Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA SABA

Zawadi ya Sala

Zawadi ya Sala

“Muumba wa mbingu na dunia” yuko tayari kusikiliza sala zetu.—Zaburi 115:15

1, 2. Kwa nini unafikiri sala ni zawadi ya pekee sana, na kwa nini tunahitaji kujua mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu sala?

DUNIA ni ndogo sana inapolinganishwa na ulimwengu wote mzima. Hivyo, Yehova anapotazama dunia, watu katika mataifa yote huonekana kama tone dogo la maji kutoka katika ndoo. (Zaburi 115:15; Isaya 40:15) Hata hivyo, ingawa sisi tunaonekana kuwa wadogo sana tunapolinganishwa na ulimwengu wote mzima, andiko la Zaburi 145:18, 19 linasema hivi: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli. Hutosheleza tamaa ya wale wanaomwogopa; husikia kilio chao cha kuomba msaada, naye huwaokoa.” Hiyo ni heshima kubwa sana! Yehova, Muumba mweza yote anataka tumkaribie, na anataka kusikiliza sala zetu. Naam, sala ni zawadi, ni zawadi ya pekee ambayo Yehova amempatia kila mmoja wetu.

2 Hata hivyo, Yehova atatusikiliza ikiwa tu tunasali kwa njia anayoikubali. Tunawezaje kusali kwa njia hiyo? Acheni tuone jinsi Biblia inavyosema kuhusu jambo hilo.

KWA NINI TUSALI KWA YEHOVA?

3. Kwa nini tunapaswa kusali kwa Yehova?

3 Yehova anataka usali au uwasiliane naye. Tunajuaje? Tafadhali soma Wafilipi 4:6, 7Hebu fikiria mwaliko huo. Mtawala wa ulimwengu wote mzima anakujali sana hivi kwamba anakualika umweleze hisia na matatizo yako.

4. Kusali kwa ukawaida kunawezaje kuimarisha urafiki wako pamoja na Yehova?

4 Sala hutusaidia kuwa na urafiki wa karibu pamoja na Yehova. Marafiki wa kweli wanapozungumza kwa ukawaida kuhusu maoni, mahangaiko, na hisia zao, urafiki wao unaimarika zaidi. Hivyo ndivyo ilivyo kuhusu uhusiano wetu pamoja na Yehova. Kupitia Biblia, anakujulisha maoni na hisia zake, na pia anakueleza mambo atakayofanya wakati ujao. Unaweza kumweleza hisia zako za ndani kabisa kwa kusali kwa ukawaida. Unapofanya hivyo, urafiki wako pamoja na Yehova utaimarika zaidi.—Yakobo 4:8.

TUNAPASWA KUFANYA NINI ILI MUNGU ASIKILIZE SALA ZETU?

5. Tunajuaje kwamba Yehova hasikilizi sala zote?

5 Je, Yehova husikiliza sala zote? Hapana. Wakati wa nabii Isaya, Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: “Ingawa mnatoa sala nyingi, mimi sisikilizi; mikono yenu imejaa damu.” (Isaya 1:15) Kwa hiyo, tusipokuwa waangalifu tunaweza kufanya mambo yanayotutenga na Yehova, hivyo kufanya asisikilize sala zetu.

6. Kwa nini ni muhimu kuwa na imani? Unawezaje kuonyesha kwamba una imani?

6 Ikiwa tunataka Yehova asikilize sala zetu, ni lazima tumwamini. (Marko 11:24) Mtume Paulo alisema hivi: “Bila imani haiwezekani kumpendeza Mungu vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kuwa yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Hata hivyo, haitoshi tu kusema kwamba tuna imani. Tunapaswa kuonyesha wazi imani yetu kwa kumtii Yehova kila siku.—Soma Yakobo 2:26.

7. (a) Kwa nini tunapaswa kuwa na heshima na unyenyekevu tunaposali kwa Yehova? (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba sisi ni wanyoofu tunaposali?

