Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI

Ukweli Kuhusu Malaika

Ukweli Kuhusu Malaika

1. Kwa nini tunahitaji kujifunza kuhusu malaika?

YEHOVA anataka tuijue familia yake. Malaika ni sehemu ya familia yake. Katika Biblia wanaitwa ‘wana wa Mungu.’ (Ayubu 38:7) Malaika hufanya kazi gani? Waliwasaidiaje watu wakati uliopita? Je, wanaweza kutusaidia?—Soma Maelezo ya Ziada 8.

2. Malaika walitoka wapi? Mungu aliumba malaika wangapi?

2 Malaika walitoka wapi? Andiko la Wakolosai 1:16 linasema kwamba baada ya Yehova kumuumba Yesu, ndipo “vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani.” Malaika pia waliumbwa. Ni malaika wangapi waliumbwa? Biblia inasema kwamba ni mamilioni ya malaika.—Zaburi 103:20; Ufunuo 5:11.

3. Andiko la Ayubu 38:4-7 linasema nini kuhusu malaika?

3 Pia, Biblia inafundisha kwamba Yehova aliwaumba malaika kabla ya kuumba dunia. Malaika walihisije dunia ilipoumbwa? Kitabu cha Biblia cha Ayubu kinasema kwamba walishangilia. Walikuwa familia iliyomtumikia Yehova kwa umoja.—Ayubu 38:4-7.

MALAIKA HUWASAIDIA WATU WA MUNGU

4. Tunajuaje kwamba malaika hupendezwa na wanadamu?

4 Sikuzote malaika hupendezwa na wanadamu na kusudi la Yehova kwa dunia. (Methali 8:30, 31; 1 Petro 1:11, 12) Ni wazi kwamba walihuzunika sana Adamu na Hawa walipomwasi Mungu. Wanahuzunika hata zaidi wanapowaona wanadamu wengi wakikataa kumtii Mungu. Hata hivyo, malaika hushangilia mtu mmoja anapotubu na kumrudia Mungu. (Luka 15:10) Malaika wanapendezwa sana na wale wanaomtumikia Mungu. Yehova huwatumia malaika kuwasaidia na kuwalinda watumishi wake duniani. (Waebrania 1:7, 14) Acheni tuchunguze baadhi ya mifano.

“Mungu wangu alimtuma malaika wake akafunga vinywa vya simba.”​—Danieli 6:22

5. Malaika waliwasaidiaje watumishi wa Mungu nyakati za kale?

5 Yehova aliwatuma malaika wawili wamsaidie Loti na familia yake kuokoka uharibifu wa majiji ya Sodoma na Gomora. (Mwanzo 19:15, 16) Miaka mingi baadaye, nabii Danieli alitupwa katika shimo la simba, lakini hawakumshambulia kwa sababu Mungu “alimtuma malaika wake akafunga vinywa vya simba.” (Danieli 6:22) Baadaye, mtume Petro alipokuwa gerezani, Yehova alimtuma malaika ili kumweka huru. (Matendo 12:6-11) Pia, malaika walimsaidia Yesu alipokuwa duniani. Kwa mfano, baada ya kubatizwa, “malaika walikuwa wakimhudumia.” (Marko 1:13) Muda mfupi kabla ya Yesu kuuawa, malaika ‘alimtia nguvu.’—Luka 22:43.

6. (a) Tunajuaje kwamba malaika huwasaidia watu leo? (b) Tutachunguza maswali gani?

6 Leo, malaika hawawatokei wanadamu. Hata hivyo, bado Mungu anawatumia malaika kuwasaidia watumishi wake. Biblia inasema hivi: “Malaika wa Yehova hupiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa Yeye, naye huwaokoa.” (Zaburi 34:7) Kwa nini tunahitaji ulinzi? Kwa sababu tuna maadui wenye nguvu ambao wanataka kutushambulia. Maadui hao ni nani? Walitoka wapi? Wanatumia njia gani kutuumiza? Ili kujibu maswali hayo, acheni tuchunguze mambo yaliyotukia muda mfupi baada ya Adamu na Hawa kuumbwa.

ADUI ZETU WASIOONEKANA

7. Shetani amefaulu kufanya nini?

7 Katika Sura ya 3 tulijifunza kwamba malaika mmoja alimwasi Mungu na alitaka kuwatawala wengine. Biblia humwita Shetani Ibilisi. (Ufunuo 12:9) Pia, Shetani alitaka wengine wamwasi Mungu. Alifaulu kumdanganya Hawa, na tangu wakati huo amewadanganya wanadamu wengi. Hata hivyo, wanadamu wachache kama vile Abeli, Enoko na Noa, waliendelea kuwa waaminifu kwa Yehova.—Waebrania 11:4, 5, 7.

8. (a) Baadhi ya malaika walibadilikaje na kuwa roho waovu? (b) Roho waovu walifanya nini ili kuokoka Gharika?

