Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SWALI LA 8

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kushambuliwa Kingono?

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kushambuliwa Kingono?

KWA NINI NI MUHIMU

Kila mwaka, mamilioni ya watu hubakwa au kutendewa vibaya kingono, na hasa vijana ndio wanaolengwa.

WEWE UNGEFANYA NINI?

Annette alikamatwa na mshambuliaji wake. Hata kabla ya kujua kilichokuwa kikiendelea alijikuta chini. Anasema, “Nilijaribu kufanya kila kitu nilichoweza kumzuia. Nilijaribu kupiga mayowe, lakini wapi. Nilimsukuma, nikatupa mateke, nikampiga ngumi, na kumkwaruza. Ndipo nikasikia kisu kikinidunga. Mwili wangu wote ukapooza kabisa.”

Ikiwa ungejikuta katika hali kama hiyo, ungetendaje?

TUA NA UFIKIRI!

Ingawa huenda ukawa makini—hasa unapotembea usiku—bado mambo mabaya yanaweza kutokea. “Si wenye mbio wanaoshinda katika mbio,” inasema Biblia, “wala wenye ujuzi wanaopata kibali; kwa sababu wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.”—Mhubiri 9:11.

Vijana fulani, kama Annette, wanatendewa vibaya na watu wasiowajua. Wengine wanashambuliwa na mtu wanayemfahamu au hata mtu wa familia. Natalie alipokuwa na umri wa miaka kumi tu, alitendewa vibaya kingono na kijana aliyekuwa akiishi karibu na kwao. “Niliogopa na kuaibika sana hivi kwamba mwanzoni sikumwambia yeyote,” anasema Natalie.

USIJILAUMU

Mpaka sasa Annette anapambana na hisia za hatia kuhusu mambo yaliyompata. Anasema hivi: “Mimi hufikiria matukio ya usiku huo tena na tena. Nahisi kwamba nilipaswa kujaribu zaidi kumzuia mtu huyo. Ukweli ni kwamba nilishikwa na hofu kubwa baada ya kudungwa kisu. Sikuweza kufanya lolote, lakini nahisi nilipaswa kufanya jambo fulani.”

Natalie pia anapambana na hisia za hatia. Anasema: “Sikupaswa kumwamini sana kijana huyo. Wazazi wetu walituwekea sheria mimi na dada yangu kwamba tunapokuwa nje tucheze pamoja, lakini sikutii. Kwa hiyo, nahisi nilimpa kijana huyo jirani yetu nafasi ya kuniumiza. Jambo lililonipata liliathiri familia yetu, nami ninajilaumu kwa kuwasababishia maumivu hayo yote. Hilo ndilo linaloniumiza zaidi.”

Ikiwa unapambana na hisia kama za Annette au za Natalie, kumbuka kwamba ikiwa ulibakwa, haikuwa kwa kupenda kwako. Watu fulani hujaribu kupunguza uzito wa kosa hilo kwa kusema kwamba ni kawaida kwa wavulana kutenda hivyo au kwamba wanaobakwa walijitakia. Hata hivyo, hakuna mtu anayestahili kubakwa. Ikiwa ulitendewa uovu huo mbaya, usijilaumu!

Ni kweli kwamba ni rahisi kusoma maneno hayo “usijilaumu” lakini huenda ikawa vigumu kuyaamini. Wengine hawazungumzi kuhusu yaliyotokea na hivyo wanaumizwa na hisia za hatia na hisia nyingine zisizofaa. Hata hivyo, kukaa kimya kunamsaidia nani—wewe au aliyekushambulia? Utafaidika ukisema yaliyokupata.

SEMA YALIYOKUPATA

Biblia inasema kwamba baada ya kukabili hali ngumu kwa muda mrefu, yule mwanamume mwadilifu Ayubu alisema hivi: “Nitaonyesha hangaiko langu kujihusu mwenyewe.” (Ayubu 10:1) Unaweza kufaidika kwa kufanya hivyo pia. Kuzungumza na mtu unayemwamini kuhusu mambo yaliyokupata kunaweza kukusaidia kupambana na hali hiyo na kupata kitulizo kutokana na hisia zako zenye kuumiza.

