Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA NNE

Jinsi Familia Yako Inavyoweza Kuwa na Furaha

Jinsi Familia Yako Inavyoweza Kuwa na Furaha

1, 2. Yehova anataka familia ziwe na hali gani?

YEHOVA MUNGU alianzisha ndoa ya kwanza. Biblia inasema kwamba alimuumba mwanamke wa kwanza na “akamleta kwa mwanamume.” Adamu alifurahi sana, naye akasema hivi: “Hatimaye huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu.” (Mwanzo 2:22, 23) Jambo hilo linaonyesha kwamba Yehova anataka wale waliofunga ndoa wawe na furaha.

2 Kwa kusikitisha, leo familia nyingi hazina furaha. Hata hivyo, Biblia ina kanuni zinazoweza kumsaidia kila mtu katika familia atimize majukumu yake na kufurahia kuwa pamoja.—Luka 11:28.

MUNGU ANATARAJIA WAUME WAFANYE NINI?

3, 4. (a) Mume anapaswa kumtendeaje mke wake? (b) Kwa nini ni muhimu kwa mume na mke kusameheana kwa hiari?

3 Biblia inasema kwamba mume mzuri anapaswa kumpenda na kumheshimu mke wake. Tafadhali, soma Waefeso 5:25-29. Sikuzote mume anamtendea mke wake kwa upendo. Pia, anamlinda, anamtunza, na hatafanya jambo lolote la kumuumiza.

4 Mume anapaswa kufanya nini mke wake akikosea? Biblia inawashauri waume hivi: “Endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” (Wakolosai 3:19) Waume, kumbukeni kwamba ninyi pia hufanya makosa. Ikiwa unataka Mungu akusamehe, unapaswa kumsamehe mke wako. (Mathayo 6:12, 14, 15) Mume na mke wataifurahia sana ndoa yao ikiwa wanasameheana kwa hiari.

5. Kwa nini mume anapaswa kumheshimu mke wake?

5 Yehova anatazamia mume amheshimu mke wake. Mume anapaswa kuzingatia mahitaji ya mke wake. Hilo ni jambo zito sana. Ikiwa mume anamtendea vibaya mke wake, Yehova hatasikiliza sala zake. (1 Petro 3:7) Yehova anawathamini watu wote wanaompenda. Hawaoni wanaume kuwa bora kuliko wanawake.

6. Ni nini maana ya mume na mke kuwa “mwili mmoja”?

6 Yesu alisema kwamba mume na mke “si wawili tena, bali mwili mmoja.” (Mathayo 19:6) Wanapaswa kuwa waaminifu kwa mmoja na mwenzake. (Methali 5:15-21; Waebrania 13:4) Mume na mke wanapaswa kutimiziana mahitaji yao ya ngono. (1 Wakorintho 7:3-5) Mume anapaswa kukumbuka kwamba “hakuna mtu anayeuchukia mwili wake, bali huulisha na kuutunza.” Hivyo, anapaswa kumpenda na kumtunza mke wake. Zaidi ya yote, mke anahitaji mume wake ampende na kumtendea kwa fadhili.—Waefeso 5:29.

MUNGU ANATARAJIA WAKE WAFANYE NINI?

7. Kwa nini familia inahitaji kuwa na kichwa?

7 Kila familia inahitaji kuwa na kichwa anayeiongoza ili mambo yafanyike kwa mpango. Biblia inasema hivi katika 1 Wakorintho 11:3: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume, nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.”

8. Mke anawezaje kumwonyesha mume wake heshima?

8 Hata waume hukosea. Lakini ikiwa mke anaunga mkono maamuzi ya mume wake na kushirikiana naye kwa hiari, familia nzima inanufaika. (1 Petro 3:1-6) Biblia inasema: “Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Namna gani ikiwa mume si mwamini? Bado mke ana wajibu wa kumheshimu. Biblia inasema hivi: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu, ili ikiwa kuna wale wasiotii lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wameshuhudia kwa macho yao mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.” (1 Petro 3:1, 2) Mfano mzuri wa mke unaweza kumsaidia mume wake akubali na kuheshimu imani ya mke wake.

9. (a) Mke anapaswa kufanya nini ikiwa hakubaliani na wazo fulani la mume wake? (b) Andiko la Tito 2:4, 5, linawashauri wake wafanye nini?

9 Mke anaweza kufanya nini ikiwa hakubaliani na wazo fulani la mume wake? Anaweza kueleza maoni yake kwa heshima. Kwa mfano, wakati fulani Abrahamu hakupendezwa na maoni ya Sara, lakini Yehova alimwambia hivi: “Msikilize.” (Mwanzo 21:9-12) Mke anapaswa kuunga mkono maamuzi yote ya mume wake ikiwa hayavunji kanuni za Biblia. (Matendo 5:29; Waefeso 5:24) Mke bora anatunza familia yake. (Soma Tito 2:4, 5.) Mume na watoto wanapoona akifanya kazi kwa bidii, watampenda na kumheshimu sana.—Methali 31:10, 28.

Kwa nini Sara ni mfano mzuri kwa wanawake?

