Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA TISA

Je, Mwisho wa Dunia Uko Karibu?

Je, Mwisho wa Dunia Uko Karibu?

1. Ni nani anayeweza kutabiri mambo ya wakati ujao?

UMEWAHI kusikiliza taarifa ya habari na kujiuliza hivi, ‘Kwa nini mambo yanazidi kuwa mabaya?’ Dunia imejaa majanga na ukatili unaofanya baadhi ya watu waamini kwamba lazima mwisho wa dunia uwe karibu sana. Je, kweli mwisho uko karibu? Je, inawezekana kujua jambo hilo? Bila shaka, inawezekana. Wanadamu hawawezi kutabiri mambo ya wakati ujao. Ni Yehova Mungu peke yake anayeweza kutabiri. Katika Biblia, anatueleza kuhusu wakati ujao wa dunia na wanadamu.—Isaya 46:10; Yakobo 4:14.

2, 3. Wanafunzi wa Yesu walitamani kujua nini, na Yesu aliwaambiaje?

2 Mwisho wa dunia unaotajwa katika Biblia, unamaanisha mwisho wa uovu wala si kuharibiwa kwa sayari yetu, dunia. Yesu aliwafundisha watu kwamba Ufalme wa Mungu utaitawala dunia. (Luka 4:43) Wanafunzi wa Yesu walitamani kujua ni lini Ufalme wa Mungu ungekuja, nao walimuuliza Yesu hivi: “Mambo haya yatakuwa lini, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Yesu hakutaja siku hususa, lakini aliwaeleza mambo ambayo yangetukia kabla ya mwisho wa dunia. Mambo ambayo Yesu alitabiri yanatukia katika siku zetu.

3 Katika sura hii tutachunguza mambo yanayothibitisha kwamba tunaishi katika siku za mwisho. Kwanza, tunahitaji kujifunza kuhusu vita iliyotokea mbinguni, ambayo imesababisha mambo yawe mabaya duniani.

VITA MBINGUNI

4, 5. (a) Ni jambo gani lililotukia mbinguni baada ya Yesu kuwa Mfalme? (b) Kulingana na Ufunuo 12:12, ni jambo gani lingetukia baada ya Shetani kutupwa duniani?

4 Katika Sura ya 8 tulijifunza kwamba Yesu aliwekwa rasmi kuwa Mfalme mbinguni mwaka 1914. (Danieli 7:13, 14) Kitabu cha Ufunuo kinasimulia mambo yaliyotokea: “Vita vikatokea ghafla mbinguni: Mikaeli [Yesu] na malaika zake wakapigana na yule joka [Shetani], naye joka na malaika zake wakapigana nao.” * Shetani na malaika zake walishindwa nao wakatupwa duniani. Hebu wazia jinsi malaika walivyoshangilia! Lakini namna gani kuhusu wanadamu duniani? Biblia inasema kwamba hicho kingekuwa kipindi cha taabu kwa wanadamu. Kwa nini? Kwa sababu Ibilisi ana hasira kali, “akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:7, 9, 12.

5 Ibilisi amesababisha matatizo mengi duniani. Ana hasira kali kwa sababu ana kipindi kifupi cha wakati kabla Mungu hajamwangamiza. Acheni sasa tuchunguze mambo ambayo Yesu alisema yangetokea katika siku za mwisho.—Soma Maelezo ya Ziada 24.

SIKU ZA MWISHO

6, 7. Vita na njaa vimesababisha nini ulimwenguni?

6 Vita. Yesu alisema: “Taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Katika siku zetu watu wengi wamekufa vitani kuliko wakati mwingine wowote katika historia. Ripoti ya shirika fulani (Worldwatch) inasema kwamba watu zaidi ya milioni mia moja wameuawa vitani tangu mwaka wa 1914. Idadi ya watu waliouawa vitani kwa kipindi cha miaka mia moja tangu mwaka wa 1900 hadi 2000 ni mara tatu zaidi ya idadi ya watu waliouawa kabla ya mwaka wa 1900. Hebu wazia uchungu na mateso ambayo watu wengi wamepata kutokana na vita!

