Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 33

Ruthu na Naomi

Ruthu na Naomi

Kulipokuwa na ukame nchini Israeli, mwanamke Mwisraeli aliyeitwa Naomi alihamia Moabu akiwa pamoja na mume wake na wanawe wawili. Baadaye, mume wa Naomi alikufa. Mwana wake mmoja alimwoa Ruthu na mwingine alimwoa Orpa, wanawake Wamoabu. Kwa kusikitisha, baada ya muda wana wa Naomi walikufa.

Naomi alipopata habari kwamba ukame umeisha nchini Israeli, aliamua kurudi nyumbani. Ruthu na Orpa waliandamana naye, hata hivyo, walipokuwa njiani, Naomi aliwaambia hivi: ‘Mlikuwa wake wazuri kwa wanangu na pia binti wakwe wazuri. Ningependa muolewe tena. Rudini Moabu.’ Wanawake hao wakamwambia, ‘Tunakupenda sana! Hatutaki kukuacha.’ Naomi akaendelea kuwasihi warudi. Mwishowe, Orpa akarudi, lakini Ruthu akabaki. Naomi akamwambia: ‘Orpa anarudi kwa watu wake na kwa miungu yake. Rudi pamoja naye, urudi nyumbani kwa mama yako.’ Hata hivyo, Ruthu akamwambia: ‘Sitakuacha. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu.’ Unafikiri Naomi alihisije Ruthu alipomwambia maneno hayo?

Ruthu na Naomi walifika Israeli mwanzoni mwa mavuno ya shayiri. Siku moja, Ruthu alienda kuokota masalio katika shamba la mwanamume aliyeitwa Boazi, mwana wa Rahabu. Boazi alisikia habari kwamba Ruthu alikuwa Mmoabu ambaye alishikamana kabisa na Naomi. Akawaamuru wafanyakazi wake waache baadhi ya masuke ili Ruthu ayaokote.

Jioni hiyo, Naomi akamuuliza Ruthu hivi: ‘Leo ulifanya kazi kwenye shamba la nani?’ Ruthu akamjibu: ‘Katika shamba la Boazi.’ Naomi akamwambia: ‘Boazi ni mtu wa ukoo wetu. Endelea kufanya kazi katika shamba lake pamoja na wanawake wengine. Huko utakuwa salama.’

Ruthu aliendelea kufanya kazi katika shamba la Boazi hadi mavuno yalipoisha. Boazi aligundua kwamba Ruthu ni mwanamke mwema na mwenye bidii. Nyakati hizo, ikiwa mwanamume angekufa bila kuwa na watoto, ndugu yake angemwoa mjane aliyebaki. Hivyo, Boazi alimwoa Ruthu. Wakapata mwana aliyeitwa Obedi, ambaye alikuja kuwa babu ya Mfalme Daudi. Marafiki wa Naomi walifurahi sana. Walimwambia hivi: ‘Yehova alikupatia Ruthu ambaye anakupenda sana, na sasa una mjukuu. Yehova na asifiwe.’

“Kuna rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu kuliko ndugu.”​—Methali 18:24