8 Wakati wa Noa, baadhi ya malaika waliasi na kuacha makao yao mbinguni ili waishi duniani kama wanadamu. Kwa nini? Biblia inasema kwamba walitaka kuoa. (Soma Mwanzo 6:2.) Lakini lilikuwa kosa kwa malaika kufanya hivyo. (Yuda 6) Wakati huo, wanadamu wengi wakawa na maadili mabaya na wakawa wakatili kama malaika hao waovu. Ndipo Yehova akaamua kuwaharibu wanadamu wote waovu kwa gharika. Hata hivyo, aliwaokoa watumishi wake waaminifu. (Mwanzo 7:17, 23) Malaika waovu walirudi mbinguni ili wasiharibiwe. Biblia huwaita roho waovu. Walichagua kumuunga mkono Shetani, naye akawa mtawala wao.—Mathayo 9:34.

9. (a) Ni nini kilichowapata roho waovu waliporudi mbinguni? (b) Tutajifunza nini katika sehemu inayofuata?

9 Kwa sababu waliasi, Yehova hakuwakubali tena katika familia yake. (2 Petro 2:4) Roho waovu hawawezi kujibadilisha na kuwa wanadamu tena, lakini bado ‘wanaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9; 1 Yohana 5:19) Hebu tuchunguze jinsi ambavyo roho waovu huwadanganya au kuwapotosha watu wengi leo.—Soma 2 Wakorintho 2:11.

JINSI ROHO WAOVU WANAVYOPOTOSHA

10. Roho waovu huwapotoshaje watu?

10 Roho waovu hutumia njia nyingi kuwapotosha watu. Watu huwasiliana na roho waovu moja kwa moja au kupitia mtu mwingine, kama vile waganga wa kienyeji. Zoea hilo huitwa kuwasiliana na roho au pepo. Hata hivyo, Biblia inatuonya tuepuke kabisa jambo lolote linalohusiana na roho waovu. (Wagalatia 5:19-21) Kwa nini? Kama vile mwindaji anavyotumia mtego kuwanasa wanyama, roho waovu hutumia ujanja kuwanasa na kuwaongoza wanadamu.—Soma Maelezo ya Ziada 26.

11. Uaguzi ni nini, na kwa nini tunapaswa kuuepuka?

11 Mbinu moja wanayotumia ni uaguzi. Uaguzi ni kutumia uchawi ili kutafuta habari za wakati ujao au jambo lisilojulikana. Huenda mtu akafanya uaguzi kwa kutazama nyota, kutafuta ishara za bahati, kusoma kadi za karata, kutazama mpira wa kioo, au kusoma viganja vya mkono. Watu wengi hufikiri kwamba uaguzi hauna madhara yoyote, hata hivyo, ni hatari sana. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba waaguzi hushirikiana na roho waovu. Katika Matendo 16:16-18 tunasoma kuhusu “roho mwovu wa uaguzi” aliyemwezesha kijakazi fulani “kubashiri.” Baada ya mtume Paulo kumfukuza roho huyo mwovu, kijakazi huyo alipoteza uwezo wa kubashiri.

12. (a) Kwa nini ni hatari kuwasiliana na wafu? (b) Kwa nini watumishi wa Mungu hawashiriki desturi za kuwasiliana na wafu?

12 Roho waovu hutumia mbinu nyingine kuwanasa watu. Wanajaribu kuwadanganya watu waamini kwamba wafu wako hai, nao wanaweza kuwasiliana nasi au kutuumiza. Kwa mfano, huenda mtu aliyefiwa na rafiki au mtu wa ukoo akamwendea mchawi ambaye hudai ana uwezo wa kuwasiliana na wafu. Huenda akamweleza jambo fulani kuhusu mtu aliyekufa na hata kuiga sauti yake. (1 Samweli 28:3-19) Pia, desturi nyingi za mazishi zinaonyesha kwamba watu wanaamini kuwa wafu huendelea kuishi mahali fulani. Desturi hizo ni pamoja na sherehe za mazishi, siku za maombezi ya wafu, dhabihu kwa ajili ya wafu, siku za kuwatakasa wajane au sherehe za kukesha. Wakristo wanapokataa kushiriki desturi hizo, huenda watu wa familia au jamii ikawashutumu, kuwadhihaki, au kukataa kushirikiana nao katika shughuli nyingine. Wakristo wanajua kwamba wafu hawaendelei kuishi. Haiwezekani kuwasiliana na wafu, wala hawawezi kutuumiza. (Zaburi 115:17) Uwe mwangalifu sana. Usijaribu kamwe kuwasiliana na wafu, wala kushiriki katika desturi zinazohusiana na roho waovu.—Soma Kumbukumbu la Torati 18:10, 11; Isaya 8:19.

