Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 12

Yakobo Alipewa Urithi

Yakobo Alipewa Urithi

Isaka alikuwa na umri wa miaka 40 alipomwoa Rebeka. Alimpenda sana. Baada ya muda walipata watoto wawili mapacha.

Mtoto wa kwanza aliitwa Esau, na mdogo wake aliitwa Yakobo. Esau alipenda kuwinda, naye alikuwa mwindaji hodari. Lakini, Yakobo alipenda kazi za nyumbani.

Wakati huo, mtoto wa kwanza alipewa vitu vingi vya baba yake, yaani, mali na shamba. Vitu hivyo viliitwa urithi. Katika familia ya Isaka, urithi ulitia ndani kuwa sehemu ya ahadi ambazo Mungu alimwahidi Abrahamu. Esau hakuthamini ahadi hizo, hata hivyo, Yakobo alizithamini sana.

Siku moja, Esau alirudi kutoka mawindoni akiwa amechoka sana. Yakobo alikuwa akipika chakula kizuri, Esau akamwambia: ‘Nina njaa sana! Tafadhali, nipe mchuzi huo!’ Yakobo akamjibu: ‘Nitakupa, lakini niapie kwanza kwamba utanipa urithi wako!’ Esau akamwambia: ‘Urithi hauna maana kwangu! Uchukue. Nipe chakula nile.’ Je, unafikiri Esau alifanya jambo la hekima? Hapana. Esau alimpa Yakobo kitu chenye thamani sana ili apewe mchuzi wa dengu.

Isaka alipozeeka, wakati wa kumbariki mtoto wake wa kwanza ulifika. Hata hivyo, Rebeka alimsaidia Yakobo, mtoto wake wa pili kupata baraka. Esau alipojua jambo hilo, alikasirika sana na akapanga kumuua Yakobo. Isaka na Rebeka walitaka kumlinda Yakobo, hivyo wakamwambia hivi: ‘Ondoka, nenda ukaishi na Labani, mjomba wako, mpaka ghadhabu ya Esau itulie.’ Yakobo alisikiliza ushauri wa wazazi wake, naye akakimbia ili aokoe uhai wake.

“Mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu mzima kisha apoteze uhai wake? Kwa kweli, mtu anaweza kutoa nini ili abadilishane na uhai wake?”​—Marko 8:36, 37