Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 16

Chagua Kumuabudu Mungu mu Njia Yenye Anapenda

Chagua Kumuabudu Mungu mu Njia Yenye Anapenda

1, 2. Tunapaswa kujiuliza ulizo gani, na sababu gani ni jambo la maana kujiuliza ulizo hilo?

KUJIFUNZA Biblia kumekusaidia ujue kama watu wengi wanasema kama wanamutumikia Mungu, lakini wanafundisha na kufanya mambo yenye Mungu anachukia. (2 Wakorinto 6:17) Njo maana Yehova anatuomba tutoke mu dini za uongo, ni kusema, “Babiloni Mukubwa.” (Ufunuo 18:2, 4) Sasa utafanya nini? Kila mutu kati yetu anapaswa kukamata uamuzi, na tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninapenda kumuabudu Mungu mu njia yenye anapenda, ao ninapenda kuendelea kumuabudu mu njia yenye nimezoea kumuabudu?’

2 Kama umekwisha kutoka mu dini (religion) ya uongo, umefanya muzuri. Lakini pengine kuko mambo fulani ao desturi fulani za dini ya uongo zenye ungali unafurahia. Tuzungumuzie basi mambo fulani na desturi fulani na tuone juu ya nini ni jambo la maana sana tuzione namna Yehova anaziona.

KUABUDU SANAMU NA WAZAZI WA ZAMANI WENYE WAMEKUFA

3. (a) Juu ya nini watu fulani wanaweza kuona kuwa ni nguvu kuacha kutumia sanamu mu ibada yao? (b) Biblia inasema nini juu ya kutumia sanamu wakati tunamuabudu Mungu?

3 Kwa miaka mingi, watu fulani wametumia sanamu ao nafasi za kuabudia mu nyumba zao. Kama unatumia vitu hivyo, unaweza kuona kuwa ni nguvu ao hata ni makosa kumuabudu Mungu bila kuvitumia. Lakini, ukumbuke kama Yehova anatufundisha namna ya kumuabudu. Na Biblia inatuambia waziwazi kama Yehova hapendi tutumie sanamu mu ibada yetu.​—Soma Kutoka 20:4, 5; Zaburi 115:4-8; Isaya 42:8; 1 Yohana 5:21.

4. (a) Juu ya nini hatupaswe kuabudu wazazi wetu wa zamani wenye wamekufa? (b) Juu ya nini Yehova aliambia watu wake wasipime kuzungumuza na watu wenye wamekufa?

4 Watu fulani wanaweza kutumia wakati mingi na nguvu mingi ili kutafuta kufurahisha wazazi wao wa zamani wenye wamekufa ao mababu. Wanaweza hata kuwaabudu. Lakini tumejifunza kama wale wenye wamekufa hawawezi kutusaidia wala kututendea mambo ya mubaya. Hawaendelee kuishi mahali fulani. Kwa kweli, ni hatari kupima kuzungumuza nao. Kila ujumbe wenye unaonekana kuwa unatoka kwa mutu wa jamaa yetu mwenye amekufa, unatoka kwa pepo wachafu. Njo maana Yehova alikataza Waisraeli wasipime kuzungumuza na watu wenye wamekufa ao kujiingiza mu aina ingine yoyote ya kupashana habari na pepo wachafu.​—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; ona Mafasirio Ingine ya 26 na 31.

5. Ni nini inaweza kukusaidia uache kutumia sanamu wakati unamuabudu Mungu na uache kuabudu wazazi wako wa zamani wenye wamekufa?

5 Ni nini inaweza kukusaidia uache kutumia sanamu wakati unamuabudu Mungu ao kuacha kuabudu wazazi wako wa zamani wenye wamekufa? Unapaswa kusoma Biblia na kuwaza sana juu ya namna Yehova anaona mambo hayo. Anaona mambo hayo kuwa “chukizo.” (Kumbukumbu la Torati 27:15) Usali kwa Yehova kila siku akusaidie uone mambo namna anayaona na akusaidie umuabudu mu njia yenye anapenda. (Isaya 55:9) Unaweza kuamini kabisa kama Yehova atakupatia nguvu zenye uko nazo lazima ili utoshe mu maisha yako mambo yote yenye kuwa na upatano na ibada ya uongo.

