Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 2

Mungu Alimuumba Mwanamume na Mwanamke wa Kwanza

Mungu Alimuumba Mwanamume na Mwanamke wa Kwanza

Yehova alipanda bustani katika eneo lililoitwa Edeni. Bustani hiyo ilikuwa na maua, miti, na wanyama wengi. Kisha, Mungu akatumia mavumbi kumuumba mwanamume wa kwanza Adamu na kumpulizia pumzi puani mwake. Ni nini kilitokea? Mtu huyo akawa hai! Yehova alimpa Adamu kazi ya kuitunza bustani, na kuwapa wanyama wote majina.

Yehova alimpa Adamu agizo muhimu. Alimwambia hivi: ‘Unaweza kula matunda ya miti yote isipokuwa matunda ya mti mmoja. Ukila matunda ya mti huo utakufa.’

Baadaye, Yehova akasema: ‘Nitamfanyia Adamu msaidizi.’ Mungu akamfanya Adamu alale usingizi mzito, halafu akachukua ubavu mmoja na kumuumba mwanamke. Mwanamke huyo aliitwa Hawa. Adamu na Hawa wakawa familia ya kwanza. Adamu alihisije alipopata mke? Alifurahi sana na kusema: ‘Yehova ameumba mwanamke kutokana na ubavu wangu! Hatimaye! Huyu ni mwenzangu.’

Yehova akawaambia Adamu na Hawa wazae watoto na kuijaza dunia. Alitaka wafurahie kufanya kazi pamoja na kuifanya dunia yote kuwa paradiso, au bustani nzuri, kama bustani ya Edeni. Lakini hawakufanikiwa kuifanya dunia kuwa paradiso. Unajua ni kwa nini? Tutajifunza zaidi katika sura inayofuata.

“Yule aliyewaumba tangu mwanzo aliwaumba mwanamume na mwanamke.”​—Mathayo 19:4