Huenda hisia zako zikawa nzito sana na zenye kulemea. Kwa nini usitafute msaada kwa kuzungumza na mtu fulani?

Annette aligundua ukweli wa jambo hilo. Anasema: “Nilizungumza na rafiki yangu wa karibu, naye akanihimiza nizungumze na wazee wawili Wakristo katika kutaniko letu. Ninafurahi kwamba nilifanya hivyo. Walizungumza nami mara kadhaa na kuniambia kwamba sipaswi kujilaumu kwa jambo lililonipata. Nilihitaji sana kusikia mambo hayo. Walinihakikishia sikufanya kosa lolote.”

Natalie alizungumza na wazazi wake kuhusu jinsi alivyotendewa vibaya. Anasema: “Walinisaidia. Walinitia moyo niwaeleze waziwazi mambo yaliyonipata, na kufanya hivyo kulinisaidia kutohuzunika sana na kuwa na hasira nyingi.”

Pia, Natalie alifarijika alipotoa sala. Anasema: “Kuzungumza na Mungu kulinisaidia hasa nyakati ambazo niliona kuwa siwezi kuzungumza na mwanadamu. Ninaposali ninaweza kuzungumza kwa uhuru. Kufanya hivyo kunanipa amani ya kweli na utulivu.”

Wewe pia unaweza kutambua kwamba kuna ‘wakati wa kupona.’ (Mhubiri 3:3) Jitunze kimwili na kihisia. Pumzika vya kutosha. Na zaidi ya yote, mtegemee Mungu wa faraja yote, Yehova.—2 Wakorintho 1:3, 4.

IKIWA UNA UMRI WA KUTOSHA KUWA NA URAFIKI NA MTU WA JINSIA TOFAUTI

Ikiwa wewe ni msichana na unashinikizwa kujihusisha katika mwenendo mchafu, hakuna ubaya kusema hivi kwa uthabiti, “Usifanye hivyo!” au, “Usiniguse!” Usinyamaze eti kwa sababu unaogopa atakuacha. Akivunja uhusiano wenu kwa sababu hiyo, basi hakufai! Unahitaji mwanamume anayeheshimu mwili wako na viwango vyako.

MASWALI KUHUSU KUSUMBULIWA KINGONO

“Nilipokuwa shule ya msingi, wavulana wangevuta kanda za sidiria yangu na kusema mambo yenye kunishushia heshima—kama vile eti jinsi ambavyo ningefurahia sana kufanya ngono pamoja nao.”—Coretta.

Unafikiri wavulana hao walikuwa:

  1. Wakimtania?

  2. Wakimchezea kimapenzi?

  3. Wakimsumbua kingono?

“Nikiwa ndani ya basi, mvulana mmoja alianza kuniambia maneno machafu na kunishika. Niliupiga mkono wake na kumwambia aondoke. Alinitazama kana kwamba nina kichaa.”—Candice.

Unafikiri mvulana huyo alikuwa akimfanyia nini Candice?

  1. Akimtania?

  2. Akimchezea kimapenzi?

  3. Akimsumbua kingono?

“Mwaka uliopita, mvulana fulani alikuwa akiniambia kila mara kwamba ananipenda na angependa niwe rafiki yake, hata ingawa kila wakati nilikataa. Nyakati nyingine, angenipapasa mkono. Nilimwambia akome, lakini hakunisikiliza. Kisha nilipokuwa nikifunga kamba za viatu, alinishika kwenye makalio.”—Bethany.

Kwa maoni yako, je, mvulana huyo alikuwa:

  1. Akimtania?

  2. Akimchezea kimapenzi?

  3. Akimsumbua kingono?

Jibu sahihi kwa visa vyote vitatu ni C.

Kuna tofauti gani kati ya kumsumbua mtu kingono na kumchezea kimapenzi au kumtania?

Mtu anayesumbuliwa kingono hafurahii jambo hilo anayefurahia ni msumbuaji. Usumbuaji huo huendelea hata baada ya msumbuaji kuambiwa aache.

Kusumbuliwa kingono ni jambo zito. Kunaweza kufanya utendewe vibaya kingono.