Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 10

Kweli Juu ya Malaika

Kweli Juu ya Malaika

1. Juu ya nini tunapaswa kujua kweli juu ya malaika?

YEHOVA anapenda tujue familia yake. Malaika wako mu familia ya Mungu. Biblia inawaita ‘wana wa Mungu.’ (Yobu 38:7) Malaika wanafanyaka nini? Namna gani walisaidia watu zamani? Wanaweza kutusaidia leo?​—Ona Mafasirio Ingine ya 8.

2. Malaika walitoka wapi? Wako ngapi?

2 Tunapaswa kujua malaika walitoka wapi. Andiko la Wakolosai 1:16 linasema kama kisha Yehova kumuumba Yesu, “vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani.” Malaika pia waliumbwa. Mungu aliumba malaika ngapi? Biblia inasema kama kuko mamia ya mamilioni ya malaika.​—Zaburi 103:20; Ufunuo 5:11.

3. Andiko la Yobu 38:4-7 linasema nini juu ya malaika?

3 Tena Biblia inasema kama Yehova aliumba malaika mbele aumbe dunia. Walijisikia namna gani wakati Mungu aliumba dunia? Kitabu cha Yobu kinasema kama walifurahi sana. Walikuwa mu familia yenye umoja na walimutumikia Yehova pamoja.​—Yobu 38:4-7.

MALAIKA WANASAIDIAKA WATU WA MUNGU

4. Ni nini inaonyesha kama malaika wanapendezwa na wanadamu?

4 Sikuzote, malaika wamependezwa na wanadamu na wamependezwa na kusudi la Yehova juu ya dunia na wanadamu. (Mezali 8:30, 31; 1 Petro 1:11, 12) Walipaswa kuhuzunika sana wakati Adamu na Eva walikosa kumutii ao kumusikia Mungu. Wanapaswa kuhuzunika zaidi leo kuona watu wengi wanakosa kumutii Yehova. Lakini wakati watu fulani wanatubu na kumurudilia Mungu, malaika wanafurahi sana. (Luka 15:10) Malaika wanapendezwa na watu wenye kumutumikia Mungu. Yehova anatumia malaika ili wasaidie na kulinda watumishi wake mu dunia. (Waebrania 1:7, 14) Tuzungumuzie basi mifano fulani.

“Mungu wangu alituma malaika wake na akafunga vinywa vya simba.”​—Danieli 6:22

5. Namna gani malaika walisaidia watumishi wa Mungu zamani?

5 Yehova alituma malaika wawili ili wamusaidie Loti na watu wa familia yake kuokoka uharibifu wa miji ya Sodoma na Gomora. (Mwanzo 19:15, 16) Mamia ya miaka kisha pale, nabii Danieli alitupwa mu shimo la simba, lakini hawakumuumiza, kwa sababu Mungu “alituma malaika wake na akafunga vinywa vya simba.” (Danieli 6:22) Kisha, wakati mutume Petro alikuwa anafungwa mu gereza, Yehova alituma malaika ili amufungue. (Matendo 12:6-11) Malaika walisaidia pia Yesu wakati alikuwa mu dunia. Kwa mufano, kisha kubatizwa, “malaika walikuwa wanamutumikia.” (Marko 1:13) Mbele tu Yesu auawe, malaika ‘alimutia nguvu.’​—Luka 22:43.

6. (a) Ni nini inaonyesha kama malaika wanasaidia watu wa Mungu leo? (b) Tutajibu maulizo gani?

6 Leo, malaika hawatokee tena watu. Lakini Mungu angali anatumia malaika ili kusaidia watumishi wake. Biblia inasema hivi: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuzunguka wale wenye kumuogopa Yeye na anawaokoa.” (Zaburi 34:7) Juu ya nini tuko na lazima ya ulinzi? Juu tuko na maadui wenye nguvu sana wenye wanapenda kututendea mubaya. Maadui hao ni nani? Walitoka wapi? Namna gani wanajaribu kututendea mubaya? Ili kujibu maulizo hayo, tuzungumuzie mambo yenye yalitendeka kisha tu Mungu kuumba Adamu na Eva.

