Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 17

Musa Aliamua Kumwabudu Yehova

Musa Aliamua Kumwabudu Yehova

Katika nchi ya Misri, watu wa familia ya Yakobo walikuja kuitwa Waisraeli. Baada ya Yakobo na Yosefu kufa, Farao mwingine alianza kutawala. Aliogopa kwamba Waisraeli wangekuwa wengi na hivyo kuwa na nguvu kuliko Wamisri. Kwa hiyo, Farao huyo aliwafanya Waisraeli kuwa watumwa. Aliwalazimisha kutengeneza matofali na kufanya kazi ngumu kwenye mashamba. Lakini kadiri Wamisri walivyowalazimisha wafanye kazi ngumu, ndivyo walivyozidi kuongezeka. Kwa kuwa Farao hakufurahia jambo hilo, aliagiza wavulana wote Waisraeli wauawe mara tu wanapozaliwa. Je, unaweza kuwazia jinsi Waisraeli walivyoogopa?

Mwanamke Mwisraeli aliyeitwa Yokebedi, alijifungua mtoto wa kiume mwenye sura nzuri. Kwa sababu alitaka kumwokoa, aliamua kumweka ndani ya kikapu, na kumficha kwenye matete yaliyo kandokando ya Mto Nile. Miriamu, dada ya mtoto huyo, alikaa karibu ili aone kitakachotokea.

Binti ya Farao alienda kuoga mtoni na akaona kikapu hicho. Ndani ya kikapu hicho, aliona mtoto akilia, naye akamsikitikia. Miriamu akamwuliza: ‘Ungependa nikutafutie mwanamke atakayemnyonyesha mtoto huyu kwa niaba yako?’ Binti ya Farao alipokubali, Miriamu akamleta Yokebedi, mama yake. Binti ya Farao akamwambia hivi: ‘Mchukue mtoto huyu uninyonyeshee, halafu nitakulipa.’

Mtoto alipokuwa mkubwa, Yokebedi akamleta kwa binti ya Farao, naye akamwita Musa na kumlea kama mtoto wake. Musa alilelewa kama mtoto wa mfalme na angeweza kupata chochote alichotaka. Lakini Musa hakumsahau Yehova. Alijua kwamba yeye alikuwa Mwisraeli, si Mmisri. Na aliamua kumtumikia Yehova.

Alipokuwa na umri wa miaka 40, Musa aliamua kuwasaidia Waisraeli wenzake. Alipomwona Mmisri akimpiga mtumwa Mwisraeli, Musa alimpiga Mmisri huyo na kumuua. Halafu akamficha ndani ya mchanga. Farao alipogundua jambo hilo, alijaribu kumuua Musa. Lakini Musa akakimbilia nchi ya Midiani. Yehova alimtunza alipokuwa huko.

“Kwa imani, Musa  . . . alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, akachagua kuteswa pamoja na watu wa Mungu.”​—Waebrania 11:24, 25