Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 26

Wale Wapelelezi Kumi na Wawili

Wale Wapelelezi Kumi na Wawili

Waisraeli waliondoka Mlima Sinai na kusafiri kwenye nyika ya Parani hadi eneo linaloitwa Kadeshi. Wakiwa huko, Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Tuma watu 12, mmoja kutoka kila kabila, wakaipeleleze nchi ya Kanaani, nchi nitakayowapa Waisraeli.’ Kwa hiyo, Musa akachagua watu 12 na kuwaambia hivi: ‘Nendeni kwenye nchi ya Kanaani mkachunguze kama inafaa kwa ajili ya kupanda chakula. Angalieni kama watu wa nchi hiyo ni dhaifu au wana nguvu na kama wanaishi katika mahema au majiji.’ Wapelelezi hao 12, kutia ndani Yoshua na Kalebu, wakaenda Kanaani.

Baada ya siku 40, wapelelezi hao wakarudi, wakiwa na tini, makomamanga, na zabibu. Wapelelezi hao wakasema hivi: ‘Ni nchi nzuri, lakini watu wanaokaa katika nchi hiyo ni wenye nguvu na majiji yake yana kuta ndefu sana.’ Naye Kalebu akasema hivi: ‘Tunaweza kuwashinda. Twendeni mara moja!’ Je, unajua kwa nini Kalebu alisema hivyo? Ni kwa sababu yeye na Yoshua walimtegemea Yehova. Lakini wale wapelelezi wengine kumi wakasema: ‘Hapana! Watu hao ni wakubwa sana, kama majitu! Sisi tulikuwa kama panzi tulipojilinganisha nao.’

Waisraeli walivunjika moyo. Wakaanza kulalamika na kuambiana hivi: ‘Tuchague kiongozi mwingine ili turudi Misri. Kwa nini twende kwenye nchi hiyo halafu tuuawe?’ Yoshua na Kalebu wakasema hivi: ‘Msimwasi Yehova, wala msiogope. Yehova atatulinda.’ Lakini Waisraeli hawakusikiliza. Hata walitaka kuwaua Yoshua na Kalebu!

Yehova alifanya nini? Alimwambia Musa hivi: ‘Ingawa nimewafanyia Waisraeli mambo mengi, bado hawanitii. Kwa sababu hiyo watakaa katika nyika hii kwa miaka 40, nao watakufa hapa. Watoto wao, Yoshua, na Kalebu ndio tu watakaoishi katika nchi niliyoahidi kuwapa.’

“Kwa nini mnaogopa, ninyi wenye imani ndogo?”​—Mathayo 8:26