7 Tunahitaji kuwa na heshima na unyenyekevu tunaposali kwa Yehova. Kwa nini? Ikiwa tungepewa nafasi ya kuzungumza na mfalme au rais, tungefanya hivyo kwa heshima. Yehova ni Mungu Mweza yote, kwa hiyo tunahitaji kuwa na heshima na unyenyekevu mwingi zaidi tunapozungumza naye. (Mwanzo 17:1; Zaburi 138:6) Pia, tunapaswa kuwa wanyoofu na kusali kwa Yehova kutoka moyoni, na sio kusali kwa kurudia maneno yaleyale tena na tena.—Mathayo 6:7, 8.

8. Tunaposali kuhusu jambo fulani, tunapaswa kufanya jambo gani lingine?

8 Mwishowe, tunaposali kuhusu jambo fulani, tunahitaji kufanya yote tunayoweza ili kutenda kulingana na sala zetu. Kwa mfano, ikiwa tumesali kwa Yehova atusaidie kupata mahitaji ya siku, na tuna uwezo wa kufanya kazi hatupaswi kuwa wavivu tukitarajia kwamba Yehova atatupatia kila kitu. Ni lazima tufanye kwa bidii kazi yoyote tunayoweza kufanya. (Mathayo 6:11; 2 Wathesalonike 3:10) Ikiwa tumesali kwa Yehova atusaidie kuacha kufanya jambo fulani baya, ni lazima tujitahidi kuepuka hali yoyote inayoweza kutuingiza kwenye kishawishi. (Wakolosai 3:5) Acheni sasa tuchunguze baadhi ya maswali ambayo watu hujiuliza kwa ukawaida kuhusu sala.

MASWALI YANAYOULIZWA KUHUSU SALA

9. Tunapaswa kusali kwa nani? Andiko la Yohana 14:6 linatufundisha nini kuhusu sala?

9 Tunapaswa kusali kwa nani? Yesu aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni.” (Mathayo 6:9) Pia, alisema hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Kwa hiyo, tunahitaji kusali kwa Yehova peke yake kupitia kwa Yesu. Inamaanisha nini kusali kupitia kwa Yesu? Ili Yehova asikilize sala zetu, tunahitaji kuheshimu mgawo wa pekee ambao Yehova amempatia Yesu. Kama tulivyojifunza, Yesu alikuja duniani ili kutukomboa kutokana na dhambi na kifo. (Yohana 3:16; Waroma 5:12) Pia, Yehova amemweka Yesu kuwa Kuhani Mkuu na Hakimu.—Yohana 5:22; Waebrania 6:20.

Unaweza kusali wakati wowote

10. Je, ni lazima tukae kwa njia fulani hususa tunaposali? Eleza.

10 Je, ni lazima tukae kwa njia fulani hususa? Hapana, Yehova hatuambii tupige magoti, tukae, au tusimame wakati tunaposali. Biblia inatufundisha kwamba tunaweza kuzungumza na Yehova tukiwa tumekaa kwa njia mbalimbali lakini kwa heshima. (1 Mambo ya Nyakati 17:16; Nehemia 8:6; Danieli 6:10; Marko 11:25) Jambo muhimu sana kwa Yehova si kukaa kwa njia fulani hususa bali ni kusali tukiwa na nia nzuri. Tunaweza kusali kwa sauti au kimyakimya mahali popote na wakati wowote iwe mchana au usiku. Tunaposali kwa Yehova, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atatusikiliza hata ikiwa sala hiyo ni ya kimyakimya.—Nehemia 2:1-6.

