Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 19

Endelea Kuwa Rafiki ya Yehova

Endelea Kuwa Rafiki ya Yehova

1, 2. Leo, ni wapi tunaweza kupata ulinzi?

WAZIA unatembea inje wakati wa upepo mukali. Mawingu yanakuwa mweusi, miangaza na mingurumo ya radi vinaanza kutokea. Kisha mvua inaanza kunyesha. Unatafuta nafasi ya kujificha. Unatulia kabisa wakati unapata mahali fulani kwenye kuwa salama na kwenye hakuna mvua!

2 Leo, tuko mu hali kama ile. Hali zenye kuwa mu dunia zinaendelea kuharibika sana. Unaweza kujiuliza hivi: ‘Ni wapi ninaweza kupata ulinzi?’ Muandikaji mumoja wa zaburi alisema hivi: “Nitamuambia Yehova: ‘Wewe ni kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu mwenye ninategemea.’” (Zaburi 91:2) Kwa kweli, leo Yehova anaweza kutupatia kitulizo wakati tunapata magumu, na anatupatia tumaini la muzuri sana juu ya wakati wenye kuja.

3. Namna gani tunaweza kumufanya Yehova kuwa kimbilio letu?

3 Namna gani Yehova anaweza kutulinda? Anaweza kutusaidia kupiganisha magumu yote yenye tuko nayo, na iko na nguvu kuliko mutu yeyote mwenye anaweza kujaribu kututendea mubaya. Hata kama jambo fulani la mubaya linatupata, tunaweza kuamini kabisa kama Yehova atatengeneza mambo wakati wenye kuja. Biblia inatutia moyo hivi: “Mubakie katika upendo wa Mungu.” (Yuda 21) Tunapaswa kutia nguvu urafiki wetu pamoja na Yehova ili atusaidie wakati wa magumu. Lakini, namna gani tunaweza kufanya vile?

YEHOVA ANAKUPENDA, NA WEWE UMUPENDE

4, 5. Namna gani Yehova ameonyesha kama anatupenda?

4 Ili tuendelee kuwa marafiki wa Yehova, tunapaswa kuelewa kama anatupenda sana. Fikiria mambo yote yenye Yehova ametufanyia. Ametupatia dunia yenye kupendeza na ameijaza mimea na wanyama wenye kupendeza sana. Tena, ametupatia chakula kitamu, na maji safi. Yehova ametumia Biblia ili atufundishe jina lake na sifa zake za muzuri. Na zaidi sana, alituonyesha upendo wake wakati alimutuma Yesu, Mwana wake, mu dunia ili atoe uzima wake kwa ajili yetu. (Yohana 3:16) Na kwa sababu ya zabihu hiyo, tuko na tumaini la muzuri sana juu ya wakati wenye kuja.

5 Yehova ameweka Ufalme wa Kimasiya, ni kusema, serikali ya mbinguni yenye itamaliza mateso yote hivi karibuni. Ufalme huo utafanya dunia kuwa paradiso. Mu paradiso hiyo, kila mutu ataishi milele katika amani na furaha. (Zaburi 37:29) Pia, Yehova anatuonyesha upendo wake kwa kutufundisha namna ya kuishi maisha ya muzuri leo. Tena, anatuomba tusali kwake, na sikuzote iko tayari kusikiliza sala zetu. Yehova ameonyesha kabisa kama anapenda kila mutu kati yetu.

6. Namna gani unaweza kuonyesha kama uko mwenye shukrani juu ya upendo wa Yehova?

6 Namna gani unaweza kuonyesha kama uko mwenye shukrani juu ya upendo wa Yehova? Upendezwe na mambo yote yenye Yehova amekufanyia. Lakini, leo watu wengi hawana shukrani. Watu wengi walikuwa vile wakati Yesu alikuwa mu dunia. Siku moja, Yesu aliponyesha watu kumi wenye walikuwa na ugonjwa wa ukoma, lakini mumoja tu njo alimushukuru. (Luka 17:12-17) Tunapenda kuwa kama mwanaume huyo mwenye alimushukuru Yesu. Sikuzote, tunapenda kuwa wenye shukrani kwa Yehova.

7. Namna gani tunapaswa kumupenda Yehova?

7 Sisi pia tunapaswa kumuonyesha Yehova kama tunamupenda. Yesu aliambia wanafunzi wake kama wanapaswa kumupenda Yehova kwa moyo wao wote, kwa nafsi yao yote, na kwa akili yao yote. (Soma Matayo 22:37.) Maana yake nini?

8, 9. Namna gani tunaweza kumuonyesha Yehova kama tunamupenda?

8 Tunapaswa tu kusema kama tunamupenda Yehova? Hapana. Kama tunamupenda Yehova kwa moyo wetu wote, kwa nafsi yetu yote, na kwa akili yetu yote, tutaonyesha vile kupitia matendo yetu. (Matayo 7:16-20) Biblia inafundisha waziwazi kama ikiwa tunamupenda Mungu, tutafuata amri zake. Ni nguvu kufanya vile? Hapana, kwa sababu “amri zake haziko muzigo muzito.”​—Soma 1 Yohana 5:3.

