Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 31

Yoshua na Wagibeoni

Yoshua na Wagibeoni

Habari kuhusu kuanguka kwa Yeriko zilienea katika mataifa mengine ya Kanaani. Wafalme wao wakaamua kuungana ili wapigane na Waisraeli. Lakini Wagibeoni wakaamua kufanya jambo tofauti. Wakiwa wamevalia mavazi yaliyochakaa wakamwendea Yoshua na kusema hivi: ‘Tumetoka nchi ya mbali sana. Tumesikia kumhusu Yehova na yote aliyowafanyia mlipokuwa Misri na Moabu. Tuahidini kwamba hamtatushambulia, nasi tutakuwa watumishi wenu.’

Yoshua aliwaamini na akaahidi hatawashambulia. Siku tatu baadaye, akagundua kwamba hawakuwa wametoka nchi ya mbali. Walikuwa wakaaji wa nchi ya Kanaani. Yoshua akawauliza Wagibeoni hivi: ‘Kwa nini mlitudanganya?’ Wakamjibu: ‘Tuliogopa! Tunajua kwamba Yehova Mungu wenu anawapigania. Tafadhali msituue.’ Yoshua akatimiza ahadi yake na kuwaacha waendelee kuishi.

Baada ya muda mfupi, wafalme watano Wakanaani na majeshi yao wakatisha kuwashambulia Wagibeoni. Yoshua na jeshi lake wakapiga mwendo usiku mzima ili kuwaokoa Wagibeoni. Vita vikaanza mapema asubuhi siku iliyofuata. Wakanaani wakaanza kukimbia kuelekea pande zote. Kila mahali walipokimbilia Yehova aliangusha mawe makubwa sana ya mvua juu yao. Kisha Yoshua akamwomba Yehova alifanye jua lisimame tuli. Kwa nini Yoshua amwombe Yehova afanye hivyo wakati ambapo jua halikuwa limewahi kusimama tuli kabla ya hapo? Kwa sababu Yoshua alimwamini Yehova. Jua halikutua kwa siku nzima hadi Waisraeli walipowashinda wafalme Wakanaani na majeshi yao.

“‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo, kwa maana linalozidi hayo linatoka kwa yule mwovu.”​—Mathayo 5:37