Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 1

Mungu Aliumba Mbingu na Dunia

Mungu Aliumba Mbingu na Dunia

Yehova Mungu ndiye Muumba wetu. Yeye aliumba vitu vyote, vinavyoonekana na visivyoonekana. Kabla ya kuumba vitu tunavyoona, aliumba malaika wengi sana. Malaika ni nani? Malaika ni viumbe ambao waliumbwa na Yehova, walio kama yeye. Hatuwezi kuwaona kama vile ambavyo hatuwezi kumwona Mungu. Yehova alimuumba malaika wa kwanza na huyo akawa msaidizi wake. Malaika huyo alimsaidia Yehova kuumba nyota, sayari, na vitu vingine vyote. Dunia yetu maridadi ni moja kati ya sayari hizo.

Kisha, Yehova aliitayarisha dunia ili wanadamu na wanyama waishi. Alifanya mwanga wa jua uangaze duniani. Aliumba milima, bahari na mito.

Alifanya nini baadaye? Yehova akasema: ‘Nitaotesha nyasi, mimea na miti.’ Miti ya matunda ya aina mbalimbali, mboga na maua yakaanza kumea. Kisha, Yehova akaumba wanyama, wanaoruka, wanaotambaa na wanaoogelea. Aliwaumba wanyama wadogo kama vile sungura, na wanyama wakubwa, kama vile tembo. Ni mnyama gani unayempenda?

Kisha, Yehova akamwambia yule malaika wa kwanza: “Na tufanye mtu.” Wanadamu wangekuwa tofauti na wanyama. Wangeweza kubuni vitu, kuzungumza, kucheka, na kusali. Wangetunza dunia na wanyama. Je, unajua mwanadamu wa kwanza aliitwa nani? Acha tuone.

“Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”​—Mwanzo 1:1