9 Wakati tunamutii Yehova, tutakuwa na maisha ya muzuri na yenye furaha. (Isaya 48:17, 18) Lakini, ni nini itatusaidia tuendelee kuwa marafiki wa Yehova? Tuone basi.

KOMALISHA URAFIKI WAKO PAMOJA NA YEHOVA

10. Juu ya nini tunapaswa kuendelea kujifunza juu ya Yehova?

10 Ni nini ilikusaidia ukuwe rafiki ya Yehova? Kujifunza Biblia kumekusaidia ufikie kumujua Yehova muzuri zaidi na kukomalisha urafiki pamoja naye. Urafiki huo ni kama moto wenye unapenda uendelee kuwaka. Moto uko na lazima ya kuni ili uendelee kuwaka, vilevile unapaswa kuendelea kujifunza juu ya Yehova ili urafiki wako pamoja naye uendelee kuwa wenye nguvu.​—Mezali 2:1-5.

Kama moto, upendo wako kwa Yehova uko na lazima ya kuni ili uendelee kuwaka

11. Kujifunza Biblia kutakuletea faida gani?

11 Wakati unaendelea kujifunza Biblia, utajua mambo yenye yatagusa kabisa moyo wako. Ona namna wanafunzi wawili wa Yesu walijisikia wakati Yesu alikuwa anawafasiria unabii wa Biblia. Walisema hivi: “Je, mioyo yetu haikukuwa inawaka wakati alikuwa anazungumuza na sisi katika barabara, na wakati alikuwa anatufasiria Maandiko waziwazi?”​—Luka 24:32.

12, 13. (a) Ni nini inaweza kufikia upendo wetu kwa Mungu? (b) Tunaweza kufanya nini ili upendo wetu kwa Yehova uendelee kuwa wenye nguvu?

12 Wakati wanafunzi wa Yesu walielewa Maandiko, waliguswa moyo. Pengine na wewe ulikuwa na furaha hiyo wakati ulianza kujifunza Biblia. Hilo lilikusaidia kumujua Yehova na kumupenda. Usiache upendo huo upoe ao upunguke.​—Matayo 24:12.

13 Wakati unakuwa rafiki ya Mungu, unapaswa kujikaza sana ili uendelee kutia nguvu urafiki wako pamoja naye. Unapaswa kuendelea kujifunza juu yake na juu ya Yesu. Ufikirie pia mambo yenye unajifunza na namna unaweza kuyatumia mu maisha yako. (Yohana 17:3) Wakati unasoma ao kujifunza Biblia, ujiulize hivi: ‘Habari hii inanifundisha nini juu ya Yehova Mungu? Juu ya nini ninapaswa kumupenda kwa moyo wangu wote na kwa nafsi yangu yote?’​—1 Timoteo 4:15.

14. Namna gani sala inatusaidia kutia nguvu upendo wetu kwa Yehova?

14 Wakati unapata rafiki muzuri, unazungumuza naye kila mara, na hilo linafanya urafiki wenu ukuwe wenye nguvu. Vilevile, wakati tunazungumuza na Yehova kila mara mu sala, hilo linafanya upendo wetu kwake ukuwe wenye nguvu. (Soma 1 Watesalonike 5:17.) Sala ni zawadi ya muzuri kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. Sikuzote, tunapaswa kumuambia mambo yenye kuwa mu moyo wetu. (Zaburi 62:8) Hatupaswe kurudilia-rudilia sala zenye tumeweka mu akili, lakini tunapaswa kusema mambo yenye kutoka kabisa mu moyo wetu. Kwa kweli, kama tunaendelea kujifunza Biblia na kusali kwa moyo wetu, tutaendelea kutia nguvu upendo wetu kwa Yehova.

KUZUNGUMUZA NA WENGINE JUU YA YEHOVA

15, 16. Namna gani unaona kazi ya kuhubiri?

15 Kama tunapenda kuendelea kuwa marafiki wa Yehova, tunapaswa pia kuzungumuza na wengine juu ya imani yetu. Kuambia wengine juu ya Yehova ni heshima kubwa sana. (Luka 1:74) Na ni daraka lenye Yesu alipatia Wakristo wote wa kweli. Kila mumoja wetu anapaswa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Umeanza kufanya vile?​—Matayo 24:14; 28:19, 20.

16 Mutume Paulo aliona kama kazi ya kuhubiri ni ya maana sana; aliita kazi hiyo “hazina.” (2 Wakorinto 4:7) Kuambia wengine juu ya Yehova na kusudi lake ni kazi ya maana zaidi yenye tunapaswa kufanya. Kufanya vile ni njia ingine ya kumutumikia Yehova, na anapendezwa na mambo yenye unamufanyia. (Waebrania 6:10) Tena, kuhubiri kunaweza kukuletea faida wewe na watu wenye kukusikiliza. Kuhubiri kunakusaidia wewe na watu wengine mukuwe marafiki wa Yehova na mupate uzima wa milele. (Soma 1 Wakorinto 15:58.) Kwa kweli, hakuna kazi ingine yenye inaweza kukuletea furaha zaidi.

