Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA NNE

Yesu Kristo Ni Nani?

Yesu Kristo Ni Nani?

1, 2. (a) Je, kujua tu jina la mtu fulani mashuhuri kunamaanisha unamjua vizuri? Eleza. (b) Watu wana maoni gani yanayotofautiana kumhusu Yesu?

KUNA watu wengi sana mashuhuri ulimwenguni. Huenda unalijua jina la mtu fulani mashuhuri. Hata hivyo, kujua jina lake hakumaanishi kwamba unamjua vizuri. Haimaanishi kwamba unajua kila jambo linalomhusu.

2 Huenda unajua mambo fulani kumhusu Yesu Kristo, ingawa aliishi duniani karibu miaka 2,000 iliyopita. Hata hivyo, watu wengi hawajui alikuwa na utu gani. Wengine wanasema alikuwa mtu mwema, wengine nabii, na wengine waamini kwamba ni Mungu. Wewe una maoni gani?—Soma Maelezo ya Ziada 12.

3. Kwa nini ni muhimu umjue Yehova Mungu na Yesu Kristo?

3 Ni muhimu kujua ukweli kumhusu Yesu. Kwa nini? Biblia inasema: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Kwa kweli, ukijua ukweli kumhusu Yehova na Yesu, unaweza kuishi milele katika dunia paradiso. (Yohana 14:6) Pia, kumjua Yesu kutakusaidia kwa sababu ametuwekea mfano bora wa jinsi ya kuishi na kuwatendea wengine. (Yohana 13:34, 35) Katika Sura ya kwanza, tulijifunza ukweli kumhusu Mungu. Sasa tutajifunza yale ambayo Biblia inafundisha kumhusu Yesu.

TUMEMPATA MASIHI!

4. Maneno “Masihi” na “Kristo” yanaonyesha nini?

4 Miaka mingi kabla Yesu hajazaliwa, Yehova aliahidi katika Biblia kwamba angemtuma Masihi, au Kristo. Neno “Masihi” linatokana na lugha ya Kiebrania, na neno “Kristo” linatokana na lugha ya Kigiriki. Majina hayo yanaonyesha kwamba Mungu angemchagua Masihi na kumpa cheo cha pekee. Masihi atatimiza ahadi zote za Mungu. Hata sasa, Yesu anaweza kukusaidia. Hata hivyo, kabla Yesu hajazaliwa, watu wengi walijiuliza, ‘Ni nani atakayekuwa Masihi?’

5. Je, wanafunzi wa Yesu waliamini kwamba Yesu alikuwa Masihi?

5 Wanafunzi wa Yesu hawakuwa na shaka kwamba alikuwa Masihi. (Yohana 1:41) Kwa mfano, Simoni Petro alimwambia hivi Yesu: “Wewe ndiye Kristo.” (Mathayo 16:16) Tuna uhakika gani kwamba Yesu ndiye Masihi?

6. Yehova alifanya nini ili kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu wamtambue Masihi?

6 Miaka mingi kabla Yesu hajazaliwa, manabii wa Mungu waliandika habari nyingi ambazo zingewasaidia watu kumtambua Masihi. Kwa nini habari hizo ni muhimu? Tuseme umeombwa uende kwenye kituo cha basi kumpokea mtu ambaye hujawahi kumwona. Bila shaka, unaweza kumtambua ikiwa umepewa maelezo ya kutosha kumhusu. Vivyo hivyo, Yehova aliwatumia manabii wake waandike mambo ambayo Masihi angefanya na yale ambayo yangempata. Kutimia kwa unabii huo kunawasaidia watu wenye mioyo minyoofu kujua kwamba Yesu ndiye Masihi.

