Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 9

Hatimaye Wapata Mtoto!

Hatimaye Wapata Mtoto!

Abrahamu na Sara walikuwa wameoana kwa miaka mingi. Waliacha nyumba yao nzuri huko Uru na sasa walikuwa wakiishi katika mahema. Lakini Sara hakuwa akilalamika kuhusu hali yao, kwa sababu alimtegemea Yehova.

Sara alitamani sana kupata mtoto hivi kwamba alimwambia Abrahamu hivi: ‘Lala na mjakazi wangu Hagari. Labda ninaweza kupata watoto kutokana naye.’ Baada ya muda, Hagari akajifungua mtoto aliyeitwa Ishmaeli.

Miaka mingi baadaye, Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 99 na Sara alipokuwa na miaka 89, walitembelewa na wageni watatu. Abrahamu aliwakaribisha ili wapumzike chini ya kivuli cha mti na kula chakula. Je, unajua wageni hao walikuwa nani? Walikuwa malaika! Walimwambia Abrahamu hivi: ‘Mwaka ujao wakati kama huu, mtapata mtoto.’ Sara alikuwa akiwasikiliza katika hema lake. Alicheka na kuwaza hivi: ‘Je, kwa kweli ninaweza kuzaa mtoto nikiwa mzee?’

Mwaka uliofuata, Sara alijifungua mtoto wa kiume, kama ambavyo malaika wa Yehova aliahidi. Abrahamu alimwita mtoto huyo Isaka, jina linalomaanisha “Kicheko.”

Isaka alipokuwa na umri wa miaka mitano hivi, Sara alimwona Ishmaeli akimfanyia mzaha Isaka. Kwa kuwa alitaka kumlinda mtoto wake, alienda kwa Abrahamu na kumwomba awafukuze Hagari na Ishmaeli. Mwanzoni, Abrahamu alikataa. Lakini Yehova alimwambia Abrahamu hivi: ‘Msikilize Sara. Nitamlinda Ishmaeli. Lakini nitatimiza ahadi yangu kupitia Isaka.’

“Kwa imani, Sara pia alipokea nguvu za kupata uzao, . .  . kwa kuwa alimwona kuwa mwaminifu Yule aliyekuwa ameahidi.”​—Waebrania 11:11