Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 14

Mtumwa Aliyemtii Mungu

Mtumwa Aliyemtii Mungu

Yosefu alikuwa mmoja wa wana wa mwisho wa Yakobo. Kaka zake waliona kuwa Yosefu ndiye aliyependwa zaidi na baba yao. Unafikiri jambo hilo lilifanya wahisije? Walianza kumwonea Yosefu wivu na kumchukia. Yosefu alipopata ndoto zisizo za kawaida, aliwaambia kuhusu ndoto hizo. Kaka zake walifikiri zinamaanisha kwamba siku moja wangemwinamia. Sasa walimchukia hata zaidi!

Siku moja, kaka za Yosefu walikuwa wakichunga kondoo karibu na jiji la Shekemu. Yakobo alimtuma Yosefu akaone wanaendeleaje. Kwa mbali walimwona Yosefu akija, nao wakaambiana hivi: ‘Yule mwota-ndoto anakuja. Basi na tumuue!’ Hivyo, wakamchukua na kumtupa ndani ya shimo refu. Lakini Yuda, mmoja wa kaka zake, akasema hivi: ‘Msimuue! Badala yake, tumuuze akawe mtumwa.’ Kwa hiyo, wakamuuza Yosefu kwa wanabiashara Wamidiani waliokuwa wakielekea Misri kwa vipande 20 vya fedha.

Kisha, kaka za Yosefu wakachovya vazi lake ndani ya damu ya mbuzi, wakalipeleka kwa baba yao na kusema: ‘Je, hili si vazi la mwanao?’ Hivyo, Yakobo akafikiri kwamba mnyama-mwitu alikuwa amemwua Yosefu. Yakobo alivunjika moyo sana. Hakuna mtu aliyeweza kumfariji.

Alipofika Misri, Yosefu aliuzwa akiwa mtumwa kwa ofisa mwenye cheo cha juu aliyeitwa Potifa. Lakini Yehova alikuwa pamoja na Yosefu. Potifa aliona kwamba Yosefu alifanya kazi vizuri na angeweza kumtumaini. Baada ya muda mfupi, Potifa akamweka juu ya mali zake zote.

Mke wa Potifa akatambua kwamba Yosefu alikuwa na sura ya kupendeza na mwenye umbo zuri. Siku baada siku alikuwa akimwambia Yosefu alale naye. Yosefu angefanya nini? Alikataa na kusema: ‘Hapana! Ni kosa kufanya hivyo. Bwana wangu ananitumaini, na wewe ni mke wake. Nikilala nawe, nitamtendea Mungu dhambi!’

Siku moja, mke wa Potifa alijaribu kumlazimisha Yosefu alale naye. Akashika vazi lake, lakini Yosefu akakimbia. Potifa aliporudi nyumbani, mke wake alimwambia kwamba Yosefu alimshambulia. Alikuwa akisema uwongo. Potifa alikasirika sana na kumfunga Yosefu gerezani. Lakini Yehova hakumsahau Yosefu.

“Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue kwa wakati unaofaa.”​—1 Petro 5:6