Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA TISA

Kaa Karibu na Yehova

Kaa Karibu na Yehova

1, 2. Tunaweza kupata wapi kimbilio?

WAZIA kwamba unatembea katika dhoruba kali. Mawingu yanazidi kutanda, radi zinapiga, na ngurumo zinasikika. Kisha mvua kubwa inaanza kunyesha. Unatafuta mahali pa kujificha. Bila shaka, unafurahi sana unapopata mahali salama!

2 Tunaishi katika kipindi kinachofanana na hali hiyo. Hali za ulimwengu zinazidi kuwa mbaya. Huenda ukajiuliza, ‘Ninaweza kupata wapi kimbilio?’ Mwandikaji wa zaburi aliandika hivi: “Nitamwambia Yehova: ‘Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu, ninayemtumaini.’” (Zaburi 91:2) Yehova anaweza kutupatia kitulizo cha matatizo yetu ya sasa, na pia tumaini zuri la wakati ujao.

3. Tunawezaje kumfanya Yehova kuwa kimbilio letu?

3 Yehova anawezaje kutulinda? Anaweza kutusaidia kukabiliana na matatizo yetu, na ana nguvu kuliko mtu yeyote anayetaka kutudhuru. Hata ikiwa tutapatwa na jambo fulani baya kwa sasa, tuna uhakika kwamba Yehova atarekebisha hali hiyo wakati ujao. Biblia inatusihi hivi: “Mwendelee kujitunza katika upendo wa Mungu.” (Yuda 21) Tunahitaji kukaa karibu na Yehova ili atusaidie tunapokabili hali ngumu. Lakini, tunawezaje kufanya hivyo?

TENDA KULINGANA NA UPENDO WA MUNGU

4, 5. Yehova ameonyeshaje kwamba anatupenda?

4 Ili tukae karibu na Yehova tunahitaji kutambua jinsi anavyotupenda. Fikiria mambo yote mazuri ambayo Yehova ametufanyia. Ametupatia dunia maridadi na kuijaza mimea na wanyama wenye kupendeza. Pia, ametupatia vyakula vitamu na maji safi ya kunywa. Kupitia Biblia, Yehova ametufundisha jina na sifa zake nzuri. Zaidi ya yote, alionyesha kwamba anatupenda alipomtuma Mwana wake mpendwa, Yesu, aje duniani ili atoe uhai wake kwa ajili yetu. (Yohana 3:16) Kwa sababu ya dhabihu hiyo, tuna tumaini zuri la wakati ujao.

5 Yehova amesimamisha Ufalme wa Kimasihi, yaani, serikali ya mbinguni ambayo hivi karibuni itaondoa mateso yote. Ufalme huo utaifanya dunia kuwa paradiso, ambayo kila mtu ataishi kwa amani na furaha milele. (Zaburi 37:29) Njia nyingine ambayo Yehova ameonyesha kwamba anatupenda ni kwa kutufundisha jinsi ya kuishi maisha bora sasa. Pia, anatualika tusali kwake, na sikuzote yuko tayari kutusikiliza. Kwa kweli, Yehova ameonyesha kwamba anampenda kila mmoja wetu.

6. Tunapaswa kuitikiaje upendo wa Yehova?

6 Tunapaswa kuitikiaje upendo wa Yehova? Mshukuru kwa yote aliyokufanyia. Inasikitisha kwamba watu wengi leo, hawana shukrani. Ilikuwa hivyo Yesu alipokuwa duniani. Wakati fulani, Yesu aliwaponya watu kumi wenye ukoma, lakini ni mmoja tu aliyemshukuru. (Luka 17:12-17) Tungependa kuwa kama mtu huyo aliyemshukuru Yesu. Sikuzote tunataka kuwa wenye shukrani kwa Yehova.

7. Tunapaswa kumpenda Yehova kadiri gani?

7 Pia, tunapaswa kumpenda Yehova. Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba lazima wampende Yehova kwa moyo, nafsi, na akili yao yote. (Soma Mathayo 22:37.) Inamaanisha nini?

8, 9. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunampenda Yehova?

8 Je, inatosha tu kusema tunampenda Yehova? Hapana. Ikiwa tunampenda Yehova kwa moyo, nafsi, na akili yetu yote, tutaonyesha hivyo kwa matendo. (Mathayo 7:16-20) Biblia inafundisha wazi kwamba ikiwa tunampenda Mungu, tutatii amri zake. Je, ni vigumu kufanya hivyo? Hapana, kwa sababu “amri zake [Yehova] si mzigo mzito.”—Soma 1 Yohana 5:3.

