Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA SABA

Kutakuwa na Ufufuo!

Kutakuwa na Ufufuo!

1-3. Sote tumehukumiwa nini, na Yehova atatuwekaje huru?

WAZIA kwamba umehukumiwa kifungo cha maisha kwa kosa ambalo hukutenda. Hakuna uwezekano wa kuachiliwa huru. Umekata tamaa, na huna la kufanya. Hata hivyo, ukiwa umekata tamaa kabisa, unagundua kwamba mtu fulani ana uwezo wa kukuweka huru na hata ameahidi kukusaidia! Utahisije?

2 Sote tumehukumiwa kifo. Hata tufanye nini, hatuwezi kukiepuka. Hata hivyo, Yehova ana nguvu za kutuweka huru kutokana na kifo. Ameahidi kwamba “adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”—1 Wakorintho 15:26.

3 Wazia jinsi utakavyohisi wakati ambao watu hawatakufa! Yehova hataondoa kifo tu, bali atawafufua wale ambao wamekufa. Fikiria jinsi mambo yatakavyokuwa. Anaahidi kwamba “waliokufa ambao hawana uwezo” wataishi. (Isaya 26:19) Katika Biblia tukio hilo linaitwa ufufuo.

MPENDWA WETU AKIFA

4. (a) Tunaweza kupata wapi faraja mtu wa familia au rafiki akifa? (b) Baadhi ya rafiki za Yesu wa karibu walikuwa nani?

4 Mtu wa familia au rafiki wa karibu akifa, sisi hulemewa na uchungu na huzuni. Tunahisi hatuna msaada. Hatuna uwezo wa kumrudishia uhai. Lakini tunaweza kupata faraja ya kweli katika Biblia. (Soma 2 Wakorintho 1:3, 4.) Acheni tuone mfano unaoonyesha kwamba Yehova na Yesu wanatamani kuwafufua wapendwa wetu. Yesu alipokuwa duniani, mara nyingi alimtembelea Lazaro na dada zake, Martha na Maria. Wote watatu walikuwa marafiki wazuri wa Yesu. Biblia inasema: “Yesu aliwapenda Martha na dada yake na Lazaro.” Lakini siku moja Lazaro alikufa.—Yohana 11:3-5.

5, 6. (a) Yesu alifanya nini alipoona familia na marafiki wa Lazaro wakiomboleza? (b) Kwa nini inafariji kujua jinsi Yesu alivyohisi kuhusu kifo?

5 Yesu alienda kuwafariji Martha na Maria. Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alienda jijini kumpokea. Alifurahi kumwona Yesu, lakini akamwambia: “kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.” Martha alifikiri Yesu amechelewa. Kisha, Yesu akamwona Maria akilia. Alipoona huzuni yao aliumia moyoni naye akalia. (Yohana 11:21, 33, 35) Aliumia sana kama vile tunavyohisi tunapofiwa na mtu tunayempenda.

6 Tunafarijika tunapojua kwamba Yesu ana hisia kama zetu kuhusu kifo. Yesu ana sifa kama za Baba yake. (Yohana 14:9) Yehova ana uwezo wa kuondoa kifo na atafanya hivyo hivi karibuni.

“LAZARO, NJOO HUKU NJE!”

7, 8. Kwa nini Martha hakutaka jiwe liondolewe kwenye kaburi la Lazaro, lakini Yesu alifanya nini?

7 Yesu alipofika kwenye kaburi ambalo Lazaro alikuwa amezikwa, mwingilio ulikuwa umefunikwa kwa jiwe kubwa. Yesu akawaambia: “Liondoeni jiwe.” Lakini Martha akapinga. Mwili wa Lazaro ulikuwa kaburini kwa siku nne. (Yohana 11:39) Hakujua kile ambacho Yesu alitaka kufanya ili kumsaidia ndugu yake.