7. Ni mifano gani miwili ya unabii inayothibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi?

7 Fikiria mifano miwili. Kwanza, miaka 700 kabla Yesu hajazaliwa, Mika alitabiri kwamba Masihi angezaliwa katika mji mdogo wa Bethlehemu. (Mika 5:2) Hivyo ndivyo ilivyokuwa! (Mathayo 2:1, 3-9) Pili, nabii Danieli alitabiri kwamba Yesu angekuwa Masihi mwaka wa 29 W.K. (Danieli 9:25) Hiyo ni mifano miwili tu ya unabii ambao unathibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa.—Soma Maelezo ya Ziada 13.

Baada ya kubatizwa, Yesu akawa Masihi au Kristo

8, 9. Ni mambo gani yaliyotukia Yesu alipobatizwa ambayo yanathibitisha kwamba yeye ndiye Masihi?

8 Yehova alifunua waziwazi kwamba Yesu ndiye Masihi. Mungu aliahidi kumpa Yohana Mbatizaji ishara ili amtambue Masihi. Yohana aliona ishara hiyo, Yesu alipomwendea ili abatizwe katika mto Yordani mwaka wa 29 W.K. Biblia inatuambia mambo yaliyotukia: “Baada ya kubatizwa, mara moja Yesu akainuka kutoka katika maji; na tazama! mbingu zikafunguliwa, naye akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu yake. Tazama! Pia, sauti ikasikika kutoka mbinguni ikisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.’” (Mathayo 3:16, 17) Yohana aliposikia na kuona ishara hiyo, alitambua kwamba Yesu ndiye Masihi. (Yohana 1:32-34) Yehova alipomimina roho yake juu ya Yesu, siku hiyohiyo Yesu akawa Masihi. Akawa Kiongozi na Mfalme aliyechaguliwa na Mungu.—Isaya 55:4.

9 Unabii wa Biblia, maneno ya Yehova mwenyewe, na ishara iliyotokea Yesu alipokuwa akibatizwa ni uthibitisho kwamba Yesu ndiye Masihi. Lakini Yesu alitoka wapi na alikuwa na utu gani? Acheni tuone jinsi Biblia inavyosema.

YESU ALITOKA WAPI?

10. Biblia inafundisha nini kuhusu maisha ya Yesu kabla ya kuja duniani?

10 Biblia inafundisha kwamba Yesu aliishi mbinguni miaka mingi kabla ya kuja duniani. Mika alisema kwamba Masihi ni wa “tangu nyakati za kale.” (Mika 5:2) Mara nyingi Yesu mwenyewe alisema kwamba aliishi mbinguni kabla hajazaliwa akiwa mwanadamu. (Soma Yohana 3:13; 6:38, 62; 17:4, 5.) Hata kabla ya kuja duniani, Yesu alikuwa na uhusiano wa pekee na Yehova.

11. Kwa nini Yehova anampenda Yesu?

11 Yehova anampenda Yesu sana. Kwa nini? Kwa sababu Mungu alimuumba kwanza kabla hajaumba vitu vingine vyote. Kwa hiyo, Yesu anaitwa “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” * (Wakolosai 1:15) Pia, Yehova anampenda sana Yesu kwa kuwa Yesu pekee ndiye aliyeumbwa moja kwa moja na Yehova. Hiyo ndiyo sababu anaitwa “Mwana wake mzaliwa pekee.” (Yohana 3:16) Pia, Yesu pekee ndiye aliyetumiwa na Yehova kuumba vitu vingine vyote. (Wakolosai 1:16) Yesu peke yake anaitwa “Neno,” kwa sababu Yehova alimtumia kuwapa ujumbe na maagizo malaika na wanadamu.—Yohana 1:14.

12. Tunajuaje kwamba Yesu na Mungu hawako sawa?

12 Baadhi ya watu wanaamini kwamba Yesu ni sawa na Mungu Mweza-Yote. Lakini Biblia haifundishi hivyo. Biblia inafundisha kwamba Yesu aliumbwa. Jambo hilo linamaanisha kwamba alikuwa na mwanzo. Lakini Yehova aliyeumba vitu vyote hana mwanzo. (Zaburi 90:2) Akiwa Mwana wa Mungu, Yesu hakujaribu kamwe kujilinganisha na Mungu. Biblia inafundisha wazi kwamba Baba ni mkuu kuliko Mwana. (Soma Yohana 14:28; 1 Wakorintho 11:3.) Yehova peke yake ndiye “Mungu Mweza-Yote.” (Mwanzo 17:1) Yeye ndiye mkuu na mwenye nguvu katika ulimwengu wote mzima.—Soma Maelezo ya Ziada 14.

