Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 70

Yesu Anaponyesha Mwanaume Mwenye Alizaliwa Kipofu

Yesu Anaponyesha Mwanaume Mwenye Alizaliwa Kipofu

YOHANA 9:1-18

  • MUTU MWENYE KUOMBA-OMBA AMBAYE NI KIPOFU TANGU KUZALIWA KWAKE ANAPONYESHWA

Ni siku ya Sabato, na Yesu angali katika Yerusalemu. Wakati yeye na wanafunzi wake wako wanatembea katika muji, wanaona mutu mwenye kuomba-omba mwenye ni kipofu tangu kuzaliwa kwake. Wanafunzi wanamuuliza Yesu: “Rabi, ni nani alitenda zambi, ni mutu huyu ao ni wazazi wake, na hivyo akazaliwa kipofu?”—Yohana 9:2.

Wanafunzi wanajua kama mutu huyo hana nafsi yenye haionekane yenye ilikuwa inaishi mbele azaliwe, lakini pengine wanajiuliza ikiwa mutu anaweza kufanya zambi wakati iko katika tumbo la uzazi la mama yake. Yesu anawajibu hivi: “Mutu huyu hakutenda zambi wala wazazi wake, lakini ilikuwa vile kusudi kazi za Mungu zifikie kufunuliwa kupitia yeye.” (Yohana 9:3) Kwa hiyo, mwanaume huyo ni kipofu, haiko kwa sababu yeye ao wazazi wake walifanya kosa ao zambi fulani. Lakini, kwa sababu ya zambi ya Adamu, wanadamu wote wanazaliwa pasipo kukamilika na kwa hiyo wanapatwa na uzaifu, kama vile kuwa kipofu. Lakini hali ya mwanaume huyo ya kuwa kipofu inapatia Yesu nafasi ya kufunua kazi za Mungu, kama vile alifanya nyakati zingine kwa kuponyesha watu magonjwa yao.

Yesu anakazia kuwa ni jambo la haraka kufanya kazi hizo. Anasema hivi: “Lazima tufanye kazi za Ule mwenye alinituma wakati ingali muchana; usiku unakuja wakati hakuna mutu mwenye anaweza kufanya kazi. Wakati ningali katika ulimwengu, mimi ndiye mwangaza wa ulimwengu.” (Yohana 9:4, 5) Ndiyo, hivi karibuni kifo cha Yesu kitafanya akuwe katika giza la kaburi kwenye hawezi kufanya jambo lolote. Lakini mbele wakati huo ufike, yeye ni mwangaza wa ulimwengu.

Lakini, Yesu atamuponyesha ule kipofu? Na ikiwa atafanya hivyo, namna gani? Yesu anatema mate kwenye udongo na kupitia mate yake anafanya matope. Kisha anakamata matope fulani na kutia katika macho ya kipofu huyo na kumuambia hivi: “Uende unawe katika kiziwa cha maji cha Siloamu.” (Yohana 9:7) Mwanaume huyo anatii. Wakati anafanya hivyo, anaona kabisa! Mwanaume huyo anafurahi sana wakati anaona kwa mara ya kwanza katika maisha yake!

Majirani na watu wengine wenye wanajua kama mutu huyo alikuwa kipofu wanashangaa sana. Wanauliza, “Je, huyu haiko ule mutu mwenye alikuwa anakaa na kuomba-omba?” Wamoja wanajibu, “Ni yeye.” Lakini wengine hawaamini. Kwa hiyo wanasema: “Hapana, lakini anamufanana.” Mwanaume huyo anasema hivi yeye mwenyewe: “Ni mimi.”—Yohana 9:8, 9.

Kwa hiyo, wanamuuliza hivi: “Namna gani basi macho yako yalifunguliwa?” Anajibu hivi: “Mutu mwenye kuitwa Yesu alifanya matope na akayapakaa kwenye macho yangu kisha akaniambia, ‘Uende mupaka Siloamu unawe.’ Basi nikaenda, nikanawa na nikaanza kuona.” Kisha wanamuuliza: “Ule mutu iko wapi?” Anawajibu hivi: “Sijue.”—Yohana 9:10-12.

Watu wanapeleka mwanaume huyo kwenye Wafarisayo wako, wenye pia wanapenda kujua namna macho yake yalifunguliwa. Anawaambia hivi: “Aliweka matope kwenye macho yangu, nikanawa, na ninaona.” Wafarisayo walipaswa kufurahi kuona mwanaume huyo mwenye kuomba-omba anaponyeshwa. Lakini kuliko kufurahi, wamoja wanamulaumu Yesu. Wanasema, “Mutu huyo hakutoka kwa Mungu, kwa maana hashike Sabato.” Lakini wengine wanasema hivi: “Namna gani mutu mwenye ni mutenda-zambi anaweza kufanya alama za namna hiyo?” (Yohana 9:15, 16) Kwa hiyo wanagawanyika.

Kwa sababu wako na maoni yenye kupingana, wanageukia mwanaume mwenye sasa iko anaona na kumuuliza hivi: “Unasema nini juu yake, kwa kuwa ni macho yako ndiyo alifungua?” Hana mashaka juu ya Yesu; kwa hiyo, anawajibu hivi: “Yeye ni nabii.”—Yohana 9:17.

Wayahudi wanakataa kuamini jambo hilo. Pengine wanawaza kuwa Yesu na mwanaume huyo wamefanya mupango fulani ili kudanganya watu. Wanaamua mara moja kama jambo lenye litamaliza ubishi ni kuuliza wazazi wake ikiwa mutoto wao alikuwa kabisa kipofu.