9 Tunapomtii Yehova, tunakuwa na furaha na maisha bora. (Isaya 48:17, 18) Hata hivyo, ni nini kitakachotusaidia kukaa karibu na Yehova? Acha tuone.

ENDELEA KUMKARIBIA YEHOVA

10. Kwa nini unapaswa kuendelea kujifunza kumhusu Yehova?

10 Ulianzaje kuwa rafiki ya Yehova? Kupitia kujifunza Biblia, umemjua zaidi Yehova na umeboresha urafiki pamoja naye. Urafiki huo ni kama moto ambao ungependa uendelee kuwaka. Kama tu moto unavyohitaji kuni ili uendelee kuwaka, unahitaji kuendelea kujifunza kumhusu Yehova ili urafiki wenu uwe imara zaidi.—Methali 2:1-5.

Kama moto, upendo wako kwa Yehova unahitaji kuongezwa kuni ili uendelee kuwaka

11. Utafaidikaje kwa kujifunza Biblia?

11 Unapoendelea kujifunza Biblia, utajifunza mambo mengi yanayokugusa moyo. Ona jinsi wanafunzi wawili wa Yesu walivyohisi Yesu alipokuwa akiwafafanulia unabii wa Biblia. Walisema hivi: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akizungumza nasi barabarani, na alipokuwa akitufungulia Maandiko waziwazi?”—Luka 24:32.

12, 13. (a) Upendo wetu kwa Mungu unaweza kupatwa na nini? (b) Tunaweza kufanya nini ili upendo wetu kwa Yehova usipoe?

12 Kama tu mioyo ya wanafunzi wa Yesu ilivyoguswa walipoelewa Maandiko, huenda ulihisi hivyo ulipoanza kuielewa Biblia. Jambo hilo lilikusaidia kumjua Yehova na kumpenda. Hungependa upendo huo upoe.—Mathayo 24:12.

13 Mara tu unapokuwa rafiki ya Mungu, unahitaji kufanya yote unayoweza ili urafiki wenu uwe imara. Lazima uendelee kujifunza kumhusu Yehova na Yesu na utafakari mambo unayojifunza na jinsi unavyoweza kuyatumia maishani. (Yohana 17:3) Unaposoma au kujifunza Biblia, jiulize: ‘Jambo hili linanifundisha nini kumhusu Yehova? Kwa nini ninapaswa kumpenda kwa moyo na nafsi yangu yote?’—1 Timotheo 4:15.

14. Sala inatusaidiaje kuimarisha upendo wetu kwa Yehova?

14 Unapokuwa na rafiki, unawasiliana naye kwa ukawaida, na jambo hilo linaimarisha urafiki wenu. Vivyo hivyo, tunapowasiliana na Yehova kwa ukawaida katika sala, upendo wetu kwake utaimarika zaidi. (Soma 1 Wathesalonike 5:17.) Sala ni zawadi bora kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. Tunapaswa kuwasiliana naye kutoka moyoni. (Zaburi 62:8) Hatupaswi kukariri sala zetu, badala yake tunapaswa kusali kutoka moyoni. Kwa kweli, ikiwa tutaendelea kujifunza Biblia na kusali kutoka moyoni, upendo wetu kwa Yehova utaimarika.

KUWAAMBIA WENGINE KUMHUSU YEHOVA

15, 16. Unaionaje kazi ya kuhubiri?

15 Pia, ikiwa tunapenda kuendelea kuwa karibu na Yehova, tunapaswa kuwaambia wengine kuhusu imani yetu. Kuwaambia wengine kuhusu Yehova ni heshima kubwa sana. (Luka 1:74) Na ni wajibu ambao Yesu aliwapa Wakristo wote wa kweli. Sote tunapaswa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Je, unafanya hivyo?—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

16 Mtume Paulo aliiona kazi ya kuhubiri kuwa “hazina.” (2 Wakorintho 4:7) Kuwahubiria wengine kumhusu Yehova na makusudi yake ndiyo kazi muhimu ambayo unaweza kufanya. Ni njia nyingine ya kumtumikia Yehova, na anathamini yale unayofanya kwa ajili yake. (Waebrania 6:10) Unapohubiri unafaidika wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza kwa sababu kufanya hivyo kunawasaidia nyote kumkaribia Yehova na kupata uzima wa milele. (Soma 1 Wakorintho 15:58.) Hakuna kazi nyingine yoyote inayoridhisha kuliko kazi ya kuhubiri.