13. Kwa nini Biblia inasema Yesu ni “mfano wa Mungu asiyeonekana”?

13 Yehova na Mwana wake, Yesu, walifanya kazi kwa ukaribu kwa miaka mingi kabla ya kuumbwa kwa mbingu na dunia. Ni lazima walipendana sana! (Yohana 3:35; 14:31) Yesu aliiga sifa za baba yake kikamilifu hivi kwamba Biblia inamwita “mfano wa Mungu asiyeonekana.”—Wakolosai 1:15.

14. Mwana mpendwa wa Yehova alizaliwa akiwa mwanadamu jinsi gani?

14 Mwana mpendwa wa Yehova alikuwa tayari kuondoka mbinguni na kuzaliwa duniani akiwa mwanadamu. Iliwezekanaje? Yehova alimhamisha kimuujiza Mwana wake kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira aliyeitwa Maria. Kwa hiyo, Yesu hakuwa na baba wa kibinadamu. Hivyo, Maria alimzaa mwana mkamilifu, na akamwita jina Yesu.—Luka 1:30-35.

YESU ALIKUWA NA UTU GANI?

15. Unawezaje kumjua vizuri Yehova?

15 Unaweza kujifunza mengi zaidi kuhusu Yesu, maisha yake, na sifa zake kwa kusoma vitabu vya Biblia vya Mathayo, Marko, Luka na Yohana. Vitabu hivyo vinaitwa Injili. Kwa kuwa Yesu ana sifa kama za Baba yake, mambo utakayosoma yatakusaidia kumjua vizuri Yehova. Ndiyo sababu Yesu alisema: “Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yohana 14:9.

16. Yesu alifundisha kuhusu nini? Mafundisho ya Yesu yalitoka wapi?

16 Watu wengi walimwita Yesu “Mwalimu.” (Yohana 1:38; 13:13) Jambo muhimu ambalo Yesu alifundisha lilikuwa “habari njema ya Ufalme.” Ufalme huo ni nini? Ni serikali ya Mungu iliyo mbinguni itakayotawala ulimwengu mzima na kuwaletea baraka watu wanaomtii Mungu. (Mathayo 4:23) Kila jambo ambalo Yesu alifundisha lilitoka kwa Yehova. Yesu alisema: “Mambo ninayofundisha si yangu, bali ni ya yule aliyenituma.” (Yohana 7:16) Yesu alijua kwamba Yehova anataka watu wasikie habari njema kwamba Ufalme wa Mungu utatawala ulimwengu mzima.

17. Yesu alifundisha wapi? Kwa nini Yesu aliwafundisha watu kwa bidii sana?

17 Yesu alifundisha wapi? Kila mahali penye watu. Alifundisha vijijini, mijini, sokoni, sehemu za ibada na kwenye nyumba za watu. Hakusubiri watu wamfuate. Aliwafuata walipokuwa. (Marko 6:56; Luka 19:5, 6) Yesu alikuwa na bidii sana, alitumia nguvu na wakati mwingi kuwafundisha watu. Kwa nini? Kwa sababu alijua kwamba Mungu alitaka afanye hivyo na sikuzote alimtii Baba yake. (Yohana 8:28, 29) Pia, Yesu alihubiri kwa sababu aliwasikitikia watu. (Soma Mathayo 9:35, 36.) Viongozi wa dini hawakufundisha watu ukweli kumhusu Mungu na Ufalme wake. Hivyo, alitaka kuwasaidia watu wengi wasikie habari njema.