TUNAPASWA KUFANYA SIKUKUU YA NOELI?

6. Juu ya nini tarehe 25 Mwezi wa 12 ilichaguliwa kuwa siku ya kukumbuka kuzaliwa kwa Yesu?

6 Noeli iko kati ya sikukuu zenye watu wengi wanapenda sana mu dunia yote, na watu wengi wanawaza kama ni sikukuu ya kukumbuka kuzaliwa kwa Yesu. Lakini sikukuu ya Noeli iko na upatano na ibada ya uongo. Kitabu kimoja kinasema kama Waroma wapagani walikuwa wanafanya sikukuu ya kuzaliwa kwa jua tarehe 25 Mwezi wa 12. Viongozi wa Kanisa walipenda wapagani wengi zaidi wakuwe Wakristo. Kwa hiyo, hata kama Yesu hakuzaliwa tarehe 25 Mwezi wa 12, waliamua kufanya sikukuu ya kuzaliwa kwa Yesu tarehe hiyo. (Luka 2:8-12) Wanafunzi wa Yesu hawakufanya sikukuu ya Noeli. Kitabu kimoja (Sacred Origins of Profound Things) kinasema kama kwa miaka 200 kisha kuzaliwa kwa Yesu, “hakuna mutu alijua tarehe kabisa ya kuzaliwa kwake, na watu wengi hawakuhangaikia jambo hilo.” Sikukuu ya Noeli ilianza kufanywa mamia ya miaka kisha Yesu kuenda mbinguni.

7. Juu ya nini Wakristo wa kweli hawafanyake sikukuu ya Noeli?

7 Watu wengi wanajua kama Sikukuu ya Noeli na desturi zake (kama vile kufanya karamu na kupatiana zawadi) vilianzishwa na wapagani. Kwa mufano, wakati fulani, sikukuu ya Noeli ilikatazwa katika Uingereza na katika sehemu fulani za Amerika, kwa sababu ilianzishwa na wapagani. Kila mutu mwenye alifanya sikukuu hiyo alikuwa anapewa malipizi. Lakini kisha wakati fulani, watu walianza kufanya tena sikukuu ya Noeli. Juu ya nini Wakristo wa kweli hawafanyake sikukuu ya Noeli? Juu wanapenda kumufurahisha Mungu mu mambo yote yenye wanafanya.

TUNAPASWA KUFANYA SIKUKUU ZA KUZALIWA?

8, 9. Juu ya nini Wakristo wa kwanza-kwanza hawakukuwa wanafanya sikukuu za kuzaliwa?

8 Sikukuu ingine yenye watu wengi wanapenda sana ni sikukuu ya kuzaliwa kwao. Wakristo wanapaswa kufanya sikukuu za kuzaliwa? Sikukuu za kuzaliwa zenye kutajwa mu Biblia zilifanywa na watu wenye hawakumuabudu Yehova. (Mwanzo 40:20; Marko 6:21) Sikukuu za kuzaliwa zilikuwa na kusudi la kuonyesha miungu ya uongo heshima. Njo maana Wakristo wa kwanza-kwanza “waliona kama kufanya sikukuu ya kuzaliwa kwa mutu ni desturi ya wapagani.”​—The World Book Encyclopedia.

9 Waroma na Wagiriki wa zamani waliamini kama kuko roho fulani yenye ilikuwa pale siku yenye kila mutu alizaliwa na kama roho hiyo ingemuchunga maisha yake yote. Kitabu kimoja (The Lore of Birthdays) kinasema kama “roho hiyo ilikuwa na upatano wa uchawi pamoja na mungu mwenye siku yake ya kuzaliwa ililingana na siku ya kuzaliwa ya mutu huyo. Na ili roho hiyo imuchunge mutu huyo, alipaswa kufanya sikukuu ya kuzaliwa kwake.”

10. Juu ya nini Wakristo hawafanyake sikukuu za kuzaliwa?

10 Unawaza kama Yehova anaitika sikukuu zenye kuwa na upatano na dini za uongo? (Isaya 65:11, 12) Hapana. Njo maana hatufanyake sikukuu za kuzaliwa ao sikukuu ingine yoyote yenye kuwa na upatano na dini ya uongo.

