Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 8

Abrahamu na Sara Walimtii Mungu

Abrahamu na Sara Walimtii Mungu

Jiji la Uru lilikuwa jirani na mji wa Babeli, ambako watu waliabudu miungu mingine tofauti na Yehova. Lakini kulikuwa na mwanamume mmoja aliyeishi katika jiji la Uru, ambaye alimwabudu Yehova pekee. Mwanamume huyo aliitwa Abrahamu.

Yehova alimwambia Abrahamu hivi: ‘Nenda utoke katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako, mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha.’ Kisha Mungu akamwahidi hivi: ‘Nami nitakufanya uwe taifa kubwa, nitawafanyia watu mambo mazuri katika dunia yote kwa sababu yako.’

Ingawa Abrahamu hakujua mahali alikokuwa akienda, alimtumaini Yehova. Kwa hiyo Abrahamu na Sara mke wake, Tera baba yao, na Loti mpwa wao walitii, wakachukua mizigo na kuanza safari ndefu.

Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 75, wakati yeye na familia yake walipofika katika nchi ambayo Yehova alitaka kuwaonyesha. Nchi hiyo iliitwa Kanaani. Mungu alizungumza na Abrahamu na kumwahidi hivi: ‘Nitaupa uzao wako nchi hii.’ Lakini Abrahamu na Sara walikuwa wazee sana na hawakuwa na mtoto. Kwa hiyo Yehova angetimiza ahadi hiyo jinsi gani?

“Kwa imani, Abrahamu . . . alitii kwa kutoka na kwenda mahali ambapo angepokea kuwa urithi; aliondoka, ingawa hakujua mahali alipokuwa akienda.”​—Waebrania 11:8