17. Juu ya nini kazi ya kuhubiri inapaswa kufanywa haraka?

17 Kazi ya kuhubiri inapaswa kufanywa haraka sana. Tunapaswa ‘kuhubiri neno,’ na tunapaswa ‘kufanya vile kwa bidii.’ (2 Timoteo 4:2) Watu wako na lazima ya kusikia juu ya Ufalme wa Mungu. Biblia inasema hivi: “Ile siku kubwa ya Yehova iko karibu! Iko karibu na inakuja haraka sana!” Mwisho ‘hautachelewa!’ (Sefania 1:14; Habakuki 2:3) Karibuni, Yehova ataharibu ulimwengu mubaya wa Shetani. Mbele jambo hilo lifanyike, tunapaswa kuonya ao kusaidia watu ili wachague kumutumikia Yehova.

18. Juu ya nini tunapaswa kumuabudu Yehova pamoja na Wakristo wengine wa kweli?

18 Yehova anapenda tumuabudu pamoja na Wakristo wengine wa kweli. Biblia inasema hivi: “Tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo ya muzuri, bila kuacha kukutana pamoja, kama vile wengine wako na desturi, lakini tutiane moyo, na kufanya vile zaidi sana kwa kadiri munaona siku ile kuwa inakaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Tunapaswa kujikaza sana kufika ku mikutano yote. Mikutano inatusaidia kutiana moyo na kutiana nguvu.

19. Ni nini inaweza kutusaidia tupende ndugu na dada zetu?

19 Wakati unakuja ku mikutano, utapata marafiki wazuri wenye watakusaidia kumuabudu Yehova. Utakutana na ndugu na dada mbalimbali wenye wanajikaza kumuabudu Yehova kama wewe. Kama wewe, nao hawakamilike na wanafanyaka makosa. Wakati wanafanya makosa, ukuwe tayari kuwasamehe. (Soma Wakolosai 3:13.) Sikuzote, ukaze akili juu ya sifa za muzuri za ndugu na dada zako. Kufanya vile kutakusaidia uwapende zaidi na ukomalishe zaidi urafiki wako pamoja na Yehova.

UZIMA WA KWELIKWELI

20, 21. “Uzima wa kwelikweli” ni nini?

20 Yehova anapenda marafiki wake wakuwe na maisha ya muzuri. Biblia inatufundisha kama maisha ya wakati wenye kuja itakuwa tofauti kabisa na maisha ya leo.

Yehova anapenda upate “uzima wa kwelikweli.” Utapata uzima huo?

21 Wakati wenye kuja, tutaishi milele, haiko miaka 70 ao 80 tu. Tutakuwa na “uzima wa milele,” afya kamilifu, amani, na furaha mu paradiso yenye kupendeza sana. Maisha hayo njo Biblia inaita “uzima wa kwelikweli.” Yehova anaahidi kama atatupatia uzima huo wa kwelikweli, lakini tunapaswa kujikaza ili ‘tushike sana’ uzima huo.​—1 Timoteo 6:12, 19.

22. (a) Tunapaswa kufanya nini ili ‘tushike sana uzima wa kwelikweli’? (b) Juu ya nini hatustahili kupata uzima wa milele?

22 Tunapaswa kufanya nini ili ‘tushike sana uzima wa kwelikweli’? Tunapaswa ‘kutenda mema’ na ‘kuwa matajiri katika matendo ya muzuri.’ (1 Timoteo 6:18) Ni kusema, tunapaswa kutumikisha mambo yenye tunajifunza mu Biblia. Lakini, hatutapata uzima huo wa kwelikweli kwa nguvu zetu wenyewe. Hatustahili hata kidogo kupata uzima wa milele. Ni zawadi ya bure yenye Yehova anapatia watumishi wake waaminifu, ni “fazili zenye hazistahiliwe.” (Waroma 5:15) Baba yetu wa mbinguni anapenda kabisa kupatia watumishi wake waaminifu zawadi hiyo.

23. Juu ya nini unapaswa kukamata maamuzi ya muzuri leo?

23 Ujiulize hivi: ‘Ninamuabudu Mungu mu njia yenye anaitika?’ Kama unaona kuwa unapaswa kufanya mabadiliko fulani, fanya mabadiliko hayo bila kukawia. Wakati tunamutumainia Yehova na tunajikaza sana kumutii, Yehova atakuwa kimbilio letu. Atalinda watu wake katika siku hizi za mwisho za ulimwengu mubaya wa Shetani. Kisha Yehova atahakikisha kama tunaishi mu Paradiso milele, kama vile tu ameahidi. Kwa kweli, unaweza kuwa na uzima wa kwelikweli, kama unakamata maamuzi ya muzuri leo!