MAADUI WETU WENYE HAWAONEKANE

7. Juu ya nini Shetani anadanganya watu?

7 Mu Sura ya 3, tulijifunza kama malaika mumoja alimupinga Mungu na alipenda kutawala wengine. Biblia inamuita Shetani Ibilisi. (Ufunuo 12:9) Tena, Shetani alipenda wengine wamupinge Mungu. Aliweza kumudanganya Eva, na kuanzia wakati huo amedanganya watu wengi. Lakini, watu fulani kama vile Abeli, Enoko, na Noa, walibakia waaminifu kwa Yehova.​—Waebrania 11:4, 5, 7.

8. (a) Namna gani malaika fulani waligeuka na kuwa pepo wachafu? (b) Pepo wachafu walifanya nini ili wasiharibiwe wakati wa Garika?

8 Mu siku za Noa, malaika fulani walimupinga Mungu na kuacha makao yao mbinguni ili wakuje kuishi kama wanadamu mu dunia. Juu ya nini? Biblia inasema kama walipenda kuwa na wanamuke. (Soma Mwanzo 6:2.) Lakini ilikuwa makosa kwa malaika kufanya vile. (Yuda 6) Kama malaika hao wabaya, watu wengi wa wakati huo walifanya mambo ya mubaya na kutenda kwa jeuri. Kwa hiyo, Yehova aliamua kuharibu wanadamu wabaya kwa kuleta garika juu ya dunia yote. Lakini aliokoa watumishi wake waaminifu. (Mwanzo 7:17, 23) Malaika hao wabaya walirudia mbinguni ili wasiharibiwe. Biblia inaita malaika hao wabaya pepo wachafu. Walijiunga na Shetani ili wamupinge Mungu, na Shetani akakuwa mutawala wao.​—Matayo 9:34.

9. (a) Ni nini ilifikia pepo wachafu wakati walirudia mbinguni? (b) Tutazungumuzia nini sasa?

9 Kwa sababu pepo hao wachafu walimupinga Yehova, hakuwaitika tena mu familia yake. (2 Petro 2:4) Pepo wachafu hawawezi tena kuvaa mwili wa wanadamu, lakini wangali ‘wanapotosha [ao, wanadanganya] dunia yote yenye kuikaliwa na watu.’ (Ufunuo 12:9; 1 Yohana 5:19) Tuzungumuzie basi namna wanadanganya watu wengi sana.​—Soma 2 Wakorinto 2:11.

NAMNA PEPO WACHAFU WANADANGANYA WATU

10. Namna gani pepo wachafu wanadanganya watu?

10 Pepo wachafu wanatumia njia za mingi juu ya kudanganya watu. Wakati watu wanapashana habari na pepo wachafu, wanafanya vile moja kwa moja ao kupitia muchawi ao mufumu. Tendo la kuzungumuza kwa njia fulani na pepo wachafu linaitwa kupashana habari na pepo wachafu. Lakini Biblia inatuamuru tuepuke mambo yote yenye kuwa na upatano na pepo wachafu. (Wagalatia 5:19-21) Juu ya nini? Kama vile tu muwindaji anatumia mutego ili akamate wanyama, pepo wachafu wanatumia udanganyifu ili kukamata watu na kuwaongoza.​—Ona Mafasirio Ingine ya 26.

11. Uaguzi ni nini, na juu ya nini tunapaswa kuepuka jambo hilo?

11 Kwa mufano, pepo wachafu wanatumia uaguzi ili wadanganye watu. Uaguzi ni kutumia uchawi ili kujaribu kujua mambo yenye yatatokea wakati wenye kuja, ao kujua mambo yenye hayajulikane. Mutu anaweza kujaribu kufanya vile kwa kuangalia nyota, kutafuta alama za mambo ya wakati wenye kuja, kusoma karte, kuangalia kitu chenye kuwa kama kioo, ao kwa kusoma mistari yenye kuwa kwenye mukono wa mutu fulani. Watu wengi wanawaza kama mambo hayo hayalete hatari. Lakini yanaleta hatari sana. Kwa mufano, Biblia inaonyesha kama pepo wachafu na watu wenye kutabiri matukio wanatumika pamoja. Andiko la Matendo 16:16-18, linazungumuzia “pepo muchafu wa uaguzi” mwenye alisaidia kijana mwanamuke fulani “kutabiri matukio.” Wakati mutume Paulo alifukuza pepo huyo muchafu, kijana huyo mwanamuke alipoteza uwezo wake wa kutabiri matukio.

