Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 29

Yehova Amchagua Yoshua

Yehova Amchagua Yoshua

Baada ya kuongoza taifa la Israeli kwa miaka mingi, Musa alikuwa anakaribia kufa. Yehova akamwambia hivi: ‘Si wewe utakayewaingiza Waisraeli kwenye Nchi ya Ahadi. Lakini nitakuruhusu uione nchi hiyo.’ Kisha Musa akamwomba Yehova achague kiongozi mpya wa kuwaongoza watu. Yehova akamwambia hivi: ‘Nenda kwa Yoshua umwambie yeye ndiye atakayekuwa kiongozi.’

Musa akaliambia taifa lote kwamba karibuni atakufa na kwamba Yehova amemchagua Yoshua awe kiongozi wa kuwaingiza katika Nchi ya Ahadi. Kisha Musa akamwambia Yoshua hivi: ‘Usiogope. Yehova atakusaidia.’ Muda mfupi baada ya hapo, Musa akapanda kwenda juu ya Mlima Nebo, na akiwa huko Yehova akamwonyesha nchi ambayo Yeye alikuwa ameahidi kuwapa Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Musa alikuwa na umri wa miaka 120 alipokufa.

Yehova akamwambia Yoshua hivi: ‘Vuka Mto Yordani, na uingie Kanaani. Nitakusadia kama tu nilivyomsaidia Musa. Hakikisha kwamba unasoma Sheria yangu kila siku. Usiogope. Uwe hodari. Nenda, na ufanye yote ambayo nimekuamuru.’

Yoshua akatuma wapelelezi wawili waende katika jiji la Yeriko. Katika hadithi inayofuata, tutaona ni nini kilichotukia huko. Waliporudi, walisema kwamba ulikuwa wakati unaofaa kuingia Kanaani. Siku iliyofuata, Yoshua akaliambia taifa lote livunje kambi. Kisha akawaambia makuhani waliokuwa wakibeba sanduku la agano watangulie kuingia katika Mto Yordani. Mto ulikuwa umefurika. Lakini mara tu miguu ya makuhani ilipokanyaga maji, mto ukaacha kutiririka, na maji yakaisha! Makuhani wakatembea mpaka katikati ya mto na kusimama hapo hadi taifa lote la Israeli lilipovuka upande ule mwingine. Unafikiri kwamba muujiza huo uliwakumbusha kile ambacho Yehova alikuwa amefanya kwenye Bahari Nyekundu?

Mwishowe, baada ya miaka hiyo yote, Waisraeli walikuwa wameingia katika Nchi ya Ahadi. Wangeweza kujenga nyumba na majiji. Wangeweza kupanda mashamba ya chakula, ya mizabibu, na ya matunda. Nchi hiyo ilikuwa ikitiririka maziwa na asali.

“Yehova atakuongoza sikuzote na kukushibisha hata katika nchi iliyokauka.”​—Isaya 58:11