Wazia shangwe waliyohisi familia ya Lazaro alipofufuliwa!​—Yohana 11:38-44

8 Yesu akamwambia Lazaro: “Njoo huku nje!” Martha na Maria walishangaa sana. “Mtu huyo aliyekuwa amekufa akatoka, miguu na mikono yake ikiwa imefungwa kwa vitambaa.” (Yohana 11:43, 44) Lazaro akawa hai tena! Aliungana tena na familia na rafiki zake. Wangeweza kumkumbatia, kumshika, na kuzungumza naye. Huo ulikuwa muujiza mkubwa sana! Yesu alikuwa amemfufua Lazaro.

“MSICHANA MDOGO, NINAKUAMBIA, ‘INUKA!’”

9, 10. (a) Ni nani aliyempa Yesu nguvu za kufufua wafu? (b) Kwa nini masimulizi ya ufufuo ni muhimu sana kwetu?

9 Je, Yesu aliwafufua wafu kwa nguvu zake? Hapana. Yesu alimwomba Yehova ampe nguvu kabla ya kumfufua Lazaro. (Soma Yohana 11:41, 42.) Si Lazaro peke yake aliyefufuliwa. Biblia inatueleza kuhusu msichana mwenye umri wa miaka 12 aliyekuwa mgonjwa sana. Baba yake, Yairo, alikuwa amekata tamaa, akamsihi Yesu amponye. Alikuwa mtoto wake wa pekee. Alipokuwa akizungumza na Yesu, wanaume fulani walikuja na kusema: “Binti yako amekufa! Kwa nini uendelee kumsumbua Mwalimu?” Lakini Yesu akamwambia Yairo: “Usiogope, uwe tu na imani, naye ataokolewa.” Kisha wakaenda nyumbani kwa Yairo. Walipokuwa wakikaribia nyumbani kwa Yairo, Yesu akaona na kusikia watu wakilia. Yesu akawaambia: “Acheni kulia, kwa maana hajafa bali amelala usingizi.” Lazima wazazi wa binti huyo walishangazwa sana na maneno ya Yesu. Yesu akaamuru watu wote waondoke kisha akaenda pamoja na wazazi wa binti hadi mahali binti alipolazwa, akamshika mkono na kumwita, akisema: “Msichana mdogo, ninakuambia, ‘Inuka!” Wazia shangwe waliyohisi wazazi wake alipoinuka na kuanza kutembea! Yesu alikuwa amemfufua binti yao. (Marko 5:22-24, 35-42; Luka 8:49-56) Kuanzia wakati huo na kuendelea kila walipomtazama binti yao, wangekumbuka jambo ambalo Yehova aliwatendea kupitia Yesu. *

10 Watu ambao Yesu aliwafufua walikufa tena baadaye. Lakini mambo tunayosoma kuwahusu ni muhimu sana kwetu kwa sababu yanatupa tumaini hakika. Yehova anatamani kuwafufua watu na atafanya hivyo.

MAMBO TUNAYOJIFUNZA KUTOKANA NA MASIMULIZI YA UFUFUO

Mtume Petro alimfufua mwanamke Mkristo Dorkasi.​—Matendo 9:36-42

Eliya alimfufua mwana wa mjane.​—1 Wafalme 17:17-24

11. Kifo cha Lazaro kinathibitishaje ukweli wa andiko la Mhubiri 9:5?

11 Biblia inasema waziwazi kwamba “waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.” Kifo cha Lazaro kilithibitisha ukweli huo. (Mhubiri 9:5) Kama Yesu alivyosema, ni kana kwamba Lazaro alikuwa amelala usingizi tu. (Yohana 11:11) Alipokuwa kaburini Lazaro hakujua “jambo lolote kamwe.”

12. Tunajuaje kwamba ufufuo wa Lazaro ulitukia?

12 Yesu alimfufua Lazaro mbele ya watu wengi. Hata maadui wa Yesu walijua kwamba alifanya muujiza huo. Lazaro alikuwa hai tena na hilo lilithibitisha waziwazi kwamba ufufuo huo ulitukia. (Yohana 11:47) Pia, watu wengi walimtembelea Lazaro nao wakaanza kuamini kwamba Yesu alitumwa na Mungu. Jambo hilo liliwachukiza adui za Yesu, hivyo wakapanga kumuua Yesu na Lazaro.—Yohana 11:53; 12: 9-11.

