alisema hivi kumhusu mwovu huyo: “Mtawala wa ulimwengu anakuja, naye hana uwezo juu yangu.”—Yohana 14:30.

Mtume Yohana aliona katika maono kile ambacho kingempata ‘yule joka mkubwa, yule nyoka wa zamani, anayeitwa Shetani na Ibilisi.’ Adui huyo mkatili wa wanadamu angetupwa kutoka mbinguni, “akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:9, 12) Wakristo wana kila sababu ya kuamini kwamba wanaishi katika “kipindi [hicho] kifupi cha wakati” na kwamba hivi karibuni ‘yule joka, yule nyoka wa zamani,’ atatupwa katika shimo refu lisilo na mwisho na hatatenda kwa miaka 1,000 Yesu anapotawala katika Ufalme wa Mungu.—Ufunuo 20:1, 2.

Katika kipindi hicho, ni nini kitakachotokea duniani, makao yetu? Ni nani watakaoishi hapa duniani, na kutakuwa na hali gani? Yesu mwenyewe alitoa majibu. Katika mfano wake wa kondoo na mbuzi, alionyesha jinsi itakavyokuwa wakati ujao kwa wanadamu walio kama kondoo, wanaoshirikiana na ndugu za Yesu na kuwatendea mema. Pia, alionyesha wazi jinsi itakavyokuwa wakati ujao kwa wale wanaotenda kinyume, wale walio kama mbuzi. Yesu alisema hivi: “Hao [mbuzi] watakatiliwa mbali milele, lakini waadilifu [kondoo] watapata uzima wa milele.”—Mathayo 25:46.

Hilo linatusaidia kuelewa maneno ambayo Yesu alimwambia mhalifu aliyekuwa ametundikwa kwenye mti kando yake. Yesu hakumwahidi mtu huyo thawabu aliyowaahidi mitume wake waaminifu, yaani, ahadi ya kuwa sehemu ya Ufalme wa mbinguni. Badala yake, Yesu alimwahidi hivi mtenda maovu huyo: “Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Kwa hiyo, mtu huyo alipata tumaini la kuishi katika Paradiso​—bustani maridadi. Inapatana na akili kuamini kwamba leo wale wanaothibitika kuwa kama kondoo na ambao wanaingia “katika uzima wa milele” watakuwa pia katika Paradiso hiyo.

Hilo linapatana na maelezo ambayo mtume Yohana alitoa kuhusu hali zitakazokuwapo wakati huo duniani. Alisema hivi: “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.

Ili mhalifu huyo afurahie uzima katika Paradiso, atahitaji kufufuliwa kutoka kwa wafu. Si yeye tu atakayefufuliwa. Yesu alionyesha wazi jambo hilo aliposema: “Saa inakuja ambayo wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka, wale waliotenda mema kwenye ufufuo wa uzima, na wale waliozoea kutenda maovu kwenye ufufuo wa hukumu.”—Yohana 5:28, 29.

Namna gani mitume waaminifu na idadi kamili ya wale watakaokuwa na Yesu mbinguni? Biblia inasema: “Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka 1,000.” (Ufunuo 20:6) Wale watakaotawala pamoja na Kristo ni wanaume na wanawake watakaotoka duniani. Basi kwa hakika watakuwa watawala mbinguni nao watawatawala wale walio duniani kwa huruma na uelewaji.—Ufunuo 5:10.

Yesu ataitumia dhabihu yake ya fidia kwa ajili ya wanadamu duniani na kuwatoa katika laana ya dhambi waliyorithi. Yeye na watawala wenzake watawasaidia wanadamu waaminifu kufikia ukamilifu. Naam, wakati huo wanadamu watafurahia maisha ambayo mwanzoni Mungu alikusudia wawe nayo alipowaambia Adamu na Hawa waongezeke na kuijaza dunia. Hata kifo kilichosababishwa na dhambi ya Adamu hakitakuwapo tena!

Kwa hiyo, Yesu atakuwa ametimiza mambo yote ambayo Yehova alimwomba afanye. Mwishoni mwa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja, Yesu atamkabidhi Baba yake Ufalme na familia ya wanadamu wakamilifu. Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu tendo hilo la Yesu la unyenyekevu: “Vitu vyote vitakapotiishwa kwake, ndipo Mwana mwenyewe atakapojitiisha pia kwa Yule aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.”—1 Wakorintho 15:28.

Ni wazi kwamba Yesu anatimiza jukumu muhimu katika kutimiza makusudi yenye utukufu ya Mungu. Na makusudi hayo yanapoendelea kutimizwa katika umilele wote, maneno aliyosema kujihusu yatathibitika kikamili kuwa ya kweli: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.”—Yohana 14:6.