12. (a) Juu ya nini ni hatari kujaribu kuzungumuza na watu wenye wamekufa? (b) Juu ya nini watumishi wa Mungu hawajiingize hata kidogo mu desturi zenye kuwa na upatano na pepo wachafu?

12 Pepo wachafu wanatumia njia ingine ili wadanganye watu. Wanajaribu kutuchochea tuamini kama inawezekana kuzungumuza na watu wenye wamekufa, na kama wanaendelea kuishi mahali fulani na wanaweza kuzungumuza na sisi, ao kutufanyia mambo ya mubaya. Kwa mufano, mutu mwenye rafiki yake ao mutu wa familia yake amekufa, anaweza kuenda kwa muchawi mwenye anasema kama anaweza kuzungumuza na watu wenye wamekufa. Muchawi anaweza kuambia mutu huyo jambo fulani lenye kufurahisha juu ya rafiki ao mutu wa familia yake mwenye amekufa, na hata anaweza kusema kama mutu huyo mwenye amekufa. (1 Samweli 28:3-19) Desturi za mingi za maziko zinategemea pia imani ya kwamba watu wenye wamekufa wangali wanaishi mahali fulani. Desturi hizo zinaweza kutia ndani mambo yenye kufanywa wakati wa maziko, kukumbuka kila mwaka siku yenye mutu fulani alikufaka, kutolea zabihu watu wenye wamekufa, desturi zenye kufanywa juu ya wajane, ao desturi fulani za kukesha wakati wa kilio. Wakati Wakristo wanakataa kufanya desturi hizo, watu wa familia yao ao wa eneo lao wanaweza kuwasema mubaya, kuwatukana, ao kukataa kujiunga nao. Lakini, Wakristo wanajua kama watu wenye wamekufa hawaendelee kuishi mahali fulani. Hatuwezi kuzungumuza nao, na hawawezi kutufanyia mambo ya mubaya. (Zaburi 115:17) Ukuwe muangalifu sana. Usipime kuzungumuza na pepo wachafu na usijiingize hata kidogo mu desturi zenye kuwa na upatano na pepo wachafu.​—Soma Kumbukumbu la Torati 18:10, 11; Isaya 8:19.

13. Watu wengi wenye zamani walikuwa wanaogopa pepo wachafu wameweza kufanya nini?

13 Zaidi ya kudanganya watu, pepo wachafu wanawaogopesha. Leo, Shetani na pepo wake wachafu wanajua kama wanabakia tu na “kipindi kifupi cha wakati” mbele Mungu awaharibu. Kwa hiyo, wako wenye jeuri sana na wakali sana kuliko zamani. (Ufunuo 12:12, 17) Lakini, watu wengi wenye zamani walikuwa wanaogopa pepo wachafu, wameacha kuwaogopa. Ni nini iliwasaidia waache kuogopa pepo wachafu?

PINGA PEPO WACHAFU NA UACHANE NAO

14. Kama Wakristo wa wakati wa mitume, namna gani tunaweza kuachana na pepo wachafu?

14 Biblia inatuambia namna ya kupinga pepo wachafu na kuachana nao. Kwa mufano, watu fulani mu muji wa Efeso walikuwa wanapashana habari na pepo wachafu mbele wajifunze kweli. Namna gani waliachana na tabia hiyo? Biblia inasema hivi: “Hesabu kubwa ya wale wenye walizoea kufanya uchawi wakakusanya vitabu vyao pamoja na wakaviteketeza [ao, wakaviunguza kabisa] kwa moto mbele ya watu wote.” (Matendo 19:19) Juu walipenda kuwa Wakristo, waliunguza kabisa vitabu vyao vyote vya mambo ya uchawi. Iko lazima kufanya vile leo pia. Kila mutu mwenye anapenda kumutumikia Yehova anapaswa kuharibu kila kitu chenye kuwa na upatano na pepo wachafu. Ni vitu kama vile vitabu, magazeti, vitu vya kuchunguza alama za nyota, filme, miziki, michezo, na hata picha zenye kuonyesha kama uchawi, pepo wachafu, na nguvu za uchawi havina hatari yoyote ao ni vyenye kufurahisha. Vitu hivyo vinatia ndani pia vitu vyenye watu wanavaa ili wasipatwe na mambo ya mubaya.​—1 Wakorinto 10:21.