18. Ni sifa gani za Yesu zinazokuvutia?

18 Yesu aliwapenda na kuwajali watu. Alikuwa mwenye fadhili na urafiki. Hata watoto walipenda kuwa karibu naye. (Marko 10:13-16) Yesu alipenda haki. Alichukia ufisadi na ukosefu wa haki. (Mathayo 21:12, 13) Aliishi wakati ambao wanawake walidharauliwa na kunyimwa baadhi ya haki zao. Lakini sikuzote Yesu aliwaheshimu na kuwastahi wanawake. (Yohana 4:9, 27) Pia, Yesu alikuwa mnyenyekevu sana. Kwa mfano, siku moja aliwaosha wanafunzi wake miguu, jambo ambalo kwa kawaida lilifanywa na watumwa.—Yohana 13:2-5, 12-17.

Yesu alihubiri mahali popote penye watu

19. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Yesu alijua mahitaji ya watu na kwamba alitaka kuwasaidia?

19 Yesu alijua mahitaji ya watu, na alitaka kuwasaidia. Jambo hilo lilionekana waziwazi alipotumia nguvu za Mungu kuwaponya kimuujiza. (Mathayo 14:14) Kwa mfano, mwanamume mwenye ukoma alimwendea Yesu na kumwambia: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Ndipo akamsikitikia, akanyoosha mkono wake akamgusa na kumwambia: “Ninataka. Takasika.” Mwanamume huyo akapona! (Marko 1:40-42) Unafikiri mwanamume huyo alihisije?

SIKUZOTE ALIKUWA MWAMINIFU KWA BABA YAKE

20, 21. Yesu ametuwekeaje mfano bora wa kumtii Mungu?

20 Yesu aliweka mfano bora wa kumtii Mungu. Licha ya hali yoyote au kutendewa vibaya na maadui wake, aliendelea kuwa mwaminifu kwa Baba yake. Kwa mfano, Yesu hakutenda dhambi Shetani alipomjaribu. (Mathayo 4:1-11) Baadhi ya watu wa familia yake hawakuamini kwamba alikuwa Masihi, hata walisema kwamba “amerukwa na akili.” Hata hivyo, Yesu aliendelea kufanya kazi ya Mungu. (Marko 3:21) Alipotendewa kikatili na adui zake, Yesu aliendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu na hakujaribu kuwadhuru.—1 Petro 2:21-23.

21 Hata alipokabili kifo cha kikatili na maumivu makali, Yesu aliendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova. (Soma Wafilipi 2:8.) Wazia jinsi alivyohitaji kuvumilia siku aliyokufa. Alikamatwa, akashtakiwa na mashahidi wa uwongo, akahukumiwa na mahakimu wenye ufisadi, akachekwa na umati, akateswa na askari, kisha wakamtundika kwenye mti wa mateso. Alipokuwa anakufa alipaza sauti: “Imetimizwa!” (Yohana 19:30) Siku tatu baada ya Yesu kufa, Yehova alimfufua na kumfanya hai katika roho. (1 Petro 3:18) Majuma machache baadaye, alirudi mbinguni, na “kuketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu,” akingojea Mungu amweke rasmi kuwa Mfalme.—Waebrania 10:12, 13.

22. Ni fursa gani tunayopata kwa sababu Yesu alikuwa mwaminifu kwa Baba yake?

22 Kwa kuwa Yesu aliendelea kuwa mwaminifu kwa Baba yake, sasa tuna fursa ya kuishi milele katika dunia paradiso, kama tu Yehova alivyoahidi. Katika sura inayofuata, tutazungumzia jinsi kifo cha Yesu kinavyotuwezesha kupata uzima wa milele.

^ fu. 11 Yehova anaitwa Baba kwa sababu yeye ni Muumba. (Isaya 64:8) Yesu anaitwa Mwana wa Mungu kwa sababu aliumbwa na Yehova. Pia, malaika na Adamu, wanaitwa wana wa Mungu.—Ayubu 1:6; Luka 3:38.