Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 13

Yakobo na Esau Wafanya Amani

Yakobo na Esau Wafanya Amani

Yehova alimwahidi Yakobo kwamba atamlinda kama alivyofanya kwa Abrahamu na Isaka. Yakobo aliishi katika eneo lililoitwa Harani. Alioa, akapata watoto na kuwa tajiri sana.

Baadaye, Yehova alimwambia Yakobo hivi: ‘Rudi katika nchi ya baba zako.’ Hivyo, Yakobo na familia yake walianza safari ndefu ya kurudi Kanaani. Wakiwa njiani, watu fulani walimjia Yakobo na kumwambia: ‘Ndugu yako Esau yuko njiani anakuja, yuko pamoja na wanaume 400!’ Yakobo aliogopa kwamba huenda Esau angemshambulia yeye na familia yake. Alisali hivi kwa Yehova: ‘ Tafadhali nilinde dhidi ya ndugu yangu.’ Siku iliyofuata, Yakobo alituma zawadi nyingi kwa Esau, yaani, kondoo, mbuzi, ng’ombe, ngamia na punda.

Usiku huo, Yakobo alipokuwa peke yake alimwona malaika! Malaika alianza kupigana naye. Walipigana mweleka hadi asubuhi. Ingawa Yakobo aliumizwa, hakuacha kupigana. Kisha malaika akamwambia: ‘Niache niende.’ Lakini Yakobo akamjibu: ‘Sitakuacha mpaka unibariki.’

Mwishowe malaika akambariki Yakobo. Sasa Yakobo alijua kwamba Yehova atamlinda ili Esau asimshambulie.

Asubuhi, Yakobo alimwona kwa mbali Esau akija na wanaume 400. Yakobo alimkaribia Esau ndugu yake na kuinama chini mara saba. Esau alimkimbilia Yakobo na kumkumbatia. Wakalia pamoja na kufanya amani. Unafikiri Yehova alihisije Yakobo alipofanya amani na ndugu yake?

Baadaye, Esau alirudi kwake, na Yakobo akaendelea na safari. Yakobo alikuwa na watoto wa kiume 12. Watoto hao ni Rubeni, Simeoni, Lawi, Yuda, Dani, Naftali, Gadi, Asheri, Isakari, Zabuloni, Yosefu, na Benyamini. Mmoja wa watoto hao, yaani, Yosefu, alitumiwa na Mungu kuwakomboa watu wake. Je, unajua alifanya hivyo jinsi gani? Acha tuone.

“Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.”​—Mathayo 5:44, 45