Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SWALI LA 5

Nifanye Nini Ninapoonewa Shuleni?

Nifanye Nini Ninapoonewa Shuleni?

KWA NINI NI MUHIMU

Jinsi unavyotenda huenda kukapunguza au kuongeza uonevu huo.

WEWE UNGEFANYA NINI?

Fikiria hali hii: Thomas hataki tena kwenda shuleni. Si leo, si kesho. Hataki kamwe kurudi shuleni. Tatizo lilianza miezi mitatu iliyopita wanafunzi wenzake walipoeneza porojo mbaya sana kumhusu. Kisha akaanza kupewa majina ya utani. Nyakati nyingine, vijana wenzake huangusha vitabu alivyobeba na kujifanya kana kwamba jambo hilo limetukia bila kukusudia, au kijana mmoja nyuma yake anamsukuma, na kufikia wakati ambapo Thomas anageuka hawezi kutambua ni nani aliyefanya hivyo. Jana, uonevu huo uligeuka ukawa mbaya hata zaidi wakati ambapo Thomas alitishwa kupitia mtandao . . .

Ikiwa ungekuwa Thomas, ungetendaje?

TUA NA UFIKIRI!

Usifikiri kwamba huna uwezo wowote! Kwa kweli, unaweza kukabiliana na mnyanyasaji bila kutumia ngumi. Jinsi gani?

  • USIONYESHE UMECHOKOZEKA. Biblia inasema hivi: “Mtu mjinga huiachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima huituliza mpaka mwisho.” (Methali 29:11) Ukitulia, bila kuonyesha umechokozeka, wanaokuonea watachoka.

  • USILIPIZE KISASI. Biblia inasema hivi: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu.” (Waroma 12:17) Kulipiza kisasi kutazidisha tu tatizo, hakutalitatua.

  • JIHADHARI. Biblia inasema hivi: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Kwa kadiri unayoweza, waepuke watu wanaoweza kukuonea au maeneo ambayo unaweza kuonewa.

  • TOA JIBU LISILOTAZAMIWA. Biblia inasema hivi: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu.” (Methali 15:1) Unaweza hata kutumia ucheshi. Kwa mfano, mwoneaji anaposema kwamba umenenepa kupita kiasi, lipuuze jambo hilo na useme: “Inaonekana ninapaswa kupunguza kilo kadhaa!”

  • ONDOKA. “Kunyamaza kunaonyesha kwamba wewe ni mkomavu na una nguvu kuliko yule mtu anayekusumbua,” anasema Nora mwenye umri wa miaka 19. “Kufanya hivyo kunaonyesha kwamba una uwezo wa kujizuia, lakini yule anayekuonea hana uwezo huo.”—2 Timotheo 2:24.

  • JITAHIDI KUJIAMINI. Mara nyingi, watu wanaowaonea wengine hutambua iwapo mtu hajiamini au hatajitetea. Lakini waoneaji wengi watakuacha wakitambua kwamba huwaruhusu wakuhangaishe.

  • MWELEZE MTU. Mtu mmoja aliyekuwa mwalimu zamani anasema: “Ningemsihi mtu yeyote anayeonewa aseme. Hilo ndilo jambo linalofaa, na huenda likazuia mtu mwingine asionewe.”

Kujiamini kutakupa nguvu ambazo anayekuonea hana