Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SWALI LA 6

Nifanye Nini Ninaposhinikizwa na Vijana Wenzangu?

Nifanye Nini Ninaposhinikizwa na Vijana Wenzangu?

KWA NINI NI MUHIMU

Unapokuwa na msimamo, utaweza kuyaongoza maisha yako, badala ya kuruhusu wengine wakuamulie cha kufanya.

WEWE UNGEFANYA NINI?

Fikiria hali hii: Brian anaingiwa na hofu anapowaona wanafunzi wenzake wawili wakimkaribia. Tayari mara mbili juma hili wamejaribu kumshawishi avute sigara. Hili ni jaribio lao la tatu.

Mvulana wa kwanza anasema hivi:

“Naona wewe ni mpweke? Acha nikutambulishe kwa rafiki.”

Anasema neno “rafiki” huku akimkonyeza jicho Brian na kumtolea kitu mfukoni.

Brian anaona sigara ambayo mvulana huyo ameshika. Sasa anaingiwa na hofu hata zaidi.

Brian anajibu, “Samahani, nimeshakwambia kwamba mimi si . . . ”

Mvulana wa pili anamkatiza: “Acha kuwa mwoga!”

“Mimi si mwoga!” Brian anajitahidi kusema kwa ujasiri.

Mvulana wa pili anaweka mkono wake kwenye mabega ya Brian na kusema kwa sauti ya chini. “Ichukue tu.”

Mvulana wa kwanza anaisogeza sigara hiyo karibu na uso wa Brian na kusema hivi akinong’oneza: “Hatutamwambia yeyote. Hakuna atakayejua.”

Wewe ungekuwa Brian ungefanyaje?

TUA NA UFIKIRI!

Je, kweli vijana hao wawili wametafakari kuhusu wanachofanya? Je, mwenendo wao unategemea mambo ambayo wao wenyewe wamejiamulia? Hapana. Kuna uwezekano mkubwa kwamba wameathiriwa na maoni ya wengine. Wanataka kukubaliwa na wengine, hivyo wamewaruhusu wawaamulie la kufanya.

Ikiwa ungekabili hali kama hiyo, ungetendaje kwa njia tofauti na hivyo kukabiliana na shinikizo kutoka kwa vijana wenzako?

  1. FIKIRIA MAPEMA HALI ZINAZOWEZA KUTOKEA

    Biblia inasema hivi: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.”—Methali 22:3.

    Mara nyingi unaweza kuona hatari mapema. Kwa mfano, unatupa jicho na kuwaona wanafunzi wenzako wakija huku wakivuta sigara. Ukifikiria mapema tatizo linaloweza kutokea, utakuwa tayari kukabiliana nalo.

  2. TAFAKARI

    Biblia inasema hivi: “Iweni na dhamiri njema.”—1 Petro 3:16.

    Jiulize, ‘Nikijiunga nao, nitahisi namna gani baadaye?’ Ni kweli kwamba huenda mwanzoni ukakubaliwa na vijana wenzako. Lakini utahisi namna gani baadaye? Uko tayari kubadili msimamo wako ili tu uwafurahishe wanafunzi wenzako? —Kutoka 23:2.

  3. FANYA UAMUZI

    Biblia inasema hivi: “Mwenye hekima huogopa [au huwa mwenye tahadhari].”—Methali 14:16.

    Maishani mwetu lazima tufanye maamuzi na kukubali matokeo yake. Biblia inaeleza kuhusu wanaume waliofanya maamuzi mazuri kama vile Yosefu, Ayubu, na Yesu. Pia, inaeleza kuhusu watu waliofanya maamuzi mabaya kama vile Kaini, Esau, na Yuda. Wewe utafanya uamuzi gani?

Biblia inasema hivi: ‘Tenda kwa uaminifu.’ (Zaburi 37:3) Ikiwa tayari umefikiria kuhusu matokeo na kufanya uamuzi, itakuwa rahisi zaidi kueleza msimamo wako kuliko unavyofikiri na utapata matokeo mazuri.

Usiwe na wasiwasi—huhitaji kuwatolea vijana wenzako hotuba. Huenda ikatosha tu kuwaambia kwa uthabiti, HAPANA. Au ili kujulisha waziwazi msimamo wako usiobadilika, unaweza kusema:

  • “Mimi msinihusishe!”

  • “Sifanyi mambo kama hayo!”

  • “Nilifikiri mnajua mimi si mtu wa aina hiyo!”

Jambo kuu ni kujibu kwa usadikisho na bila kusita. Ukifanya hivyo, huenda ukashangaa kuona vijana wenzako wakiacha usumbufu wao mara moja!

JINSI YA KUKABILI DHIHAKA

Unapokubali kushinikizwa na vijana wenzako, unakuwa kama roboti wanayoiongoza watakavyo

Namna gani vijana wenzako wakikudhihaki? Utafanya nini wakisema, “Una shida gani—unaogopa?” Tambua kwamba aina hii ya dhihaka imekusudiwa tu kukushinikiza ufanye kama wanavyotaka. Unaweza kufanya nini? Kuna angalau mambo mawili unayoweza kufanya.

  • Unaweza kukubali dhihaka hizo. (“Ni kweli, ninaogopa!” Kisha waeleze kifupi kwa nini unaogopa.)

  • Unaweza kuwashinikiza wao pia kwa kuwaeleza sababu yako ya kukataa kisha uwaambie jambo ambalo litawafanya waone upumbavu wa mambo wanayofanya. (“Mtu mwerevu hawezi kuvuta sigara!”)

Vijana wenzako wakiendelea kukudhihaki, ondoka! Unavyozidi kukaa hapo, ndivyo utakavyoshinikizwa zaidi. Unapoondoka unaonyesha kwamba huruhusu wengine wabadili msimamo wako.

Ukweli ni kwamba huwezi kuwazuia kabisa vijana wenzako kukushinikiza. Lakini unaweza kuamua utafanya nini, uwajulishe msimamo wako, na utende kulingana na uamuzi wako. Kwa kweli, wewe ndiye mwenye mamlaka ya kuamua!—Yoshua 24:15.