7 Njaa. Yesu alisema: “Kutakuwa na upungufu wa chakula.” (Mathayo 24:7) Ingawa kuna chakula kingi kuliko wakati mwingine wowote, watu wengi hawapati chakula cha kutosha. Kwa nini? Kwa sababu hawana pesa za kutosha kununua chakula au mashamba ya kukuza chakula. Zaidi ya watu bilioni moja ulimwenguni ni maskini hohehahe. Shirika la Afya Ulimwenguni linasema kwamba mamilioni ya watoto hufa kila mwaka kwa sababu ya utapiamlo.

8, 9. Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba unabii wa Yesu kuhusu matetemeko na magonjwa unatimia?

8 Matetemeko ya Ardhi. Yesu alitabiri hivi: “Kutakuwa na matetemeko makubwa ya ardhi.” (Luka 21:11) Matetemeko makubwa ya ardhi hutokea kila mwaka. Tangu mwaka 1900, zaidi ya watu milioni mbili wamekufa kwa sababu ya matetemeko. Ingawa teknolojia imesaidia kugundua matetemeko kabla ya kutokea, bado matetemeko yameua watu wengi.

9 Magonjwa. Yesu alitabiri kwamba kungekuwa na “magonjwa.” Magonjwa hatari yanaenea kwa haraka na kuua watu wengi. (Luka 21:11) Ingawa madaktari wamejifunza kutibu magonjwa mengi, bado kuna baadhi ya magonjwa ambayo hayatibiki. Ripoti moja inasema kwamba kila mwaka watu wengi wanakufa kutokana na magonjwa kama vile kifua kikuu, malaria, na kipindupindu. Zaidi ya hayo, madaktari wamegundua magonjwa mapya zaidi ya 30 na baadhi ya magonjwa hayo hayana tiba.

WATU WA SIKU ZA MWISHO

10. Unabii wa 2 Timotheo 3:1-5 unatimiaje leo?

10 Andiko la 2 Timotheo 3:1-5 linasema hivi: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Mtume Paulo alieleza jinsi ambavyo watu wengi wangetenda katika siku za mwisho. Alisema watu wangekuwa

  • wenye kujipenda wenyewe

  • wenye kupenda pesa

  • wasiotii wazazi

  • wasio washikamanifu

  • wasio na upendo wa asili

  • wasiojizuia

  • wakali

  • wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu

  • wakionekana kama watu wanaomwogopa Mungu lakini wakizikana nguvu zake

11. Kulingana na Zaburi 92:7, ni jambo gani litakalowapata watu waovu?

11 Je, hivyo ndivyo watu walivyo katika eneo unaloishi? Hali iko hivyo ulimwenguni pote. Lakini, hivi karibuni Mungu atawaondoa watu hao. Anaahidi hivi: “Waovu wanapochipuka kama magugu, na watenda mabaya wote wanapositawi, ni ili waangamizwe [au, kuharibiwa] milele.”—Zaburi 92:7.

HABARI NJEMA KATIKA SIKU ZA MWISHO

12, 13. Yehova ametufundisha mambo gani katika siku za mwisho?

12 Biblia ilitabiri kwamba katika siku za mwisho, ulimwengu mzima ungejaa maumivu na mateso. Lakini pia inasema kuhusu mambo mazuri ambayo yangetukia.

“Habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.”​—Mathayo 24:14

13 Uelewaji wa Biblia. Nabii Danieli alitabiri kuhusu siku za mwisho. Aliandika hivi: “Ujuzi wa kweli utakuwa mwingi.” (Danieli 12:4) Mungu angewasaidia watu wake waielewe Biblia vizuri zaidi kuliko ilivyokuwa zamani. Yehova amefanya hivyo hasa tangu mwaka 1914. Kwa mfano, ametufundisha jina lake, kusudi lake kwa dunia, ukweli kuhusu fidia, hali ya wafu, na tumaini la ufufuo. Tumejifunza kwamba ni Ufalme wa Mungu pekee unaoweza kusuluhisha matatizo yetu. Pia, tumejifunza jinsi ya kuwa na furaha na jinsi tunavyoweza kumpendeza Mungu katika maisha yetu. Hata hivyo, watumishi wa Mungu wanatumiaje mambo wanayojifunza? Unabii mwingine utatusaidia kupata jibu.—Soma Maelezo ya Ziada 21 na 25.