13. Kwa nini tuwe na uhakika kwamba Yehova atawafufua wafu?

13 Yesu alisema kwamba “wote walio katika makaburi ya ukumbusho” watafufuliwa. (Yohana 5:28) Jambo hilo linamaanisha kwamba watu wote ambao Yehova anawakumbuka watafufuliwa. Lakini ili Yehova amfufue mtu, anahitaji kukumbuka kila kitu kuhusu mtu huyo. Je, kweli anaweza kukumbuka? Kuna mabilioni ya nyota angani. Biblia inasema kwamba Yehova anajua majina ya nyota hizo zote. (Soma Isaya 40:26.) Kama anaweza kukumbuka jina la kila nyota, ni wazi kwamba atakumbuka kwa urahisi kila kitu kuhusu wale ambao atawafufua. Zaidi ya yote, Yehova aliumba kila kitu. Kwa hiyo, tuna uhakika kwamba ana uwezo wa kuwafufua wafu.

14, 15. Tunajifunza nini kutokana na maneno ya Ayubu kuhusu ufufuo?

14 Ayubu, aliyekuwa mwaminifu, aliamini ufufuo. Aliuliza hivi: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Kisha akamwambia Yehova: “Utaita, nami nitakujibu. Utaitamani sana kazi ya mikono yako.” Kwa kweli, Ayubu alijua kwamba Yehova anatamani sana kuwafufua watu wakati ujao.—Ayubu 14:13-15.

15 Unahisije kuhusu tumaini la ufufuo? Huenda ukajiuliza, ‘Je, ndugu na rafiki zangu waliokufa watafufuliwa?’ Tunafarijika kujua kwamba Yehova anatamani sana kuwafufua wafu. Acheni tuchunguze jinsi Biblia inavyosema kuhusu wale watakaofufuliwa na mahali watakapoishi.

“WATAISIKIA SAUTI YAKE NA KUTOKA”

16. Wale watakaofufuliwa wataishi maisha ya aina gani?

16 Zamani, wale ambao walifufuliwa waliungana na familia na marafiki zao tena duniani. Jambo hilo litatukia pia wakati ujao, lakini kwa njia bora hata zaidi. Kwa nini? Kwa sababu wale watakaofufuliwa watapata nafasi ya kuishi milele duniani na hawatakufa tena kamwe. Pia, wataishi katika dunia iliyo tofauti sana na leo. Hakutakuwa na vita, uhalifu, na magonjwa.

17. Ni nani watakaofufuliwa?

17 Ni nani watakaofufuliwa? Yesu alisema kwamba “wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Pia, andiko la Ufunuo 20:13 linasema: “Na bahari ikawatoa wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na Kaburi vikawatoa wafu waliokuwa ndani yake.” Ndiyo, mabilioni ya watu watakuwa hai tena. Mtume Paulo alisema kwamba “waadilifu na wasio waadilifu” watafufuliwa. (Soma Matendo 24:15.) Alimaanisha nini?

Katika Paradiso, wafu watafufuliwa na kuungana na wapendwa wao

18. “Waadilifu” watakaofufuliwa ni nani?

18 “Waadilifu” wanatia ndani watumishi waaminifu wa Yehova walioishi kabla ya Yesu kuja duniani. Watu kama Noa, Abrahamu, Sara, Musa, Ruthu, na Esta watafufuliwa waishi hapa duniani. Unaweza kusoma kuhusu baadhi ya wanaume na wanawake hao katika Waebrania sura ya 11. Vipi kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova wanaokufa katika siku zetu? Wao pia ni “waadilifu,” kwa hiyo watafufuliwa.

19. “Wasio waadilifu” ni nani? Yehova atawapa fursa gani?

19 “Wasio waadilifu” ni mabilioni ya watu ambao hawakupata fursa ya kujifunza kumhusu Yehova. Ingawa walikufa, Yehova hajawasahau. Atawafufua, na kuwapa fursa ya kujifunza kumhusu na kumtumikia.

