Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 27

Walimwasi Yehova

Walimwasi Yehova

Muda fulani baadaye Waisraeli walipokuwa bado nyikani, Kora, Dathani, Abiramu, na watu wengine 250 walimwasi Musa. Walimwambia hivi: ‘Imetosha! Kwa nini wewe uwe kiongozi wetu na Haruni awe kuhani mkuu? Yehova yuko katikati yetu sisi sote, hayuko kati ya wewe na Haruni peke yake.’ Jambo hilo halikumfurahisha Yehova. Aliona kwamba walikuwa wakimwasi yeye!

Musa akamwambia Kora na watu waliokuwa wakimuunga mkono hivi: ‘Kesho njooni kwenye maskani, na mje na vyetezo vilivyojaa uvumba. Yehova atatuonyesha amemchagua nani.’

Siku iliyofuata, Kora na wale wanaume 250 wakaenda kukutana na Musa kwenye maskani. Wakafukiza uvumba kana kwamba wao walikuwa makuhani. Yehova akamwambia Musa na Haruni: ‘Jitengeni na Kora na wanaume hawa.’

Ingawa Kora alikuwa ameenda kukutana na Musa kwenye maskani, Dathani, Abiramu, na familia zao walikataa kwenda. Yehova akawaambia Waisraeli wajitenge na mahema ya Kora, Dathani, na Abiramu. Mara moja, Waisraeli wakajitenga nao. Dathani, Abiramu, na familia zao wakasimama nje ya mahema yao. Ghafla nchi ikapasuka na kuwameza! Kwenye maskani, moto ukashuka na kumteketeza Kora na wale wanaume 250 waliokuwa pamoja naye.

Kisha Yehova akamwambia Musa hivi: ‘Chukua fimbo moja kutoka kwa kiongozi wa kila kabila, na uandike jina lake juu ya fimbo hiyo. Lakini kwenye fimbo ya kabila la Lawi, uandike jina la Haruni. Uziweke ndani ya maskani, na fimbo ya mtu nitakayemchagua itachipuka maua.’

Siku iliyofuata Musa akatoa nje fimbo zote na kuwaonyesha viongozi. Fimbo ya Haruni ilikuwa na maua yanayomea na lozi zilizoiva. Kwa njia hiyo, Yehova akathibitisha kwamba alikuwa amemchagua Haruni kuwa kuhani mkuu.

“Watiini wale wanaoongoza kati yenu na mnyenyekee.”​—Waebrania 13:17