11. Tunaweza kusali kwa Yehova kuhusu mambo gani?

11 Tunaweza kusali kuhusu nini? Tunaweza kusali kuhusu jambo lolote kulingana na mapenzi ya Yehova. Biblia inasema hivi: “Tukiomba chochote kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1 Yohana 5:14) Je, tunaweza kusali kuhusu mambo ya kibinafsi? Ndiyo. Kusali kwa Yehova kunapaswa kuwa sawa na kuzungumza na rafiki wa karibu. Tunaweza kumweleza Yehova jambo lolote tunalofikiria au lililo moyoni mwetu. (Zaburi 62:8) Tunaweza kusali kwake ili atupatie roho takatifu itusaidie kufanya yaliyo sawa. (Luka 11:13) Tunaweza kusali kwa Yehova atupatie hekima ili tufanye maamuzi kwa njia nzuri, pia tunaweza kusali ili atupatie nguvu za kushinda hali ngumu. (Yakobo 1:5) Tunapaswa kumwomba Yehova atusamehe dhambi zetu. (Waefeso 1:3, 7) Pia, tunapaswa kusali kwa ajili ya wengine, kutia ndani familia yetu na ndugu na dada kutanikoni.—Matendo 12:5; Wakolosai 4:12.

12. Ni mambo gani muhimu tunayoweza kutaja katika sala zetu?

12 Tunapaswa kutanguliza mambo gani katika sala zetu? Tunapaswa kumtanguliza Yehova na mapenzi yake. Tunaweza kumshukuru kutoka moyoni kwa mambo yote ambayo ametufanyia. (1 Mambo ya Nyakati 29:10-13) Tunajua jambo hilo kwa sababu Yesu alipokuwa duniani aliwafundisha wanafunzi wake jinsi ya kusali. (Soma Mathayo 6:9-13.) Alisema kwamba wanapaswa kusali kwanza kuhusu kutakaswa kwa jina la Mungu, yaani, waliheshimu na kuliona kuwa takatifu. Kisha Yesu alisema kwamba tunapaswa kusali Ufalme wa Mungu uje ili kufanya mapenzi ya Yehova hapa duniani. Baada ya kusali kuhusu mambo hayo muhimu, Yesu alisema kwamba tunaweza kusali kuhusu mahitaji yetu. Tunaonyesha mambo yaliyo muhimu zaidi katika maisha yetu ikiwa tutamtanguliza Yehova na mapenzi yake katika sala zetu.

13. Sala zetu zinapaswa kuwa na urefu gani?

13 Sala zetu zinapaswa kuwa na urefu gani? Biblia haisemi kuhusu jambo hilo. Sala zetu zinaweza kuwa ndefu au fupi ikitegemea hali. Kwa mfano, kabla ya kula tunaweza kutoa sala fupi lakini tunaweza kutoa sala ndefu tunapomshukuru Yehova au tunapomweleza mahangaiko yetu. (1 Samweli 1:12, 15) Hatungependa kutoa sala ndefu ili tu kujionyesha, kama ambavyo baadhi ya watu walifanya katika siku za Yesu. (Luka 20:46, 47) Yehova hapendezwi na sala kama hizo. Jambo muhimu kwa Yehova ni kusali kutoka moyoni.

14. Tunapaswa kusali mara ngapi, na jambo hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova?

14 Tunapaswa kusali mara ngapi? Yehova anatualika tuwasiliane naye kwa ukawaida. Biblia inasema kwamba tunapaswa “kusali bila kuacha,” ‘kudumu katika sala’ na ‘kusali sikuzote.’ (Mathayo 26:41; Waroma 12:12; 1 Wathesalonike 5:17) Yehova yuko tayari kutusikiliza wakati wowote. Tunaweza kumshukuru kila siku kwa sababu ya upendo na ukarimu wake. Pia, tunaweza kumwomba atupatie mwongozo, nguvu na faraja. Kwa kweli, ikiwa tunaithamini sana zawadi hii ya sala, tutatumia kila fursa tunayopata ili kusali kwake.

