Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA SITA

Amua Kumwabudu Mungu

Amua Kumwabudu Mungu

1, 2. Unapaswa kujiuliza swali gani, na kwa nini ni muhimu kufanya hivyo?

KUPITIA kujifunza Biblia, umetambua kwamba watu wengi wanaodai wanamwabudu Mungu hufundisha au kufanya mambo ambayo Mungu anachukia. (2 Wakorintho 6:17) Ndiyo sababu, Yehova anatuamuru tutoke katika dini za uwongo, yaani, “Babiloni Mkubwa.” (Ufunuo 18:2, 4) Utafanya nini? Kila mtu anapaswa kufanya uamuzi na kujiuliza hivi, ‘Je, nitamwabudu Mungu kulingana na mapenzi yake au nitamwabudu jinsi nipendavyo?’

2 Umefanya vizuri ikiwa umeacha kushirikiana na dini ya uwongo. Hata hivyo, huenda ikawa vigumu kuacha baadhi ya mazoea na desturi fulani za dini za uwongo ambazo ulizoea. Hebu tuchunguze baadhi ya mazoea na desturi hizo na tuone umuhimu wa kuwa na maoni kama ya Yehova.

KUABUDU SANAMU NA MABABU

3. (a) Kwa nini huenda wengine wakaona ni vigumu kuacha kutumia sanamu katika ibada? (b) Biblia inasema nini kuhusu kutumia sanamu katika ibada?

3 Kwa miaka mingi, baadhi ya watu wamekuwa na vihekalu katika nyumba zao au wametumia sanamu katika ibada. Ikiwa ulikuwa na mazoea hayo, huenda ukaona ni vigumu au ni kosa kumwabudu Mungu bila kutumia sanamu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova hutufundisha jinsi tunavyopaswa kumwabudu. Biblia inasema wazi kwamba Yehova hataki tutumie sanamu katika ibada.—Soma Kutoka 20: 4, 5; Zaburi 115:4-8; Isaya 42:8; 1 Yohana 5:21.

4. (a) Kwa nini hatupaswi kuwaabudu mababu zetu waliokufa? (b) Kwa nini Yehova aliwakataza watu wake kuwasiliana na wafu?

4 Baadhi ya watu hutumia muda na nguvu nyingi ili kuwapendeza mababu zao waliokufa. Huenda hata wakawaabudu. Hata hivyo, tumejifunza kwamba wafu hawawezi kutusaidia au kutuumiza. Hawaendelei kuishi mahali pengine. Kwa kweli, ni hatari kujaribu kuwasiliana na wafu kwa sababu habari yoyote ambayo huenda tukafikiri inatoka kwa mpendwa wetu aliyekufa, inatoka kwa roho waovu. Ndiyo sababu, Yehova aliwaamuru Waisraeli wasiwasiliane na wafu au kujihusisha na ushirikina wa aina yoyote ile.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; soma Maelezo ya Ziada 26 na 31.

5. Ni nini kitakachokusaidia kuacha kuabudu mababu waliokufa na kuacha kutumia sanamu katika ibada?

5 Ni nini kitakachokusaidia kuacha kutumia sanamu katika ibada au kuabudu mababu waliokufa? Unapaswa kusoma Biblia na kutafakari kwa makini maoni ya Yehova kuhusu mambo hayo. Mambo hayo ‘yanamchukiza’. (Kumbukumbu la Torati 27:15) Sali kwa Yehova kila siku ili akusaidie kuwa na maoni kama yake na umwabudu kwa njia inayofaa. (Isaya 55:9) Uwe na uhakika kwamba Yehova atakusaidia uache kabisa mazoea yote ya dini za uwongo.

JE, TUNAPASWA KUSHEREHEKEA KRISMASI?

6. Kwa nini Desemba 25 ilichaguliwa kuwa siku ya kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu?

6 Krismasi ni sikukuu maarufu sana ambayo husherehekewa duniani pote, na wengi huamini kwamba ni sherehe ya kukumbuka kuzaliwa kwa Yesu. Hata hivyo, Krismasi inatokana na ibada ya uwongo. Kitabu kimoja kinasema kwamba Waroma wapagani walisherehekea kuzaliwa kwa jua Desemba 25. Viongozi wa makanisa walitaka wapagani wengi wawe Wakristo, hivyo waliamua kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu Desemba 25 ingawa Yesu hakuzaliwa tarehe hiyo. (Luka 2:8-12) Wanafunzi wa Yesu hawakusherehekea Krismasi. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba miaka 200 baada ya Yesu kuzaliwa, “hakuna mtu ambaye alijua siku hususa ambayo Yesu alizaliwa, na ni watu wachache tu ambao walitaka kujua.” (Sacred Origins of Profound Things) Krismasi ilianza kusherehekewa miaka mingi baada ya Yesu kuishi duniani.

