Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 23

Waisraeli Wamtolea Yehova Ahadi

Waisraeli Wamtolea Yehova Ahadi

Miezi miwili hivi baada ya Waisraeli kutoka Misri, walifika kwenye Mlima Sinai na kupiga kambi. Yehova akamwita Musa, naye akapanda juu mlimani, kisha Yehova akamwambia hivi: ‘Mimi niliwaokoa Waisraeli. Ikiwa watanitii na kushika sheria zangu, watakuwa watu wangu wa pekee.’ Musa akashuka kutoka mlimani na kuwaambia Waisraeli maneno ambayo Yehova alikuwa amesema. Walimjibuje? Walisema hivi: ‘Tutafanya kila kitu ambacho Yehova anatuambia tufanye.’

Musa akapanda tena juu mlimani. Akiwa huko, Yehova akamwambia: ‘Baada ya siku tatu, nitazungumza nanyi. Waonye watu wasijaribu kupanda juu kwenye Mlima Sinai.’ Musa akateremka kutoka mlimani na kuwaambia Waisraeli wajitayarishe kusikiliza kile ambacho Yehova atasema.

Siku tatu baadaye, Waisraeli waliona umeme na wingu zito kwenye mlima. Pia, walisikia sauti kubwa sana ya mingurumo na pembe. Kisha Yehova akashuka kwenye mlima katika moto. Waisraeli wakaogopa sana na kutetemeka. Mlima wote ulitetemeka sana na ulifunikwa kwa moshi. Sauti ya pembe ikazidi kuwa kubwa. Kisha Mungu akasema: ‘Mimi ni Yehova. Msiabudu miungu mingine.’

Musa akapanda tena juu mlimani, na Yehova akampa sheria ambazo zilionyesha jinsi watu walivyopaswa kumwabudu na jinsi walivyopaswa kujiendesha. Musa akaandika sheria hizo kisha akawasomea Waisraeli. Wakaahidi hivi: ‘Tutafanya mambo yote ambayo Yehova ametuambia tufanye.’ Naam, Waisraeli walikuwa wamemtolea Mungu ahadi. Je, wangeitimiza?

“Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.”​—Mathayo 22:37