Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 10

Mkumbuke Mke wa Loti

Mkumbuke Mke wa Loti

Loti aliishi na Abrahamu mjomba wake, katika nchi ya Kanaani. Hatimaye, Abrahamu na Loti wakawa na mifugo mingi na hakukuwa na eneo la kutosha kwa ajili ya wanyama wao. Abrahamu alimwambia Loti: ‘Kwa kuwa nafasi haitoshi kuishi pamoja, tafadhali jitenge nami. Chagua upande utakaopenda kwenda nami nitaenda upande ule mwingine.’ Bila shaka Abrahamu hakuwa mchoyo, sivyo?

Loti aliona sehemu ya nchi iliyo nzuri sana karibu na jiji la Sodoma. Kulikuwa na maji mengi na nyasi mbichi. Kwa hiyo akachagua eneo hilo na kuhamia.

Watu walioishi katika jiji la Sodoma na jiji jirani la Gomora walikuwa wabaya sana. Kwa kweli, walikuwa wabaya sana ndiyo sababu Yehova aliamua kuharibu majiji hayo. Lakini Yehova alitaka kumwokoa Loti na familia yake, kwa hiyo aliwatuma malaika wawili wamwambie Loti hivi: ‘Tokeni haraka mahali hapa, kwa sababu Yehova ataliharibu jiji hili!’

Loti hakuondoka mara moja. Alichelewa. Kwa hiyo malaika walimchukua Loti, mke wake, na binti zake wawili na kuwatoa nje ya jiji, kisha wakawaambia hivi: ‘Kimbieni ili kuokoa uhai wenu! Msitazame nyuma, mkitazama nyuma mtakufa!’

Walipofika katika jiji la Soari, Yehova alinyesha mvua ya moto na kiberiti katika majiji ya Sodoma na Gomora. Majiji hayo mawili yaliharibiwa kabisa. Mke wa Loti hakumtii Yehova, aligeuka nyuma na akawa nguzo ya chumvi! Lakini Loti na binti zake walikuwa salama kwa sababu walimtii Yehova. Walihuzunika sana kwa sababu mke wa Loti hakumtii Yehova. Hata hivyo, walifurahi kwa kuwa walisikiliza maagizo ya Yehova.

“Kumbukeni mke wa Loti.”​—Luka 17:32