Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 16

Ayubu Alikuwa Nani?

Ayubu Alikuwa Nani?

Katika nchi ya Usi, kulikuwa na mtu aliyemwabudu Yehova. Aliitwa Ayubu. Alikuwa tajiri sana na alikuwa na familia kubwa. Alikuwa mwenye fadhili, aliwasaidia maskini, wanawake ambao waume zao walikuwa wamekufa, na watoto ambao hawakuwa na wazazi. Lakini, je, hilo lilimaanisha kwamba hangepatwa na matatizo yoyote kwa sababu alifanya mambo mazuri?

Ayubu hakujua kwamba Shetani Ibilisi alikuwa akimchunguza. Yehova alimwambia hivi Shetani: ‘Je, umemwona mtumishi wangu Ayubu? Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani. Ananisikiliza na kufanya mambo mazuri.’ Shetani akamjibu hivi: ‘Ni kweli kwamba Ayubu anakutii. Unamlinda na kumbariki. Umempa mali na mifugo. Ukichukua vitu hivyo vyote, ataacha kukuabudu.’ Yehova akasema hivi: ‘Unaweza kumjaribu Ayubu. Lakini usimwue.’ Kwa nini Yehova alimruhusu Shetani amjaribu Ayubu? Alikuwa na uhakika kwamba Ayubu angeendelea kuwa mwaminifu.

Shetani alianza kumjaribu Ayubu kwa kumletea misiba mbalimbali. Kwanza, aliwatuma watu fulani walioitwa Wasabea waibe ng’ombe na punda za Ayubu. Kisha, moto ukawateketeza kondoo wote wa Ayubu. Watu wengine walioitwa Wakaldayo, wakaiba ngamia zake. Watumishi waliokuwa wakitunza mifugo hiyo, wakauawa. Kisha Ayubu akapata habari za msiba mbaya zaidi. Watoto wote wa Ayubu walikufa walipoangukiwa na nyumba waliyokuwa wakifanyia sherehe. Ayubu alivunjika moyo, lakini hakuacha kumwabudu Yehova.

Shetani alitaka Ayubu ateseke hata zaidi, kwa hiyo, akamletea Ayubu majipu kwenye mwili mzima. Ayubu alikuwa na maumivu makali sana. Ayubu hakujua kwa nini alikuwa akipatwa na mambo yote hayo. Hata hivyo, bado Ayubu aliendelea kumwabudu Yehova. Mungu aliona jinsi Ayubu alivyotenda na akafurahi sana.

Kisha Shetani akatuma watu watatu waende kumjaribu Ayubu. Walimwambia hivi: ‘Lazima uwe umefanya dhambi na unajaribu kuificha. Sasa Mungu anakuadhibu.’ Ayubu alisema hivi: ‘Sijafanya kosa lolote.’ Lakini akaanza kufikiri kwamba Yehova ndiye aliyemletea matatizo hayo, na akasema kwamba Mungu hakuwa akimtendea kwa haki.

Kijana mmoja aliyeitwa Elihu alikuwa akisikiliza mazungumzo hayo kimyakimya. Kisha akasema hivi: ‘Mambo yote mliyosema si ya kweli. Yehova ni mkuu kuliko tunavyoweza kufikiri. Hawezi kamwe kufanya mambo maovu. Anaona kila jambo, naye huwasaidia watu wanapokuwa na matatizo.’

Kisha Yehova akazungumza na Ayubu na kumwambia hivi: ‘Ulikuwa wapi nilipokuwa nikiumba mbingu na dunia? Kwa nini unasema kwamba sitendi kwa haki? Unazungumza, lakini hujui kwa nini mambo fulani hutukia.’ Ayubu alisema hivi: ‘Nilikosea. Nilisikia habari zako, lakini sasa nimekujua. Hakuna jambo lolote linaloweza kukushinda. Ninaomba msamaha.’

Majaribu yake yalipoisha, Yehova alimponya Ayubu na kumpa mali nyingi kuliko zile alizokuwa nazo mwanzoni. Ayubu aliishi kwa miaka mingi akiwa mwenye furaha. Yehova alimbariki Ayubu kwa sababu ya kumtii hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. Je, utamwiga Ayubu kwa kuendelea kumwabudu Yehova hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo?

“Mmesikia kuhusu uvumilivu wa Ayubu na mmeona matokeo ambayo Yehova alileta.”​—Yakobo 5:11