17. Kwa nini kazi ya kuhubiri inahitaji kufanywa haraka?

17 Kazi ya kuhubiri inahitaji kufanywa haraka sana. Tunapaswa ‘kulihubiri neno,’ na tunapaswa ‘kufanya hivyo kwa uharaka.’ (2 Timotheo 4:2) Watu wanahitaji kusikia kuhusu Ufalme wa Mungu. Biblia inasema: “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu! Iko karibu, nayo inakuja haraka sana!” Mwisho ‘hautachelewa!’ (Sefania 1:14; Habakuki 2:3) Kwa kweli, hivi karibuni, Yehova atauharibu ulimwengu mwovu wa Shetani. Kabla ya hilo kutukia, watu wanahitaji kuonywa ili waamue kumtumikia Yehova.

18. Kwa nini tunapaswa kumwabudu Yehova pamoja na Wakristo wa kweli?

18 Yehova anataka tumwabudu pamoja na Wakristo wa kweli. Biblia inasema: “Na acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukutana pamoja, kama wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile ikikaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Tunapaswa kufanya yote tunayoweza ili kuhudhuria mikutano yote. Kwenye mikutano tunapata fursa ya kutiana moyo na kuimarishana.

19. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwapenda ndugu na dada zetu Wakristo?

19 Unapohudhuria mikutano, utapata marafiki wazuri ambao watakusaidia kumwabudu Yehova. Utakutana na ndugu na dada wanaofanya yote wanayoweza ili kumwabudu Yehova kama wewe. Wao pia si wakamilifu na wanakosea. Wanapokosea uwe tayari kuwasamehe. (Soma Wakolosai 3:13.) Sikuzote kazia sifa nzuri za ndugu na dada zako Wakristo, kufanya hivyo kutakusaidia kuwapenda na kumkaribia zaidi Yehova.

UZIMA ULIO WA KWELI

20, 21. “Uzima ulio wa kweli” ni nini?

20 Yehova anataka rafiki zake wawe na maisha bora kabisa. Biblia inatufundisha kwamba wakati ujao maisha yetu yatakuwa tofauti kabisa na maisha ya leo.

Yehova angependa ufurahie “uzima ulio wa kweli.” Je, utafurahia?

21 Wakati ujao, hatutaishi kwa miaka 70 au 80 tu, bali tutaishi milele. Tutafurahia “uzima wa milele” tukiwa na afya njema, amani na furaha katika dunia paradiso. Huo ndio “uzima ulio wa kweli” unaotajwa katika Biblia. Yehova anatuahidi kutupatia uzima ulio wa kweli, hata hivyo ni lazima tufanye yote tunayoweza ili ‘kuushika imara.’—1 Timotheo 6:12, 19.

22. (a) Tunawezaje ‘kushika imara uzima ulio wa kweli’? (b) Kwa nini uzima wa milele ni zawadi?

22 Tunawezaje ‘kushika imara uzima ulio wa kweli’? Lazima ‘tutende mema’ na ‘tuwe matajiri katika matendo mazuri.’ (1 Timotheo 6:18) Hilo linamaanisha kwamba tunahitaji kutumia yale tunayojifunza katika Biblia. Hata hivyo, uzima ulio wa kweli hautegemei jitihada zetu wenyewe. Uzima wa milele ni zawadi ambayo Yehova huwapa watumishi wake waaminifu, ni “fadhili zisizostahiliwa.” (Waroma 5:15) Kwa kweli, Baba yetu wa mbinguni anataka kuwapa watumishi wake waaminifu zawadi hiyo.

23. Kwa nini unapaswa kufanya uamuzi unaofaa sasa?

23 Jiulize, ‘Je, ninamwabudu Mungu kwa njia anayokubali?’ Ukitambua kwamba unahitaji kufanya mabadiliko fulani, chukua hatua bila kukawia. Tunapofanya yote tunayoweza ili kumtii Yehova na kumtegemea yeye, atakuwa kimbilio letu. Atawalinda watu wake waaminifu katika siku za mwisho za ulimwengu mwovu wa Shetani. Kisha, Yehova atahakikisha kwamba tutaishi milele katika paradiso kama tu alivyoahidi. Naam, unaweza kuwa na uzima ulio wa kweli ikiwa utafanya uamuzi unaofaa sasa!