Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 3

Adamu na Hawa Hawakumtii Mungu

Adamu na Hawa Hawakumtii Mungu

Siku moja Hawa alipokuwa peke yake, nyoka alizungumza naye. Alimwuliza hivi: ‘Je, ni kweli kwamba Mungu amewakataza kula matunda ya miti yote?’ Hawa akajibu hivi: ‘Tunaweza kula matunda ya miti, isipokuwa mti mmoja. Tukila matunda ya mti huo, tutakufa.’ Nyoka akamwambia: ‘Hamtakufa. Kwa kweli, mkila matunda ya mti huo, mtakuwa kama Mungu.’ Je, nyoka alisema kweli? Hapana, huo ulikuwa uwongo. Lakini Hawa aliamini maneno hayo. Kadiri Hawa alivyoendelea kuyatazama matunda ya mti huo, ndivyo alivyozidi kutamani kuchuma na kula. Alikula matunda hayo na kisha akampatia Adamu. Adamu alijua kwamba wangekufa ikiwa wangemwasi Mungu. Hata hivyo, Adamu aliamua kula tunda hilo.

Baadaye, Yehova alizungumza na Adamu na Hawa. Aliwauliza kwa nini wamemwasi. Hawa alimlaumu nyoka, na Adamu akamlaumu Hawa. Kwa kuwa Adamu na Hawa hawakumtii Yehova, aliwafukuza katika bustani. Ili kuwazuia wasirudi katika bustani, Mungu aliwaweka malaika na upanga uliowaka moto ili kulinda mwingilio wa bustani.

Yehova aliahidi kumwadhibu kiumbe aliyemdanganya Hawa. Si nyoka halisi aliyezungumza na Hawa. Yehova hakuwaumba nyoka wakiwa na uwezo wa kuzungumza. Malaika mbaya alimfanya nyoka azungumze. Alifanya hivyo ili kumdanganya Hawa. Malaika huyo anaitwa Shetani Ibilisi. Wakati ujao, Yehova atamharibu Shetani ili asiendelee kuwashawishi watu wafanye mambo mabaya.

“Ibilisi . . . alikuwa muuaji alipoanza, naye hakusimama imara katika kweli, kwa sababu kweli haimo ndani yake.”​—Yohana 8:44