7. Kwa nini Wakristo wa kweli hawasherehekei Krismasi?

7 Watu wengi wanajua kwamba Krismasi na desturi zake kama vile sherehe za kupeana zawadi zilitokana na wapagani. Kwa mfano, wakati fulani nchini Uingereza na maeneo fulani ya Amerika, sikukuu ya Krismasi ilipigwa marufuku kwa sababu ya chanzo chake cha kipagani. Yeyote aliyesherehekea aliadhibiwa. Hata hivyo, baadaye watu walianza kusherehekea tena Krismasi. Kwa nini Wakristo wa kweli hawasherehekei Krismasi? Kwa sababu wanataka kumpendeza Mungu katika kila jambo wanalofanya.

JE, TUNAPASWA KUSHEREHEKEA SIKU ZA KUZALIWA?

8, 9. Kwa nini Wakristo wa mapema hawakusherehekea siku za kuzaliwa?

8 Watu wengi pia husherehekea siku zao za kuzaliwa. Je, Wakristo wanapaswa kusherehekea siku za kuzaliwa? Sherehe pekee za kukumbuka siku za kuzaliwa zinazotajwa katika Biblia zilifanywa na watu ambao hawakumwabudu Yehova. (Mwanzo 40:20; Marko 6:21) Sherehe za siku za kuzaliwa zilifanywa ili kuheshimu miungu ya uwongo. Ndiyo sababu, Wakristo wa karne ya kwanza “waliona kusherehekea siku ya kuzaliwa kuwa ni desturi ya kipagani.”—The World Book Encyclopedia.

9 Waroma na Wagiriki wa kale waliamini kwamba roho fulani ilikuwepo mtu alipozaliwa na ilimlinda maishani mwake. Kitabu The Lore of Birthdays kinasema hivi: “Roho hiyo ilikuwa na uhusiano wa kichawi na mungu ambaye siku yake ya kuzaliwa ililingana na siku ya kuzaliwa ya mtu huyo.”

10. Kwa nini Wakristo hawapaswi kusherehekea siku za kuzaliwa?

10  Je, unafikiri Yehova anakubali sikukuu ambazo zinahusiana na dini za uwongo? (Isaya 65:11, 12) Hapana. Hiyo ndiyo sababu hatusherehekei siku za kuzaliwa au sikukuu nyingine zinazohusiana na dini za uwongo.

JE, NI MUHIMU KUJUA CHANZO?

11. Kwa nini baadhi ya watu husherehekea sikukuu? Unapaswa kuzingatia jambo gani?

11 Ingawa baadhi ya watu wanajua kwamba Krismasi na sikukuu nyingine zilitokana na wapagani, bado wanaendelea kuzisherehekea. Wanafikiri kwamba sikukuu ni wakati mzuri wa kuwa pamoja na familia zao. Je, wewe una maoni hayo? Si vibaya kutenga wakati ili kuwa pamoja na familia yako. Yehova alianzisha familia, na angependa tuwe na uhusiano mzuri pamoja na familia. (Waefeso 3:14, 15) Hata hivyo, tunapaswa kuzingatia zaidi uhusiano wetu pamoja na Yehova kuliko kuwapendeza watu wa familia zetu kwa kusherehekea sikukuu zinazotokana na dini za uwongo. Ndiyo sababu mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kuhakikisha jambo linalokubalika kwa Bwana.”—Waefeso 5: 10.

12. Kwa nini Yehova anazikataa sikukuu fulani?

12 Watu wengi hufikiri kwamba si muhimu kujua chanzo cha sikukuu, hata hivyo, hilo halipatani na maoni ya Yehova. Mungu hukataa sikukuu zinazotokana na dini za uwongo, zinazowatukuza wanadamu au nembo za taifa. Kwa mfano, Wamisri walikuwa na sherehe nyingi kwa ajili ya miungu yao ya uwongo. Baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri, waliiga sikukuu moja ya kipagani na kuiita “sherehe kwa ajili ya Yehova.” Yehova aliwaadhibu kwa sababu ya kufanya hivyo. (Kutoka 32:2-10) Kama nabii Isaya alivyosema, hatupaswi ‘kugusa kitu chochote kichafu.’—Soma Isaya 52:11.

UWE MWENYE FADHILI UNAPOSHUGHILIKA NA WENGINE

13. Huenda ukajiuliza maswali gani baada ya kuamua kuacha kusherehekea sikukuu?

13 Huenda ukajiuliza maswali mengi baada ya kuamua kuacha kusherehekea sikukuu fulani. Kwa mfano: Ninawezaje kuwajibu wafanyakazi wenzangu wanaponiuliza kwa nini sisherehekei Krismasi pamoja nao? Ninaweza kufanya nini nikipewa zawadi ya Krismasi? Ninaweza kufanya nini ikiwa mwenzi wangu wa ndoa anataka tusherehekee sikukuu? Ninawezaje kuwasaidia watoto wangu ili wasihisi vibaya kwa sababu hawasherehekei siku za kuzaliwa au sikukuu nyingine?

