Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 11

Jaribu la Imani

Jaribu la Imani

Abrahamu alimfundisha mwana wake Isaka kumpenda Yehova na kutumaini ahadi Zake. Hata hivyo, Isaka alipokuwa na umri wa miaka 25, Yehova alimwambia Abrahamu afanye jambo fulani ambalo lilikuwa gumu sana. Jambo gani?

Mungu alimwambia Abrahamu: ‘Tafadhali, mchukue mwana wako wa pekee na umtoe akiwa dhabihu kwenye mlima katika nchi ya Moria.’ Abrahamu hakujua ni kwa nini Yehova alimwomba afanye jambo hilo. Hata hivyo, alimtii Yehova.

Asubuhi na mapema, Abrahamu, Isaka na watumishi wake wawili walianza safari ya kwenda Moria. Baada ya kusafiri kwa siku tatu, waliiona milima kwa mbali. Abrahamu aliwaambia watumishi wake wabaki, ili yeye na Isaka waende wakatoe dhabihu. Abrahamu alichukua kisu naye Isaka alibeba kuni. Isaka alimuuliza baba yake hivi: ‘Mnyama wa dhabihu yuko wapi?’ Abrahamu akamjibu: ‘Yehova ataandaa.’

Walipofika mlimani walijenga madhabahu. Kisha, Abrahamu akamfunga Isaka mikono na miguu na kumweka juu ya madhabahu.

Abrahamu akainua kisu ili amchinje. Mara moja, malaika wa Yehova akaita kutoka mbinguni akisema: ‘Abrahamu! Usimchinje mwana wako! Sasa ninajua kwamba una imani katika Mungu kwa sababu ulikuwa tayari kumtoa mwana wako kuwa dhabihu.’ Kisha, Abrahamu akamwona kondoo akiwa amejinasa kwenye kichaka. Bila kukawia alimfungua Isaka na kutoa dhabihu ya kondoo.

Kuanzia siku hiyo, Yehova alimwita Abrahamu kuwa rafiki yake. Je, unajua ni kwa nini? Abrahamu alifanya kila kitu ambacho Yehova alimwagiza, hata ingawa nyakati fulani hakuelewa sababu za kufanya hivyo.

Yehova alirudia ahadi yake kwa Abrahamu: ‘Nitakubariki nami nitafanya watoto wako wawe wengi.’ Hilo lilimaanisha kwamba Yehova angewabariki watu wote wema kupitia familia ya Abrahamu.

“Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”​—Yohana 3:16