13. Watu wengi ambao waliwaogopa roho waovu wamefaulu kufanya nini?

13 Roho waovu huwatisha na kuwapotosha watu. Shetani na roho wake waovu wanajua kwamba wana “kipindi kifupi cha wakati” kabla ya kuangamizwa, hivyo wana hasira nyingi na jeuri kuliko wakati mwingine wowote. (Ufunuo 12:12, 17) Hata hivyo, watu wengi ambao zamani waliwaogopa roho waovu, hawawaogopi tena. Ni nini kimewasaidia kushinda woga huo?

WAPINGE ROHO WAOVU

14. Kama Wakristo wa karne ya kwanza, tunawezaje kuwapinga roho waovu?

14 Biblia hutueleza jinsi ya kuwapinga roho waovu. Kwa mfano, baadhi ya watu katika jiji la Efeso walikuwa wakiwasiliana na roho waovu kabla ya kujifunza ukweli. Ni nini kilichowasaidia kuacha zoea hilo? Biblia inasema hivi: “Idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya uchawi wakakusanya vitabu vyao pamoja na kuviteketeza mbele ya kila mtu.” (Matendo 19:19) Kwa sababu walitaka kuwa Wakristo waliteketeza vitabu vyote vilivyohusiana na uchawi. Sisi pia tunahitaji kufanya kama wao. Ni lazima mtu anayetaka kumtumikia Yehova, aharibu vitu vyote vinavyohusiana na roho waovu. Vitu hivyo ni pamoja na vitabu, magazeti, kutazama nyota, sinema, muziki, na michezo inayohusisha kuwasiliana na roho waovu, au nguvu za uchawi. Pia, vinatia ndani hirizi zinazovaliwa ili kujilinda na roho waovu.1 Wakorintho 10:21.

15. Ni jambo gani lingine tunalohitaji kufanya ili kumpinga Shetani na roho waovu?

15 Miaka kadhaa baada ya Wakristo huko Efeso kuharibu vitabu vyao vya uchawi, Mtume Paulo aliandika kwamba bado walihitaji kuendelea ‘kupambana’ na kupigana na “majeshi ya roho waovu.” (Waefeso 6:12) Ingawa walichoma vitabu vyao, bado roho waovu walijaribu kuwadhuru. Kwa hiyo, walihitaji kufanya nini? Paulo aliwaambia: “Chukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwa kuitumia mtaizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu.” (Waefeso 6:16) Kama vile ngao inavyomkinga askari vitani, imani yetu itatulinda. Tukimtumaini kabisa Yehova, atatulinda na tutamshinda Shetani na roho waovu.—Mathayo 17:20.

16. Tunawezaje kuimarisha imani yetu katika Yehova?

16 Tunawezaje kuimarisha imani yetu katika Yehova? Tunapaswa kusoma Biblia kila siku na kumtegemea ili atulinde. Tukimtumaini Yehova, Shetani na roho wake waovu hawataweza kutudhuru.—1 Yohana 5:5.

17. Tunapaswa kufanya jambo gani lingine ili kujilinda na roho waovu?

17 Wakristo huko Efeso walihitaji kufanya jambo gani lingine? Waliishi katika jiji ambalo lilijaa mazoea ya kuwasiliana na roho waovu. Kwa hiyo Paulo aliwaambia hivi: ‘Endeleeni kusali kila wakati.’ (Waefeso 6:18) Walihitaji kumwomba Yehova awalinde nyakati zote. Namna gani sisi? Tunaishi katika ulimwengu uliojaa mazoea ya kuwasiliana na roho waovu. Kwa hiyo, tunahitaji kumwomba Yehova atulinde, na tusali kwa kutumia jina lake. (Soma Methali 18:10.) Tukiendelea kumwomba Yehova atukomboe kutokana na Shetani, atajibu sala zetu.—Zaburi 145:19; Mathayo 6:13.

18, 19. (a) Tunawezaje kushinda vita dhidi ya Shetani na roho waovu? (b) Sura inayofuata itajibu swali gani?

18 Tukiharibu kila kitu kinachohusiana na roho waovu na kumtegemea Yehova atulinde, tunaweza kumpinga Shetani na roho waovu. Hatupaswi kuwaogopa. (Soma Yakobo 4:7, 8.) Yehova ana nguvu kuliko roho waovu. Aliwaadhibu katika siku za Noa, na atawaangamiza wakati ujao. (Yuda 6) Kumbuka kwamba hatupigani vita hivyo peke yetu, Yehova hutumia malaika wake ili kutulinda. (2 Wafalme 6:15-17) Tuwe na uhakika kwamba tunaweza kushinda vita dhidi ya Shetani na roho waovu kwa sababu Yehova atatusaidia.—1 Petro 5:6, 7; 2 Petro 2:9.

19 Hata hivyo, kwa nini Mungu hajamwangamiza Shetani na roho waovu ambao wanasababisha mateso? Sura inayofuata itajibu swali hilo.