15. Tunapaswa kufanya jambo gani lingine ili tupinge Shetani na pepo wachafu?

15 Miaka fulani kisha Wakristo wa Efeso kuharibu vitabu vyao vya mambo ya uchawi, mutume Paulo aliandika kama walipaswa kuendelea ‘kupambana’ na kupiganisha “majeshi ya pepo wachafu.” (Waefeso 6:12) Hata kama walikuwa wameunguza vitabu vyao, pepo wachafu waliendelea kujaribu kuwatendea mambo ya mubaya. Kwa hiyo, walipaswa kufanya jambo gani lingine? Paulo aliwaambia hivi: “Muchukue ngao kubwa ya imani, yenye kwa kuitumia mutaweza kuzimisha mishale yote yenye kuwaka moto ya ule muovu.” (Waefeso 6:16) Kama vile tu ngao inalinda askari mu vita, imani inaweza kutulinda. Kama tuko na imani kabisa kwamba Yehova anaweza kutulinda, tutaweza kumupinga Shetani na pepo wachafu.​—Matayo 17:20.

16. Namna gani tunaweza kutia nguvu imani yetu katika Yehova?

16 Namna gani tunaweza kutia nguvu imani yetu katika Yehova? Tunapaswa kusoma Biblia kila siku na kujifunza kumutegemea Yehova ili atulinde. Kama tuko na imani yenye nguvu katika Yehova, Shetani na pepo wachafu hawataweza kutufanyia mambo ya mubaya.​—1 Yohana 5:5.

17. Ili tupate ulinzi juu ya pepo wachafu tunapaswa kufanya jambo gani lingine?

17 Wakristo mu muji wa Efeso walipaswa kufanya jambo gani lingine? Waliishi mu muji wenye ulijaa mambo ya kupashana habari na pepo wachafu. Kwa hiyo, Paulo aliwaambia hivi: ‘Muendelee kusali kila wakati.’ (Waefeso 6:18) Kila wakati walipaswa kumuomba Yehova awalinde. Na sisi tunapaswa kufanya nini? Na sisi tunaishi mu ulimwengu wenye kujaa mambo ya kupashana habari na pepo wachafu. Kwa hiyo, sisi pia tunapaswa kumuomba Yehova atulinde, na tunapaswa kutumia jina lake wakati tunasali. (Soma Mezali 18:10.) Kama tunaendelea kumuomba Yehova atukomboe na Shetani, Yehova atajibu sala zetu.​—Zaburi 145:19; Matayo 6:13.

18, 19. (a) Namna gani tunaweza kupata ushindi mu vita yetu juu ya Shetani na pepo wachafu? (b) Tutajibu ulizo gani mu habari yenye kufuata?

18 Kama tunaachana na kila kitu chenye kuwa na upatano na pepo wachafu na kutegemea ulinzi wa Yehova, tunaweza kupinga Shetani na pepo wachafu. Hatupaswe kuwaogopa. (Soma Yakobo 4:7, 8.) Yehova iko na nguvu zaidi kupita pepo wachafu. Aliwapatia malipizi wakati wa Noa, na wakati wenye kuja atawaharibu. (Yuda 6) Kumbuka kama, hatupigane vita peke yetu. Yehova anatumia malaika wake ili watulinde. (2 Wafalme 6:15-17) Tunapaswa kuamini kabisa kama kwa musaada wa Yehova, tunaweza kupata ushindi mu vita yetu juu ya Shetani na pepo wachafu.​—1 Petro 5:6, 7; 2 Petro 2:9.

19 Shetani na pepo wachafu wanaendelea kuleta mateso sana, juu ya nini Mungu hajawaharibu? Tutapata jibu la ulizo hilo mu habari yenye kufuata.