Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 34

Gideoni Aliwashinda Wamidiani

Gideoni Aliwashinda Wamidiani

Baada ya muda, Waisraeli walimwacha tena Yehova na kuanza kuabudu miungu ya uwongo. Kwa miaka saba, Wamidiani waliiba mifugo na kuharibu mazao ya Waisraeli. Kwa hiyo, ili kuwatoroka Wamidiani, Waisraeli walijificha kwenye mapango na milima. Wakamwomba Yehova awasaidie. Hivyo, Yehova alimtuma malaika kwa mwanamume aliyeitwa Gideoni. Malaika akamwambia hivi: ‘Yehova amekuchagua wewe kuwa shujaa mwenye nguvu.’ Gideoni akamuuliza: ‘Ninawezaje kuwaokoa Waisraeli? Sina uwezo wowote.’

Ni nini ambacho kingemthibitishia Gideoni kwamba kweli Yehova alikuwa amemchagua? Gideoni alichukua manyoya ya kondoo na kuyaweka chini, kisha, akamwambia hivi Yehova: ‘Kesho asubuhi nikikuta umande kwenye manyoya lakini eneo lingine liwe kavu, nitajua kwamba umenichagua niwaokoe Waisraeli.’ Kesho yake, manyoya yalikuwa yamelowa lakini eneo lingine lilikuwa kavu! Kisha, Gideoni akaomba kwamba asubuhi inayofuata, Yehova afanye eneo liwe na umande lakini manyoya yawe makavu. Sala hiyo ilipojibiwa, Gideoni akaamini kabisa kwamba Yehova alikuwa amemchagua. Akakusanya askari wake ili kwenda kupigana na Wamidiani.

Yehova akamwambia hivi Gideoni: ‘Nitawapa Waisraeli ushindi. Lakini kwa kuwa una askari wengi, unaweza kufikiri kwamba mmeshinda kwa nguvu zenu wenyewe. Waambie kwamba ikiwa kuna mtu yeyote anayeogopa, na arudi nyumbani.’ Kwa hiyo, askari 22,000 wakarudi nyumbani, wakabaki askari 10,000. Kisha, Yehova akasema: ‘Bado una askari wengi mno. Wapeleke kwenye kijito na uwaambie wanywe maji. Baki na wale tu watakaokunywa maji huku wakiangalia maadui.’ Ni wanaume 300 tu waliokuwa macho wakati wanakunywa maji. Yehova aliahidi kwamba wanaume hao wachache watalishinda jeshi la Midiani lenye askari 135,000.

Usiku huo, Yehova alimwambia Gideoni hivi: ‘Huu ndio wakati wa kuwashambulia Wamidiani!’ Gideoni aliwapa watu wake baragumu na mitungi mikubwa iliyokuwa na mienge ndani yake. Akawaambia hivi: ‘Nitazameni na mfanye kama ninavyofanya.’ Kisha, Gideoni akapiga baragumu, akavunja mtungi, akanyoosha mwenge wake, na kusema: ‘Upanga wa Yehova na wa Gideoni!’ Wanaume wake 300 wakafanya vivyo hivyo. Wamidiani waliogopa na kukimbia ovyoovyo. Kukawa na vurugu, nao wakaanza kushambuliana wenyewe kwa wenyewe. Kwa mara nyingine tena, Yehova aliwasaidia Waisraeli kuwashinda maadui zao.

“Ili nguvu zinazopita zile za kawaida ziwe za Mungu na si kutoka kwetu.”​—2 Wakorintho 4:7