NI JAMBO LA MAANA KABISA KUJUA NAMNA SIKUKUU FULANI ILIANZA?

11. Juu ya nini watu fulani wanafanyaka sikukuu? Ni jambo gani lenye unapaswa kuhangaikia sana?

11 Watu fulani wanajua kama wapagani njo walianzisha sikukuu ya Noeli na sikukuu zingine, lakini wanaendelea kuzifanya. Wanaona kama wakati wa sikukuu hizo wanapata nafasi ya muzuri ya kupitisha wakati pamoja na watu wa familia zao. Na wewe unaona vile? Haiko mubaya kupitisha wakati pamoja na watu wa familia yako. Yehova njo alianzisha familia, na anapenda tukuwe na urafiki wa muzuri pamoja na watu wa familia yetu. (Waefeso 3:14, 15) Lakini, tunapaswa kuhangaikia sana kuwa na urafiki wa muzuri pamoja na Yehova kuliko kufurahisha watu wa familia yetu kwa kufanya sikukuu za dini za uongo. Njo maana mutume Paulo alisema hivi: “Muendelee kuhakikisha ni nini yenye kukubaliwa kwa Bwana.”​—Waefeso 5:10.

12. Ni nini inafanya Yehova asiitike sikukuu fulani?

12 Watu wengi wanawazaka kama haiko lazima kujua namna sikukuu fulani ilianza, lakini Yehova yeye hawaze vile. Haitike sikukuu zenye zilianzishwa na dini ya uongo ao zenye kusifu watu ao inchi. Kwa mufano, Wamisri walikuwa wanafanya sikukuu za mingi kwa ajili ya miungu yao ya uongo. Kisha Waisraeli kutoka Misri, waliiga sikukuu fulani ya kipagani ya Wamisri na wakaita sikukuu hiyo, “sikukuu kwa ajili ya Yehova.” Lakini Yehova aliwapatia azabu ao malipizi juu ya jambo hilo. (Kutoka 32:2-10) Kama vile nabii Isaya alisema, hatupaswe ‘kugusa kitu chochote kichafu!’​—Soma Isaya 52:11.

TENDEA WENGINE KWA HESHIMA

13. Unaweza kujiuliza maulizo gani wakati unaamua kuacha kufanya sikukuu fulani?

13 Wakati unaamua kuacha kufanya sikukuu fulani, unaweza kujiuliza maulizo mingi. Kwa mufano: Ninaweza kujibu namna gani kama wafanyakazi wenzangu wananiuliza juu ya nini sifanyake sikukuu ya Noeli pamoja nao? Ninaweza kufanya nini kama mutu fulani ananipatia zawadi ya Noeli? Ninaweza kufanya nini kama bibi ao bwana yangu ananiomba nifanye sikukuu fulani? Namna gani ninaweza kusaidia watoto wangu wasihuzunike juu hawafanye sikukuu fulani ao sikukuu ya kuzaliwa kwao?

14, 15. Unaweza kufanya nini kama mutu fulani anakutakia sikukuu njema ao anakupatia zawadi?

14 Mu kila hali, ni jambo la maana kutumia akili ya muzuri wakati unaamua jambo lenye utasema ao kufanya. Kwa mufano, kama mutu anakutakia sikukuu njema, hautanyamaza. Unaweza tu kusema, “Aksanti.” Lakini kama mutu fulani anapenda kujua mambo mingi, unaweza kumuambia juu ya nini haufanyake sikukuu fulani. Lakini sikuzote, ufanye vile kwa upole, na kwa heshima, na usiseme mambo yenye yanaweza kumukwaza. Biblia inasema hivi: “Maneno yenu yakuwe yenye kupendeza sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mujue namna munapaswa kumujibu kila mutu.” (Wakolosai 4:6) Pengine unaweza kumuambia kama unapenda kupitisha wakati pamoja na wengine na kuwapatia zawadi lakini umeamua kuepuka kufanya vile wakati wa sikukuu hizo.