14, 15. Unaweza kufanya nini mtu fulani anapokutakia heri ya sikukuu au kukupatia zawadi?

14 Ni muhimu kutumia hekima tunapoamua jinsi ya kushughulikia hali tofauti-tofauti tunazokabili. Kwa mfano, ikiwa mtu anakutakia heri ya sikukuu, hupaswi kumpuuza. Unaweza kusema, “Asante”. Hata hivyo, ikiwa mtu angependa kujua zaidi kwa nini husherehekei sikukuu, usisite kumweleza. Pamoja na hayo, wakati wote uwe mwenye fadhili, busara na heshima. Biblia inasema hivi: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yaliyokolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:6) Huenda ikafaa kuwaeleza kwamba unapenda kushirikiana na wengine, hata kutoa na kupokea zawadi, lakini, ungependa kufanya hivyo wakati mwingine tofauti na wakati wa sikukuu.

15 Unaweza kufanya nini ikiwa mtu fulani anakupa zawadi? Biblia haina sheria kuhusu kila jambo, lakini inatuhimiza tudumishe dhamiri njema. (1 Timotheo 1:18, 19) Huenda mtu anayekupa zawadi hajui kwamba wewe husherehekei sikukuu. Au huenda akasema hivi: “Ninajua kwamba husherehekei sikukuu, hata hivyo ningependa kukupatia zawadi.” Ikitegemea hali, unaweza kuamua kukubali au kukataa zawadi hiyo. Lakini, jitahidi kudumisha dhamiri njema katika uamuzi unaofanya. Hatungependa kufanya jambo lolote ambalo litaharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova.

WEWE NA FAMILIA YAKO

Wale wanaomwabudu Yehova wana furaha

16. Unapaswa kufanya nini ikiwa watu wa familia wanataka kusherehekea sikukuu?

16 Unapaswa kufanya nini ikiwa watu wa familia yako wanataka kusherehekea sikukuu? Usiwakataze. Kumbuka kwamba wana haki ya kuamua mambo wanayotaka kufanya. Uwe mwenye fadhili na uheshimu maoni yao kama vile ambavyo ungependa waheshimu maoni yako. (Soma Mathayo 7:12.) Hata hivyo, utafanya nini ikiwa watu wa familia wanataka ushirikiane nao wakati wa sikukuu? Kabla ya kuamua jambo la kufanya, sali kwa Yehova ili akusaidie kufanya uamuzi unaofaa. Fikiria hali hiyo, na ufanye utafiti. Kumbuka kwamba sikuzote, unataka kumpendeza Yehova.

17. Unaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wako wasihisi wamekosa kitu fulani kwa sababu ya kutosherehekea sikukuu?

17 Unaweza kufanya nini ili watoto wako wasihisi wamekosa kitu fulani kwa sababu ya kutosherehekea sikukuu? Mara kwa mara, pangeni kufanya mambo ambayo watafurahia. Pia, unaweza kuwafurahisha kwa kuwapatia zawadi. Mojawapo ya zawadi bora ambayo unaweza kuwapatia watoto wako ni kutenga wakati wa kuwa pamoja nao na kuwapenda.

SHIRIKIANA NA DINI YA KWELI

18. Kwa nini tunapaswa kuhudhuria mikutano ya Kikristo?

18 Ili tumpendeze Yehova, tunapaswa kuacha kushirikiana na dini za uwongo na kuepuka desturi na sikukuu za dini hizo. Pia, tunapaswa kushirikiana na dini ya kweli. Jinsi gani? Njia moja ni kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. (Soma Waebrania 10:24, 25.) Mikutano ni sehemu muhimu sana katika ibada ya kweli. (Zaburi 22:22; 122:1) Tunapokutana pamoja tunatiana moyo.—Waroma 1:12.

19. Kwa nini ni muhimu kuwaeleza wengine kuhusu kweli za Biblia ambazo umejifunza?

19 Njia nyingine ya kushirikiana na ibada ya kweli ni kuwaeleza wengine mambo ambayo umejifunza katika Biblia. Watu wengi wanahangaishwa na mambo mabaya yanayotendeka duniani. Huenda unawajua baadhi ya watu wanaohangaishwa na mambo hayo. Waeleze kuhusu tumaini zuri la wakati ujao. Kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kuwaeleza wengine kweli za Biblia, kutakusaidia kushinda tamaa ya kushirikiana na dini ya uwongo pamoja na desturi zake. Uwe na uhakika kwamba utakuwa na furaha na Yehova atabariki jitihada zako za kumwabudu kwa njia inayofaa.—Malaki 3:10.