Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA NANE

Je, Ninapaswa Kujiweka Wakfu kwa Mungu na Kubatizwa?

Je, Ninapaswa Kujiweka Wakfu kwa Mungu na Kubatizwa?

1. Huenda ukajiuliza swali gani baada ya kujifunza kwa makini kitabu hiki?

UMEJIFUNZA kweli nyingi za Biblia katika kitabu hiki, kama vile ahadi ya Mungu ya uzima wa milele, hali ya wafu, na tumaini la ufufuo. (Mhubiri 9:5; Luka 23:43; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:3, 4) Labda umeanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova na unaamini kwamba ibada yao ni ya kweli. (Yohana 13:35) Huenda umeanza kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yehova, na umeamua kumtumikia. Basi huenda ukajiuliza, ‘Ninapaswa kufanya nini ili nimtumikie Mungu?’

2. Ni nini kilichomchochea mwanamume Mwethiopia atake kubatizwa?

2 Hivyo ndivyo alivyohisi mwanamume fulani Mwethiopia aliyeishi wakati wa Yesu. Muda fulani baada ya Yesu kufufuliwa, Filipo, mwanafunzi wa Yesu alimhubiria mwanamume huyo. Filipo alimhakikishia mwanamume huyo kuwa Yesu alikuwa Masihi. Mwanamume Mwethiopia alichochewa sana na mambo aliyojifunza, hivi kwamba akasema: “Tazama! Hapa kuna maji; ni nini kinachonizuia kubatizwa?”—Matendo 8:26-36.

3. (a) Yesu aliwaamuru wanafunzi wake wafanye nini? (b) Mtu anapaswa kubatizwa jinsi gani?

3 Biblia inafundisha wazi kwamba ili umtumikie Yehova unapaswa kubatizwa. Yesu aliwaamuru wafuasi wake ‘wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote na kuwabatiza.’ (Mathayo 28:19) Yesu alituwekea kielelezo alipobatizwa. Yesu hakunyunyiziwa maji kichwani bali alizamishwa kabisa ndani ya maji. (Mathayo 3:16) Leo pia, Mkristo anapobatizwa, ni lazima azamishwe kabisa ndani ya maji.

4. Unapobatizwa unawaonyesha nini wengine?

4 Unapobatizwa, unawaonyesha wengine kwamba unataka kuwa rafiki ya Mungu na ungependa kumtumikia. (Zaburi 40:7, 8) Hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Ninapaswa kufanya nini ili nibatizwe?’

UJUZI NA IMANI

5. (a) Kabla ya kubatizwa unapaswa kufanya nini? (b) Kwa nini ni muhimu kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kikristo?

5 Kabla ya kubatizwa, ni lazima umjue Yehova na Yesu. Umeanza kupata ujuzi huo kwa kujifunza Biblia. (Soma Yohana 17:3.) Ujuzi peke yake hautoshi. Biblia inasema kwamba ni lazima ‘tujazwe ujuzi sahihi’ wa mapenzi ya Yehova. (Wakolosai 1:9) Mikutano ya Mashahidi wa Yehova itakusaidia kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova. Hiyo ni sababu moja muhimu ya kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.—Waebrania 10:24, 25.

Kabla ya kubatizwa, ni lazima ujifunze Biblia

6. Unapaswa kuwa na ujuzi wa Biblia kadiri gani ili ubatizwe?

6 Ni kweli kwamba Yehova hatazamii ujue kila kitu katika Biblia ili ubatizwe. Yehova hakutazamia Mwethiopia ajue kila kitu ili abatizwe. (Matendo 8:30, 31) Tutaendelea kujifunza kumhusu Yehova milele. (Mhubiri 3:11) Hata hivyo, ili ubatizwe unapaswa kujua na kukubali mafundisho ya msingi ya Biblia.—Waebrania 5:12.

7. Kujifunza Biblia kumekusaidiaje?

7 Biblia inasema: “Bila imani haiwezekani kumpendeza Mungu.” (Waebrania 11:6) Hivyo, ili ubatizwe unapaswa kuwa na imani. Biblia inasema kwamba watu fulani katika jiji la kale la Korintho walisikia mafundisho ya wafuasi wa Yesu, nao “wakaanza kuamini na kubatizwa.” (Matendo 18:8) Vivyo hivyo, kujifunza Biblia kumekusaidia kuamini ahadi za Mungu na nguvu ya dhabihu ya Yesu inayoweza kutuokoa kutokana na dhambi na kifo.—Yoshua 23:14; Matendo 4:12; 2 Timotheo 3:16, 17.

ZUNGUMZA NA WENGINE KUHUSU KWELI ZA BIBLIA

8. Ni nini kitakuchochea kuwaeleza wengine kuhusu mambo ambayo umejifunza?

8 Kadiri unavyojifunza Biblia na kuona faida zake maishani ndivyo imani yako itakavyozidi kuimarika. Utachochewa kuwaeleza wengine mambo unayojifunza. (Yeremia 20:9; 2 Wakorintho 4:13) Hata hivyo, utawahubiria nani?