15 Unaweza kufanya nini kama mutu fulani anakupatia zawadi? Biblia haitupatie sheria juu ya kila jambo, lakini inasema kama tunapaswa kuendelea kuwa na zamiri ya muzuri. (1 Timoteo 1:18, 19) Pengine mutu mwenye anakupatia zawadi hajue kama haufanyake sikukuu hiyo. Ao anaweza kusema hivi: “Ninajua kama wewe haufanyake sikukuu hii, lakini ninapenda tu kukupatia zawadi.” Ikuwe anajua ao hapana, unaweza kuamua kama utakamata ile zawadi ao hapana. Lakini, kama unaamua kukubali ao kukataa, hakikisha kama unaendelea kuwa na zamiri ya muzuri. Hatupendi kufanya jambo lolote lenye linaweza kuharibu urafiki wetu pamoja na Yehova.

TENDEA KWA HESHIMA WATU WA FAMILIA YAKO

Watu wenye kumutumikia Yehova wako na furaha

16. Unaweza kufanya nini kama watu wa familia yako wanakuomba ufanye sikukuu fulani?

16 Unaweza kufanya nini kama watu wa familia yako wanakuomba ufanye sikukuu fulani? Usibishane nao. Ukumbuke kama wako na haki ya kuamua mambo yenye wanapenda kufanya. Uwatendee kwa adabu na uheshimie maamuzi yao kama vile wewe pia unapenda waheshimie maamuzi yako. (Soma Matayo 7:12.) Lakini utafanya nini kama watu wa familia yako wanapenda upitishe wakati pamoja nao wakati wa sikukuu fulani? Mbele ya kuamua jambo la kufanya, usali kwa Yehova ili akusaidie ukamate uamuzi wa muzuri. Ufikirie hali hiyo, na utafute habari juu ya hali hiyo. Ukumbuke kama, sikuzote unapenda kumufurahisha Yehova.

17. Namna gani unaweza kusaidia watoto wako wasijisikie kama wanakosa kitu fulani wakati wengine wanafanya sikukuu fulani?

17 Unaweza kufanya nini ili kusaidia watoto wako wasijisikie kama wanakosa kitu fulani wakati wanaona wengine wanafanya sikukuu fulani? Mara kwa mara, unaweza kuwafanyia jambo fulani lenye watafurahia. Tena, uzoee kuwapatia zawadi zenye hawakuwazia. Na zawadi ya muzuri zaidi yenye unaweza kupatia watoto wako ni kupitisha wakati pamoja nao na kuwaonyesha upendo.

UABUDU MUNGU MU NJIA YENYE ANAPENDA

18. Juu ya nini tunapaswa kuenda ku mikutano ya Kikristo?

18 Ili tumufurahishe Yehova, tunapaswa kuachana na dini za uongo na desturi na sikukuu zenye kuwa na upatano na dini za uongo. Lakini tunapaswa pia kumuabudu Mungu mu njia yenye anapenda. Namna gani? Kwa mufano, tunapaswa kuenda kila mara ku mikutano ya Kikristo. (Soma Waebrania 10:24, 25.) Mikutano ni sehemu ya maana sana ya ibada ya kweli. (Zaburi 22:22; 122:1) Tunaweza kutiana moyo wakati tunakusanyika pamoja.​—Waroma 1:12.

19. Juu ya nini ni jambo la maana kuambia wengine juu ya kweli za Biblia zenye umejifunza?

19 Kuambia wengine juu ya mambo yenye umejifunza mu Biblia ni sehemu ingine ya ibada ya kweli. Watu wengi wanasikia huzuni juu ya mambo ya mubaya yenye kufanyika mu dunia. Pengine unajua watu fulani wenye kujisikia vile. Uzungumuze nao juu ya tumaini lako la muzuri sana kwa ajili ya wakati wenye kuja. Kama unaenda kila mara ku mikutano ya Kikristo na kuambia wengine juu ya kweli ya Biblia, utaona kama hauna tena tamaa ya kujiunga na dini ya uongo na kufanya desturi zake. Unaweza kuwa hakika kama utakuwa na furaha na kama Yehova atakubariki sana wakati unachagua kumuabudu mu njia yenye anapenda.​—Malaki 3:10.