Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 19

Mapigo Matatu ya Kwanza

Mapigo Matatu ya Kwanza

Waisraeli walilazimishwa kufanya kazi ngumu wakiwa watumwa. Yehova alimtuma Musa na Haruni wamwambie hivi Farao: ‘Waruhusu watu wangu waondoke ili wakaniabudu huko nyikani.’ Kwa kiburi, Farao akasema hivi: ‘Mimi sijali Yehova anasema nini, na sitawaruhusu Waisraeli waondoke.’ Kisha Farao akawalazimisha wafanye kazi ngumu hata zaidi. Yehova angemfundisha Farao somo. Unajua alifanya nini? Alileta Mapigo Kumi juu ya Misri. Yehova alimwambia hivi Musa: ‘Farao amekataa kunisikiliza. Kesho asubuhi atakuwa kwenye Mto Nile. Nenda ukamwambie, kwa kuwa amekataa kuwaruhusu watu wangu waondoke, maji yote ya Mto Nile yatageuka kuwa damu.’ Musa alitii na akaenda kwa Farao. Farao aliona Haruni akiyapiga maji ya Mto Nile kwa fimbo yake, nayo yakageuka kuwa damu. Samaki wakafa, mto ukaanza kunuka, na hakukuwa na maji safi ya kunywa kutoka kwenye Mto Nile. Lakini bado Farao alikataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke.

Baada ya siku saba, Yehova alimtuma tena Musa kwa Farao akamwambie hivi: ‘Usipowaruhusu watu wangu waondoke, vyura watajaa katika nchi yote ya Misri.’ Haruni akainua fimbo yake na vyura wakaanza kuijaza nchi. Kulikuwa vyura katika nyumba za watu, vitandani, na kwenye vyombo. Vyura walikuwa kila mahali! Farao alimwambia Musa amwombe Yehova akomeshe pigo hilo. Akaahidi kwamba angewaruhusu Waisraeli waende. Kisha Yehova akakomesha pigo hilo, na Wamisri wakawakusanya vyura hao mafungu-mafungu. Nayo nchi ikaanza kunuka. Lakini kwa mara nyingine tena Farao hakuwaruhusu Waisraeli waondoke.

Baada ya hapo, Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Mwambie Haruni apige mavumbi ya dunia kwa fimbo yake, nayo yatakuwa chawa, au wadudu wadogo wanaouma.’ Papo hapo, chawa wakajaa kila mahali. Baadhi ya watu wa Farao walimwambia hivi: ‘Pigo hili limetoka kwa Mungu.’ Lakini bado Farao hakuwaruhusu Waisraeli waondoke.

“Nitawafanya wajue nguvu zangu na uwezo wangu, nao watajua kwamba jina langu ni Yehova.”​—Yeremia 16:21