Imani inapaswa kukuchochea kuwaambia wengine kuhusu mambo unayoamini

9, 10. (a) Unaweza kuanza kuwahubiria nani mambo ambayo umejifunza? (b) Unapaswa kufanya nini ikiwa unataka kuhubiri na kutaniko?

9 Unaweza kuzungumza na watu wa familia, marafiki, majirani, au wafanyakazi wenzako mambo unayojifunza. Hata hivyo, uwe mwenye fadhili na upendo unapozungumza nao. Baadaye, unaweza kuanza kuhubiri na kutaniko. Ukihisi kwamba ungependa kuanza kuhubiri na kutaniko, mjulishe yule anayekufundisha Biblia. Ikiwa yule anayekufundisha Biblia anaona kwamba unastahili na unaishi kulingana na viwango vya Biblia, mipango itafanywa ili wewe na mwalimu wako mzungumze pamoja na wazee wawili wa kutaniko.

10 Ni mambo gani yatakayozungumziwa katika mkutano huo? Wazee watazungumza na wewe ili kujua kama unaelewa na kuamini mafundisho ya msingi ya Biblia, kama unaishi kulingana na kanuni za Biblia, na kama kweli unataka kuwa Shahidi wa Yehova. Kumbuka kwamba wazee wanalichunga kutaniko lote, kutia ndani wewe, hivyo usiogope kuzungumza nao. (Matendo 20:28; 1 Petro 5:2, 3) Baada ya mkutano huo, wazee watakujulisha ikiwa unastahili kuanza kuhubiri na kutaniko.

11. Kwa nini ni muhimu kufanya mabadiliko kabla ya kuanza kuhubiri na kutaniko?

11 Huenda wazee wakakushauri ufanye mabadiliko fulani kabla ya kuanza kuhubiri na kutaniko. Kwa nini ni muhimu kufanya mabadiliko hayo? Kwa sababu tunapozungumza na wengine kumhusu Mungu, tunamwakilisha Yehova nasi tunapaswa kuishi kwa njia inayomheshimu.—1 Wakorintho 6:9, 10; Wagalatia 5: 19-21.

TUBU NA UGEUKE

12. Kwa nini sote tunapaswa kutubu?

12 Kuna jambo lingine ambalo unapaswa kufanya kabla ya kubatizwa. Mtume Petro alisema hivi: “Kwa hiyo, tubuni na mgeuke ili dhambi zenu zifutwe.” (Matendo 3:19) Kutubu kunamaanisha nini? Kunamaanisha kusikitikia na kujutia makosa ambayo umefanya. Kwa mfano, ikiwa ulikuwa mwasherati, unapaswa kutubu. Hata ikiwa ulijitahidi kuishi maisha safi, unapaswa kutubu kwa sababu sote ni watenda dhambi na hivyo tunapaswa kumwomba Mungu msamaha.—Waroma 3:23; 5:12.

13. ‘Kugeuka’ kunamaanisha nini?

13 Je, inatosha tu kusikitikia na kujutia dhambi ambazo umefanya? La. Mtume Petro alisema kwamba unapaswa ‘kugeuka.’ Hilo linamaanisha kwamba unapaswa kuacha kabisa mwenendo mbaya wa zamani na kuanza kufanya mambo mema. Kwa mfano, wazia kwamba unasafiri kwenda eneo fulani kwa mara ya kwanza. Baada ya muda, unatambua kwamba unaelekea upande usiofaa. Utafanya nini? Bila shaka, utapunguza mwendo, utasimama na kugeuka, kisha ufuate njia inayofaa. Vivyo hivyo, unapoendelea kujifunza Biblia, utatambua kwamba kuna mazoea au tabia ambazo unapaswa kuacha. Uwe tayari ‘kugeuka,’ yaani, kufanya mabadiliko yanayofaa, na kuanza kutenda mema.

JIWEKE WAKFU

Je, umemwahidi Yehova kwamba utamtumikia?

14. Unajiweka wakfu kwa Yehova jinsi gani?

14 Kujiweka wakfu kwa Yehova ni hatua nyingine muhimu unayopaswa kuchukua kabla ya kubatizwa. Unapojiweka wakfu kwa Yehova katika sala, unamwahidi kwamba utamwabudu yeye peke yake na kutanguliza mapenzi yake maishani.—Kumbukumbu la Torati 6:15.

15, 16. Ni nini kinachomchochea mtu kujiweka wakfu kwa Mungu?

15 Unapomwahidi Yehova kwamba utamtumikia ni sawa na kumwahidi mtu unayempenda kwamba mtaishi pamoja katika maisha yenu yote. Wazia kwamba mwanamume na mwanamke wanaanzisha urafiki. Kadiri mwanamume anavyomjua mwanamke huyo vizuri atazidi kumpenda na atataka kumwoa. Ingawa huo ni uamuzi mzito, mwanamume huyo yuko tayari kukubali wajibu huo kwa sababu anampenda.

