Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SWALI LA 4

Ninaweza Kurekebishaje Makosa Yangu?

Ninaweza Kurekebishaje Makosa Yangu?

KWA NINI NI MUHIMU

Kukubali makosa yako kutakufanya uwe mwenye kutegemeka na kuaminika zaidi.

WEWE UNGEFANYA NINI?

Fikiria hali hii: Tim anacheza na rafiki zake. Anatupa mpira na kuvunja kioo cha gari la jirani yao.

Ikiwa ungekuwa Tim, ungefanya nini?

TUA NA UFIKIRI!

CHAGUA MOJA KATI YA MAMBO HAYA MATATU:

  1. Kimbia.

  2. Laumu mtu mwingine.

  3. Mwambie jirani kilichotendeka, na umwombe ulipie kioo hicho.

Huenda ukashawishika kuchagua kufanya Jambo la 1. Lakini kuna sababu zinazofaa za kufunua makosa uliyofanya —iwe ni kosa la kuvunja kioo au kosa lingine lolote.

SABABU TATU ZA KUKUBALI MAKOSA YAKO

  1. Ndilo jambo linalofaa.

    Biblia inasema hivi: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.

  2. Watu wana mwelekeo wa kuwasamehe wale wanaokubali makosa yao.

    Biblia inasema hivi: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.”—Methali 28:13.

  3. Jambo muhimu hata zaidi, utamfurahisha Mungu.

    Biblia inasema hivi: “Mtu mwenye hila ni chukizo kwa Yehova, lakini urafiki Wake uko pamoja na watu wanyoofu.”—Methali 3:32.

Karina, mwenye umri wa miaka 20, alipewa tiketi na polisi ya kumtoza faini kwa sababu ya kuendesha gari kasi sana, naye akajaribu kumficha baba yake jambo hilo. Lakini hangeweza kuficha milele. Karina anasema hivi: “Mwaka mmoja hivi baadaye, baba alijua kuhusu tiketi hiyo. Nilijipata matatani!”

Alijifunza jambo gani? Karina anasema: “Kuficha makosa kunafanya hali iwe mbaya hata zaidi. Bado utalipia makosa hayo baadaye!”

JIFUNZE KUTOKANA NA MAKOSA YAKO

Biblia inasema hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yakobo 3:2) Kama tulivyoona ni ishara ya ukomavu na unyenyekevu kukubali makosa yetu mara tu tukoseapo.

Mbali na hilo unapaswa pia kujifunza kutokana na makosa yako. Msichana anayeitwa Vera anasema: “Mimi hujitahidi kujifunza jambo fulani kutokana na kila kosa ninalofanya ili linisaidie kuboresha utu wangu na nijue jinsi ya kushughulikia hali hiyo kwa njia tofauti wakati ujao.” Hebu tuone jinsi unavyoweza kufanya hivyo.

Unachukua baiskeli ya baba yako halafu unaiharibu. Utafanya nini?

  • Utanyamaza na kutumaini kwamba baba yako hatatambua.

  • Utamwambia baba yako kilichotokea.

  • Utamwambia baba yako kilichotokea lakini ulaumu mtu mwingine.

Unaanguka mtihani kwa sababu hukujitayarisha vizuri. Utafanya nini?

  • Utalaumu mtihani.

  • Utakubali ulistahili kuanguka.

  • Utadai kwamba mwalimu anakuonea.

Unapokazia fikiria makosa uliyofanya zamani ni kama unakazia macho kioo cha kuangalia nyuma huku ukiendesha gari

Fikiria tena visa hivyo viwili na ujaribu kuwazia ungekuwa (1) baba yako na (2) mwalimu wako. Unafikiri baba yako na mwalimu wako wangekuonaje ikiwa ungekubali makosa yako bila tatizo? Wangekuwa na maoni gani kukuhusu ikiwa ungeficha makosa yako?

Sasa fikiria kuhusu kosa ulilofanya ndani ya mwaka mmoja uliopita kisha ujibu maswali yafuatayo.

Ulifanya kosa gani? Ulishughulikiaje kosa hilo?

  • Nilijaribu kuficha.

  • Nilimlaumu mtu mwingine.

  • Nilikubali mara moja.

Ikiwa hukukubali kosa lako, ulihisije baadaye?

  • Safi. Nimeponyoka!

  • Mwenye hatia. Nilipaswa kusema kweli.

Ungeshughulikiaje hali hiyo kwa njia nzuri zaidi?

Ulijifunza nini kutokana na kosa lako?

UNA MAONI GANI?

Kwa nini watu fulani hawakubali makosa yao?

Watu watakuonaje ikiwa sikuzote wewe huficha makosa yako, lakini watakuonaje ikiwa unakubali makosa yako?—Luka 16:10.