14. Habari njema ya Ufalme inahubiriwa katika nchi na lugha ngapi, na ni nani wanaoihubiri?

14 Kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Alipokuwa akizungumzia siku za mwisho, Yesu alisema hivi: “Habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:3, 14) Habari njema ya Ufalme inahubiriwa katika lugha zaidi ya 700 katika nchi zaidi ya 230. Naam, ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova kutoka “mataifa yote na makabila” wanawasaidia watu kuuelewa Ufalme wa Mungu na mambo utakayowafanyia wanadamu. (Ufunuo 7:9) Wanafanya kazi hiyo bila malipo. Ingawa wanapingwa na kuteswa na watu wengi, hakuna kitu kitakachozuia kazi ya kuhubiri kama Yesu alivyotabiri.—Luka 21:17.

UTAFANYA NINI?

15. (a) Je, unaamini kwamba tunaishi katika siku za mwisho, kwa nini? (b) Ni nini kitakachowapata wale wasiomtii Mungu? (c) Wale wanaomtii Mungu wataona nini?

15 Je, unaamini kwamba tunaishi katika siku za mwisho? Unabii mwingi unaohusu siku za mwisho umetimia. Hivi karibuni Yehova atasimamisha kazi ya kuhubiri habari njema, na “mwisho” utakuja. (Mathayo 24:14) Mwisho ni nini? Mwisho unamaanisha vita vya Har–Magedoni, Mungu atakapowaangamiza watu waovu. Yehova atamtumia Yesu na malaika zake wenye nguvu kuwaangamiza watu wote wasiomtii Yeye na Mwana wake. (2 Wathesalonike 1:6-9) Hatimaye, Shetani na roho wake waovu hatawadanganya tena wanadamu. Wale wote wanaomtii Mungu na kuukubali Ufalme wake wataona utimizo wa unabii wote uliotolewa na Mungu.—Ufunuo 20:1-3; 21:3-5.

16. Kwa kuwa mwisho uko karibu, unahitaji kufanya nini?

16 Hivi karibuni, ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani utaharibiwa. Kwa hiyo, ni muhimu ujiulize hivi, ‘Ninahitaji kufanya nini?’ Yehova anataka uendelee kujifunza Biblia. Usipuuze kujifunza Biblia. (Yohana 17:3) Kila juma, Mashahidi wa Yehova huhudhuria mikutano inayowasaidia watu kuielewa Biblia. Jitahidi kuhudhuria mikutano hiyo. (Soma Waebrania 10:24, 25.) Unapojua kwamba unahitaji kufanya mabadiliko, usisite kuyafanya. Ukifanya hivyo, uhusiano wako na Yehova utaimarika.—Yakobo 4:8.

17. Kwa nini watu wengi watashtuka mwisho utakapokuja?

17 Mtume Paulo alieleza kwamba uharibifu wa waovu utakuja bila kutarajiwa “kama vile mwizi anavyokuja usiku.” (1 Wathesalonike 5:2) Yesu alitabiri kuwa watu wengi wangepuuza uthibitisho wa kwamba tunaishi katika siku za mwisho. Alisema hivi: “Kama siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu [au, siku za mwisho] kutakavyokuwa. Kwa maana kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina, nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:37-39.

18. Yesu alitutolea onyo gani?

18 Yesu alionya kwamba hatupaswi kukengeushwa “na kula na kunywa kupita kiasi na mahangaiko ya maisha.” Alisema kwamba mwisho utakuja ghafla, “kama mtego.” Pia, alisema siku hiyo “itakuja juu ya wale wote wanaoishi juu ya uso wa dunia yote.” Halafu akaendelea kusema hivi: “Basi, endeleeni kukesha sikuzote mkiomba dua [au, mkisali kwa unyoofu] ili mfanikiwe kuponyoka mambo yote hayo ambayo lazima yatukie, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.” (Luka 21:34-36) Kwa nini tunapaswa kutii onyo la Yesu? Kwa sababu ulimwengu mwovu wa Shetani utaharibiwa hivi karibuni. Ni wale tu walio na kibali cha Yehova na Yesu watakaookolewa na kuishi milele katika ulimwengu mpya.—Yohana 3:16; 2 Petro 3:13.

^ fu. 4 Mikaeli ni jina lingine la Yesu. Kwa habari zaidi, soma Maelezo ya Ziada 23.