16 Kadiri unavyojifunza mengi kumhusu Yehova, ndivyo utakavyompenda zaidi na kutaka kumtumikia. Hilo litakuchochea kusali na kumwahidi kumtumikia. Biblia inasema kwamba yeyote anayetaka kumfuata Yesu lazima “ajikane mwenyewe.” (Marko 8:34) Inamaanisha nini? Inamaanisha kwamba kumtii Yehova kutakuwa jambo kuu katika maisha yako. Kutanguliza mapenzi ya Yehova kutakuwa muhimu kuliko malengo na mambo unayopenda.—Soma 1 Petro 4:2.

USIOGOPE KUSHINDWA

17. Kwa nini baadhi ya watu wanaogopa kujiweka wakfu kwa Yehova?

17 Baadhi ya watu hawataki kujiweka wakfu kwa Yehova kwa sababu wanaogopa kwamba watashindwa kuendelea kumtumikia. Huenda wanaogopa kwamba watamkosea, au wanafikiri kwamba wasipojiweka wakfu, hawatawajibika mbele za Yehova.

18. Ni nini kitakachokusaidia kushinda hofu ya kumkosea Yehova?

18 Upendo wako kwa Yehova utakusaidia kushinda hofu ya kumkosea. Kwa kuwa unampenda, utajitahidi kutimiza ahadi yako. (Mhubiri 5:4; Wakolosai 1:10) Haitakuwa vigumu kwako kufanya mapenzi ya Yehova. Mtume Yohana aliandika hivi: “Kwa maana kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 Yohana 5:3.

19. Kwa nini hupaswi kuogopa kujiweka wakfu kwa Yehova?

19 Si lazima uwe mkamilifu ili ujiweke wakfu kwa Yehova. Hatazamii tufanye mambo yanayozidi uwezo wetu. (Zaburi 103:14) Atakusaidia kufanya mema. (Isaya 41:10) Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote, “naye atavinyoosha vijia vyako.”—Methali 3:5, 6.

TANGAZO LA HADHARANI LA WOKOVU

20. Unapaswa kuchukua hatua gani nyingine baada ya kujiweka wakfu?

20 Je, unafikiri uko tayari kujiweka wakfu kwa Yehova? Ukijiweka wakfu utakuwa tayari kwa hatua nyingine. Hatua hiyo ni kubatizwa.

21, 22. Unatoaje “tangazo la hadharani” la imani yako?

21 Mjulishe mratibu wa baraza la wazee wa kutaniko lenu kwamba umejiweka wakfu kwa Yehova na ungependa kubatizwa. Kisha, atapanga baadhi ya wazee wapitie mafundisho ya msingi ya Biblia pamoja nawe. Wakiona unastahili, watakujulisha kwamba utabatizwa katika kusanyiko linalofuata la Mashahidi wa Yehova. Kusanyikoni, hotuba inayoeleza maana ya ubatizo itatolewa. Kisha, msemaji wa hotuba hiyo atawaomba walio tayari kwa ubatizo wajibu maswali mawili rahisi. Kwa kujibu maswali hayo, utafanya “tangazo la hadharani” la imani yako.—Waroma 10:10.

22 Kisha utabatizwa. Utazamishwa kabisa ndani ya maji. Kwa kubatizwa, utawaonyesha watazamaji kwamba umejiweka wakfu kwa Yehova na sasa wewe ni Shahidi wa Yehova.

MAANA YA UBATIZO WAKO

23. Inamaanisha nini kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu”?

23 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangebatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Soma Mathayo 28:19.) Inamaanisha nini? Inamaanisha kutambua mamlaka ya Yehova na fungu la Yesu katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu, na jinsi Mungu anavyotumia roho takatifu kutimiza mapenzi yake.—Zaburi 83:18; Mathayo 28:18; Wagalatia 5:22, 23; 2 Petro 1:21.

Unapobatizwa, unaonyesha kwamba unataka kufanya mapenzi ya Mungu

24, 25. (a) Ubatizo unamaanisha nini? (b) Tutazungumzia nini katika sura ya mwisho ya kitabu hiki?

24 Ubatizo unawakilisha jambo muhimu sana. Kuzamishwa katika maji, kunamaanisha kwamba umekufa au umeacha maisha yako ya zamani. Unapoinuka kutoka katika maji, utaanza maisha mapya yaani kufanya mapenzi ya Mungu. Inamaanisha kwamba kuanzia sasa na kuendelea utamtumikia Yehova. Kumbuka kwamba hujajiweka wakfu kwa mwanadamu, shirika, au kazi fulani. Umejiweka wakfu kwa Yehova.

25 Kujiweka wakfu kutakusaidia kuimarisha urafiki wako pamoja na Mungu. (Zaburi 25:14) Hilo halimaanishi kwamba mtu ataokolewa kwa sababu tu amebatizwa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.” (Wafilipi 2:12) Ubatizo ni mwanzo tu. Hata hivyo, unawezaje kukaa karibu na Yehova? Sura ya mwisho ya kitabu hiki itajibu swali hilo.