20. Kwa nini si watu wote watakaofufuliwa?

20 Je, hilo linamaanisha kwamba kila mtu aliyekufa atafufuliwa? Hapana. Yesu alisema kwamba baadhi ya watu hawatafufuliwa. (Luka 12:5) Ni nani atakayeamua ikiwa mtu anastahili kufufuliwa au la? Yehova ndiye mwamuzi mkuu, lakini amempa pia Yesu mamlaka ya “kuwa mwamuzi wa walio hai na wafu.” (Matendo 10:42) Wote watakaohukumiwa kuwa waovu hawatafufuliwa.—Soma Maelezo ya Ziada 19.

WANAOFUFULIWA KWENDA MBINGUNI

21, 22. (a) Wale watakaofufuliwa kwenda mbinguni watakuwa na mwili gani? (b) Ni nani aliyekuwa wa kwanza kupata ufufuo wa mbinguni?

21 Biblia inatuambia pia kwamba baadhi ya watu wataishi mbinguni. Watu wanaofufuliwa kwenda mbinguni, hawafufuliwi na mwili wa nyama. Wanafufuliwa wakaishi mbinguni wakiwa na mwili wa roho.

22 Yesu alikuwa mwanadamu wa kwanza kupata ufufuo huo. (Yohana 3:13) Yehova alimfufua Yesu siku tatu baada ya kifo chake. (Zaburi 16:10; Matendo 13:34, 35) Yesu hakufufuliwa akiwa na mwili wa kibinadamu. Mtume Petro anaeleza kwamba “aliuawa katika mwili, lakini akafanywa kuwa hai katika roho.” (1 Petro 3:18) Yesu alifufuliwa akiwa mtu wa roho mwenye nguvu! (1 Wakorintho 15:3-6) Hata hivyo, Biblia inasema kwamba hatakuwa peke yake.

23, 24. “Kundi dogo” ambalo Yesu alizungumzia ni nani na ni wangapi?

23 Kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake waaminifu: “Ninaenda zangu kuwatayarishia mahali.” (Yohana 14:2) Jambo hilo linamaanisha kwamba baadhi ya wafuasi wake wangefufuliwa ili waishi pamoja naye mbinguni. Ni wangapi? Yesu alisema kwamba wangekuwa wachache tu, “kundi dogo.” (Luka 12:32) Mtume Yohana aliona idadi kamili alipomwona Yesu akiwa “amesimama juu ya Mlima Sayuni [mbinguni], na pamoja naye 144,000.”—Ufunuo 14:1.

24 Wakristo 144,000 walianza kufufuliwa lini? Biblia inaeleza kwamba ufufuo huo ungeanza baada ya Yesu kuanza kutawala mbinguni. (1 Wakorintho 15:23) Sasa tunaishi katika kipindi hicho, wengi kati ya hao 144,000 tayari wamefufuliwa kwenda mbinguni. Wale waliobaki duniani hufufuliwa mara tu baada ya kufa ili wakaishi mbinguni. Hata hivyo, watu wengi watafufuliwa wakati ujao ili waishi katika Paradiso duniani.

25. Tutajifunza nini katika sura inayofuata?

25 Hivi karibuni, Yehova atawaweka wanadamu wote huru kutokana na kifo, na hakitakuwapo tena! (Soma Isaya 25:8.) Hata hivyo, wale wanaofufuliwa kwenda mbinguni watafanya nini huko? Biblia inaeleza kwamba watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme wa Mungu. Tutajifunza mengi kuhusu ufalme huo katika sura inayofuata.

^ fu. 9 Katika masimulizi mengine, Biblia inatueleza kuhusu ufufuo wa vijana na watu wazima, wanaume na wanawake, Waisraeli na wakaaji wageni. Unaweza kusoma masimulizi hayo katika 1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37; 13:20, 21; Mathayo 28:5-7; Luka 7:11-17; 8:40-56; Matendo 9:36-42; 20:7-12.