Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 69

Je, Baba Yao Ni Abrahamu au Ni Ibilisi?

Je, Baba Yao Ni Abrahamu au Ni Ibilisi?

YOHANA 8:37-59

  • WAYAHUDI WADAI KWAMBA ABRAHAMU NI BABA YAO

  • YESU ALIKUWAPO KABLA YA ABRAHAMU

Akiwa bado Yerusalemu kwa ajili ya Sherehe ya Vibanda, Yesu anaendelea kufundisha kweli muhimu. Baadhi ya Wayahudi walio hapo wamemwambia: “Sisi ni uzao wa Abrahamu na hatujawahi kuwa watumwa.” Yesu anawajibu: “Ninajua kwamba ninyi ni uzao wa Abrahamu. Lakini mnataka kuniua, kwa sababu neno langu halifanyi maendeleo kati yenu. Ninasema mambo niliyoona nilipokuwa na Baba yangu, lakini ninyi mnafanya mambo mliyosikia kutoka kwa baba yenu.”—Yohana 8:33, 37, 38.

Kwa ufupi Yesu anamaanisha hivi: Kwamba Baba yake ni tofauti na baba yao. Bila kujua anachomaanisha Yesu, Wayahudi wanarudia dai lao: “Baba yetu ni Abrahamu.” (Yohana 8:39; Isaya 41:8) Kihalisi wao ni wazao wake. Basi wanafikiri kwamba wana imani kama ya Abrahamu, rafiki ya Mungu.

Hata hivyo, Yesu anatoa jibu la kushangaza: “Kama mngekuwa watoto wa Abrahamu, mngefanya kazi za Abrahamu.” Kwa kweli, mwana halisi humwiga baba yake. Yesu anaendelea kusema: “Lakini sasa mnataka kuniua, mimi ambaye nimewaambia kweli niliyosikia kutoka kwa Mungu. Abrahamu hakufanya hivyo.” Kisha Yesu anasema maneno haya yanayoshangaza: “Mnafanya kazi za baba yenu.”—Yohana 8:39-41.

Bado Wayahudi hawaelewi Yesu anazungumza kuhusu nani. Wanadai kwamba wao si wana haramu kwa kusema: “Hatukuzaliwa kutokana na uasherati; tuna Baba mmoja tu, Mungu.” Je, kweli Mungu ndiye Baba yao? Yesu anawaambia: “Kama Mungu angekuwa Baba yenu, mngenipenda, kwa maana nilitoka kwa Mungu nami nipo hapa. Sikuja kwa uamuzi wangu mwenyewe, bali Yeye ndiye aliyenituma. Yesu anauliza swali kisha analijibu yeye mwenyewe: “Kwa nini hamwelewi mambo ninayosema? Kwa sababu hamwezi kusikiliza neno langu.”—Yohana 8:41-43.

Yesu amejaribu kuonyesha matokeo ya kumkataa. Lakini sasa anasema hivi moja kwa moja: “Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mnataka kufanya tamaa za baba yenu.” Baba yao yukoje? Yesu anamtambulisha hivi waziwazi: “Alikuwa muuaji alipoanza, naye hakusimama imara katika kweli.” Yesu anaongezea hivi: “Yule anayetoka kwa Mungu husikiliza maneno ya Mungu. Kwa sababu hiyo, ninyi hamsikilizi, kwa kuwa hamtoki kwa Mungu.”—Yohana 8:44, 47.

Shutuma hiyo inawakasirisha Wayahudi, nao wanauliza: “Je, hatusemi kweli tunaposema, ‘Wewe ni Msamaria na una roho mwovu’?” Kwa kumwita Yesu “Msamaria,” wanaonyesha jinsi wanavyomdharau. Lakini Yesu anapuuza matusi yao kwa kusema: “Mimi sina roho mwovu bali ninamheshimu Baba yangu, lakini ninyi mnanivunjia heshima.” Hilo ni jambo zito kwa kuwa Yesu anaahidi hivi: “Yeyote akishika maneno yangu, hataona kifo kamwe.” Hamaanishi kwamba mitume na wengine wanaomfuata hawatakufa kamwe kihalisi. Badala yake, hawatapatwa kamwe na uharibifu wa milele, yaani, “kifo cha pili,” bila tumaini la kufufuliwa.—Yohana 8:48-51; Ufunuo 21:8.

Hata hivyo, Wayahudi wanayaelewa maneno ya Yesu kihalisi, nao wanasema: “Sasa tunajua una roho mwovu. Abrahamu alikufa, na manabii vilevile, lakini wewe unasema, ‘Yeyote akishika maneno yangu hataonja kifo kamwe.’ Wewe si mkuu kuliko Abrahamu baba yetu ambaye alikufa, sivyo? . . . Unafikiri wewe ni nani?”—Yohana 8:52, 53.

Ni wazi Yesu anafundisha kwamba yeye ndiye Masihi. Lakini badala ya kujibu moja kwa moja swali kuhusu utambulisho wake, anasema: “Nikijitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu. Baba yangu ambaye mnasema ni Mungu wenu, ndiye anayenitukuza. Ninyi bado hamjamjua, lakini mimi ninamjua. Kama ningesema simjui, ningekuwa mwongo kama ninyi.”—Yohana 8:54, 55.

Sasa Yesu anarejelea mfano wa babu yao aliyekuwa mwaminifu: “Baba yenu Abrahamu alishangilia sana tazamio la kuona siku yangu, naye aliiona na kushangilia.” Naam, Abrahamu aliamini ahadi ya Mungu, naye alitazamia kuja kwa Masihi. Bila kuamini jambo hilo Wayahudi wanamuuliza: “Wewe hujafika umri wa miaka 50, na bado umemwona Abrahamu?” Yesu anawajibu: “Kwa kweli ninawaambia, mimi nimekuwapo kabla Abrahamu hajakuwapo.” Anazungumzia wakati alipokuwa mbinguni akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu kabla ya kuwa mwanadamu.—Yohana 8:56-58.

Wayahudi wakiwa wamekasirishwa na dai la Yesu kwamba aliishi kabla ya Abrahamu, wanataka kumpiga mawe. Lakini Yesu anaondoka bila kujeruhiwa.