10. Biblia inasema nini kuhusu kutengana na talaka?

10 Nyakati fulani kuna hali zinazoweza kufanya wenzi wa ndoa watengane au kutalikiana. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba “mke hapaswi kutengana na mume wake” na “mume hapaswi kumwacha mke wake.” (1 Wakorintho 7:10, 11) Huenda kwa sababu ya matatizo fulani mazito wenzi wa ndoa wakaamua kutengana, hata hivyo huo ni uamuzi mzito. Namna gani kuhusu talaka? Biblia inasema kwamba sababu pekee inayoweza kufanya mume au mke watalikiane ni uasherati.—Mathayo 19:9.

MUNGU ANATARAJIA WAZAZI WAFANYE NINI?

Yesu ni mfano mzuri kwa kila mshiriki wa familia

11. Watoto wanahitaji nini kutoka kwa wazazi?

11 Wazazi, tumieni wakati mwingi iwezekanavyo pamoja na watoto wenu. Watoto wanawahitaji ninyi wazazi zaidi ya kitu kingine chochote, wanahitaji muwafundishe kumhusu Yehova.—Kumbukumbu la Torati 6: 4-9.

12. Wazazi wanapaswa kufanya nini ili kuwalinda watoto wao?

12 Ulimwengu wa Shetani umekuwa mwovu sana, pia kuna baadhi ya watu ambao wanataka kuwadhuru watoto wetu, kwa kuwatendea vibaya kingono. Ni vigumu kwa baadhi ya wazazi kuwafundisha watoto wao kuhusu ngono. Hata hivyo, wazazi wanapaswa kuwaonya watoto wao kuhusu watu hao wabaya na kuwafundisha jinsi ya kuwaepuka. Wazazi, mnapaswa kuwalinda watoto wenu. *1 Petro 5:8.

13. Wazazi wanapaswa kuwafundishaje watoto wao?

13 Wazazi wana wajibu wa kuwafundisha watoto wao tabia nzuri. Unawezaje kuwafundisha watoto wako tabia nzuri? Watoto wako wanahitaji nidhamu, lakini nidhamu haipaswi kutolewa kwa ukatili. (Yeremia 30:11) Kwa hiyo, usimwadhibu mtoto wako unapokuwa na hasira. Usitumie maneno makali ‘yanayochoma kama upanga’ ambayo yatawaumiza. (Methali 12:18) Wafundishe watoto wako umuhimu wa kutii.—Waefeso 6:4; Waebrania 12:9-11; soma Maelezo ya Ziada 30.

MUNGU ANATARAJIA WATOTO WAFANYE NINI?

14, 15. Kwa nini watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao?

14 Yesu alimtii Baba yake sikuzote, hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. (Luka 22:42; Yohana 8:28, 29) Yehova anatarajia watoto wawatii wazazi wao.—Waefeso 6:1-3.

15 Watoto, hata mkihisi kwamba ni vigumu kuwatii wazazi wenu, kumbukeni kwamba mkiwa watiifu, mtamfurahisha Yehova na wazazi wenu. *Methali 1:8; 6:20; 23:22-25.

Ni nini kitakachowasaidia vijana kumtii Mungu wanaposhawishiwa kufanya mambo mabaya?

16. (a) Shetani anatumia njia gani kuwashawishi vijana wafanye mambo mabaya? (b) Kwa nini ni muhimu kuchagua marafiki wanaompenda Yehova?

16 Ibilisi anaweza kuwatumia rafiki zako na vijana wengine ili wakushawishi ufanye mambo mabaya. Anajua kwamba itakuwa vigumu kwako kuwapinga. Kwa mfano, Dina binti ya Yakobo alikuwa na marafiki ambao hawakumpenda Yehova. Urafiki huo ulimletea matatizo mengi sana yeye na pia familia yake. (Mwanzo 34:1, 2) Ikiwa rafiki zako hawampendi Yehova, wanaweza kukushawishi ufanye mambo yanayomchukiza, hivyo kukuumiza wewe, familia yako, na Mungu. (Methali 17:21, 25) Kwa kweli, ni muhimu kutafuta marafiki wanaompenda Yehova.—1 Wakorintho 15:33.

FAMILIA YAKO INAWEZA KUWA NA FURAHA

17. Kila mtu katika familia ana wajibu gani?

17 Washiriki wa familia wanapofuata mwongozo wa Mungu, wanaepuka matatizo mengi. Hivyo, ikiwa wewe ni mume mpende mke wako. Mke, unapaswa kumheshimu na kumtii mume wako, pia unapaswa kuiga mfano wa mke anayetajwa katika Methali 31:10-31. Ikiwa wewe ni mzazi, wafundishe watoto wako kumpenda Mungu. (Methali 22:6) Ikiwa wewe ni baba, ongoza familia yako “vizuri.” (1 Timotheo 3:4, 5; 5:8) Nanyi watoto, watiini wazazi wenu. (Wakolosai 3:20) Kumbuka kwamba kila mtu katika familia anaweza kukosea, hivyo uwe mnyenyekevu na kuwaomba wengine msamaha. Naam, Biblia ina mwongozo wa Yehova kwa ajili ya kila mtu katika familia.

^ fu. 12 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu jinsi ya kuwalinda watoto wako katika kitabu Jifunze kutoka kwa Mwalimu Mkuu, sura ya 32, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 15 Mtoto anaweza kukataa kutii ikiwa mzazi anataka avunje sheria za Mungu.—Matendo 5:29.