15. Kwa nini tunapaswa kusema “amina” mwishoni mwa sala?

15 Kwa nini tunapaswa kusema “amina” mwishoni mwa sala? Neno “amina” humaanisha “bila shaka” au “na iwe hivyo.” Ni njia ya kuonyesha kwamba tunakubaliana na yale yaliyotajwa katika sala, na hilo linamaanisha kwamba sisi ni wanyoofu. (Zaburi 41:13) Biblia inatufundisha kwamba ni vizuri pia kusema “amina,” kimyakimya au kwa sauti, mwishoni mwa sala inayotolewa kwa ajili ya watu wote ili kuonyesha kwamba tunakubaliana na yale yaliyotajwa.—1 Mambo ya Nyakati 16:36; 1 Wakorintho 14:16.

JINSI MUNGU ANAVYOJIBU SALA ZETU

16. Je, kweli Yehova husikiliza sala zetu? Fafanua.

16 Je, kweli Yehova hujibu sala zetu? Ndiyo. Biblia inasema kwamba yeye ni “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Yehova husikiliza na kujibu sala zinazotolewa kwa unyoofu na mamilioni ya watu, naye hujibu kwa njia mbalimbali.

17. Yehova anawatumiaje malaika na watumishi wake walio duniani kujibu sala zetu?

17 Yehova huwatumia malaika na watumishi wake walio duniani kujibu sala zetu. (Waebrania 1:13, 14) Kuna mifano mingi ya watu ambao walisali ili wapate msaada wa kuielewa Biblia na baada ya muda mfupi wakatembelewa na Shahidi wa Yehova. Biblia inaonyesha kwamba malaika wanashiriki kutangaza “habari njema” duniani kote. (Soma Ufunuo 14:6.) Pia, huenda tumewahi kusali kwa Yehova kuhusu tatizo fulani hususa kisha tukapokea msaada tuliohitaji kutoka kwa Wakristo wenzetu.—Methali 12:25; Yakobo 2:16.

Yehova anaweza kujibu sala zetu kupitia msaada tunaopokea kutoka kwa Wakristo wenzetu

18. Yehova anaitumiaje roho takatifu na Biblia kujibu sala zetu?

18 Yehova hutumia roho yake takatifu kujibu sala zetu. Tunapoomba msaada wa kukabiliana na tatizo fulani, anaweza kutumia roho yake takatifu kutupatia mwongozo na kutuimarisha. (2 Wakorintho 4:7) Pia, Yehova hutumia Biblia kujibu sala zetu na kutusaidia kufanya maamuzi kwa hekima. Tunaposoma Biblia, tunaweza kupata maandiko fulani yanayoweza kutusaidia. Yehova anaweza kumchochea mtu fulani kutoa maelezo yanayoweza kutusaidia katika mikutano au anaweza kumtumia mzee wa kutaniko atusomee jambo fulani lenye kutia moyo katika Biblia.—Wagalatia 6:1.

19. Kwa nini nyakati fulani huenda ikaonekana kwamba Yehova hajajibu sala zetu?

19 Nyakati fulani huenda tukajiuliza hivi: ‘Kwa nini Yehova bado hajajibu sala zangu?’ Kumbuka kwamba yeye anajua wakati na njia inayofaa ya kujibu sala zetu. Anajua kile tunachohitaji hasa. Hivyo, tunapoendelea kusali kuhusu jambo hilo tunaonyesha wazi kwamba tuna uhitaji na pia tuna imani kumwelekea. (Luka 11:5-10) Nyakati nyingine Yehova hujibu sala zetu kwa njia tusiyotarajia. Kwa mfano, tunaweza kusali kuhusu hali fulani ngumu tunayokabili, hata hivyo, badala ya kuondoa tatizo hilo, anaweza kutupatia nguvu za kuendelea kuvumilia.—Soma Wafilipi 4:13.

20. Kwa nini tunapaswa kusali kwa Yehova mara nyingi zaidi?

20 Kwa kweli ni heshima kubwa kuwasiliana na Yehova katika sala! Tunaweza kuwa na hakika kwamba atatusikiliza. (Zaburi 145:18) Kadiri tunavyosali mara nyingi kwa Yehova kutoka moyoni, ndivyo urafiki wetu pamoja naye utakavyoimarika.